● Ni katika Hafla ya Usiku wa Wanawake wa Mahakama-Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani
● Jaji Masabo awahimiza pia kujiendeleza kimasomo
Na HALIMA MNETE &
HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma
Wanawake watumishi wa
Mahakama ya Tanzania wamehimizwa kuendelea kuzingatia uadilifu, weledi na
uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao sambamba na kuendeleza juhudi za
kukuza usawa wa kijinsia katika Mhimili huo.
Wito huo umetolewa na Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe.Dkt. Juliana Masabo
ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla ya Watumishi wanawake wa Mahakama ya Maadhimisho
ya Siku ya Wanawake Duniani iliyofanyika tarehe 08 Machi 2026 kwenye Ukumbi wa
Cathedral jijini Dodoma, jijini Dodoma.
Akizungumza wakati wa
kufungua hafla hiyo, Mhe. Dkt. Masabo aliwashukuru wanawake wote waliojitokeza
kushiriki maadhimisho hayo, huku akibainisha kuwa, ushiriki wao unaonesha
dhamira ya dhati ya wanawake wa Mahakama katika kuimarisha mchango wao katika
utoaji wa haki kwa jamii.
Alisema Maadhimisho ya
Siku ya Wanawake Duniani, ambayo yalianza kuadhimishwa mwaka 1911, yanalenga
kuikumbusha jamii kuhusu nafasi, haki na mchango wa mwanamke katika maendeleo
ya jamii.
Kwa mujibu wa takwimu
zilizotolewa na Jaji Masabo, kuna jumla ya watumishi wanawake 342 katika Makao
Makuu ya Mahakama, Mahakama ya Rufani, Masjala Kuu, Divisheni za Mahakama Kuu
pamoja na Mahakama Kuu Dodoma (IJC) wanaofanya kazi katika nafasi mbalimbali
ikiwemo Majaji, Naibu Wasajili, Wakurugenzi, Mahakimu, Wasaidizi wa Sheria wa
Majaji, Wakuu wa Vitengo pamoja na kada nyingine za utumishi.
Aidha, ilielezwa kuwa,
katika Mhimili wa Mahakama kuna maendeleo yanayoonekana katika usawa wa
kijinsia kwenye nafasi za uongozi ambapo takwimu zinaonesha, kwamba kati ya
Majaji 39 wa Mahakama ya Rufani, Wanawake ni 13 sawa na asilimia 33, huku
katika Majaji 104 wa Mahakama Kuu wanawake wakiwa 40 sawa na asilimia 38.
Kadhalika, kati ya Naibu
Wasajili 82 waliopo wanawake ni 42 sawa na asilimia 51, jambo linaloonesha
ongezeko la ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi ndani ya Mhimili huo.
Katika hafla hiyo, Watumishi
wanawake wa Mahakama walipongezwa pia kwa kushiriki matendo ya huruma kwa
kutembelea watoto wenye mahitaji maalum katika Hospitali ya Benjamin Mkapa
jijini Dodoma, ambapo walitoa msaada wa mahitaji mbalimbali pamoja na
kugharamia matibabu ya mtoto mchanga aliyekuwa katika chumba cha wagonjwa
mahututi (ICU).
Akizungumzia, Maadhimisho
ya mwaka huu, Mhe. Dkt. Masabo alisema Kaulimbiu ya mwaka 2026 inayosema, “Haki
na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi Kufikia Dira 2050” inapaswa
kuwa chachu kwa wanawake kujitathmini namna wanavyotekeleza wajibu wao katika
kuhakikisha haki na usawa vinazingatiwa katika utoaji wa huduma za haki.
Aidha, Jaji Mfawidhi huyo
aliwahimiza wanawake kuendelea kupendana, kusaidiana na kuinuana ili kuwa
daraja la mafanikio kwa wanawake wengine, huku akitoa wito kwa Menejimenti ya
Mahakama kuendelea kuwaamini na kuwapa fursa zaidi za uongozi na maendeleo ya
kitaaluma.
Aidha, kupitia
maadhimisho hayo washiriki walipata fursa ya kupata ushauri kutoka kwa Mkufunzi
katika Masuala ya Afya ya Akili kutoka Hospitali ya Taifa-Muhimbili, Dkt. Garvin Kweka kuhusu umuhimu wa
usawazishaji wa majukumu ya kazi na familia (work-life balance), elimu
inayolenga kuwasaidia wanawake kuboresha afya ya akili, kuimarisha utendaji
kazi kazini pamoja na kuendeleza ustawi wa familia.
Watumishi wanawake walioshiriki katika sherehe hiyo ni kutoka Makao Makuu ya Mahakama, Mahakama ya Rufani, Masjala Kuu, Divisheni za Mahakama Kuu pamoja na Mahakama Kuu Dodoma (IJC).
Matukio katika picha Hafla ya Usiku wa Wanawake wa Mahakama-Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.
Sehemu ya Watumishi wanawake wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika hafla ya Usiku wa Wanawake wa Mahakama kusherehekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani jana tarehe 08 Machi, 2026 kwenye Ukumbi wa Cathedral uliopo jijini Dodoma.
Ukataji keki maalum zilizoandaliwa kwa ajili ya kusherehekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani tarehe 08 Machi, 2026.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

























Hakuna maoni:
Chapisha Maoni