Jumatatu, 9 Machi 2026

MAWAKILI MKOA WA MWANZA WALA KICHAPO GEITA

Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita

Timu ya mpira wa miguu ya Mahakama Kuu Kanda ya Geita imeibuka na ushindi wa mabao 3–2 dhidi ya Timu ya Mawakili kutoka Mwanza katika mchezo wa kirafiki uliochezwa Machi 7, 2026.

Mchezo huo ulifanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi na Sekondari St. Aloysius vilivyopo Shilabela, Manispaa ya Geita, ambapo timu hizo zilionyesha ushindani mkubwa na burudani kwa mashabiki waliohudhuria.

Katika mchezo huo, bao la kwanza la Mahakama Kuu Geita lilifungwa na Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Nyang’hwale, Robert Nyando. Bao la pili lilifungwa na Ateba Stephano huku bao la tatu likifungwa na Mhasibu wa Mahakama Kuu Geita, Goodluck Machange.

Kwa upande wa Timu ya Mawakili Mwanza, bao la kwanza lilifungwa kwa njia ya penalti na Wakili Fredrick Magaiwa baada ya mlinda mlango wa Mahakama Kuu Geita kushika mpira ndani ya eneo la hatari. Bao la pili lilifungwa na Wakili Hensen Emmanuel.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Jaji wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Geita, Griffin Mwakapeje, kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, aliwakaribisha wageni hao katika Mahakama Kuu Geita na kuwashukuru kwa kushiriki mchezo huo.

Alisema lengo la michezo hiyo ni kuimarisha mahusiano, ushirikiano na kubadilishana mawazo kati ya Wadau wa sekta ya sheria.

“Nia ya mashindano haya ni kutuleta pamoja, tusahau kwa muda majukumu ya kesi na kujumuika katika kujenga ushirikiano pamoja na kubadilishana mawazo. Pia inaonyesha kuwa licha ya majukumu mengi ya kisheria tuliyonayo, bado tunashiriki kikamilifu katika michezo,” alisema Jaji Mwakapeje.

Aidha, alimshukuru Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Fredrick Lukuna, kwa kuratibu na kufanikisha mashindano hayo. Aliongeza kuwa baada ya ujio wa Mawakili wa Mwanza mjini Geita, watumishi wa Mahakama Kuu Geita pia watafanya ziara ya kwenda Mwanza kwa ajili ya michezo kama sehemu ya kuimarisha ushirikiano huo.

Aliwasihi Mawakili wa Mwanza kuangalia uwezekano wa kusaidia Mkoa wa Geita kupata chapter yake ya Chama cha Mawakili ili kuimarisha shughuli za kisheria na ushirikiano katika ukanda huo.

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Mawakili (Mwanza Chapter) aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Geita kwa kukubali mwaliko na kushiriki mchezo huo.

Alisema licha ya timu yao kupoteza, wamefurahishwa na kiwango cha wachezaji wao na wameuchukulia mchezo huo kama fursa ya kuimarisha timu yao pamoja na afya za Mawakili.

Aliongeza kuwa hatua za Mkoa wa Geita kuwa na chapter yake ya Chama cha Mawakili zinaendelea vizuri, huku akiwakaribisha watumishi wa Mahakama Kuu Geita kutembelea Mwanza kwa ajili ya mchezo mwingine wa kirafiki siku zijazo.

Wachezaji wa Timu ya Mahakama na Mawakili Mwanza wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya mechi kuanza.

Wachezaji wa kikosi cha kwanza kutoka katika Timu ya Mawakili wa Serikali na Kujitegemea Mwanza wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya mechi kuanza.

Wachezaji wa kikosi cha kwanza  kutoka timu ya Mahakama Kuu Kanda ya Geita wakiwa katika picha ya pamoja.

Mchuano ukiwa unaendelea, William Msuya wa Mahakama ya Mwanzo Kharumwa akijaribu kumpokonya mpira Wakili wa Serikali Mwanza.

Wachezaji na Mashabiki wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Griffin Mwakapeje (wa katikati msitari wa kwanza) na Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Fredrick Lukuna wa tatu kushoto mistari wa kwanza).
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni