Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama-Dodoma
Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, watumishi Wanawake wa Mahakama
ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma tarehe 06 Machi, 2026 walitembelea watoto
njiti (premature) wanaopatiwa matibabu katika Hospitali ya Benjamin Mkapa.
Watoto hao ni wale waliozaliwa kabla ya wakati na waliokuwa
wakipatiwa huduma hospitalini hapo wakiwa na umri wa kuanzia siku moja hadi
siku 28 tangu kuzaliwa.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Afisa Rasilimali Watu
Mwandamizi wa Mahakama, Bi. Gladness Godwin Massawe alisema lengo la wanawake kutembelea
Hospitali hiyo ni kujionea hali ya watoto hao pamoja na kutambua umuhimu wao
katika jamii.
Alisema katika kuadhimisha siku hiyo waliamua kushiriki
katika tendo la kijamii kwa kuwatembelea watoto hao na kuwapatia baadhi ya
mahitaji muhimu pamoja na kugharamia matibabu ya mtoto mmoja aliyekuwa
akipatiwa huduma katika Chumba cha Uangalizi Maalum (ICU).
Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya kuonesha upendo,
mshikamano na kuwapa matumaini watoto hao pamoja na familia zao.
Wakati huohuo akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo kwa niaba ya Uongozi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto, Dkt. Rehema Yona alishukuru kwa msaada huo.
"Msaada huu umeleta faraja na matumaini kwa watoto pamoja na wazazi wao na umeonesha moyo wa upendo na kujali jamii," alisema Dkt. Rehema huku akiwatakia heri na baraka kwa kuendelea kushirikiana na jamii katika kusaidia wenye uhitaji.
Watumishi wanawake wa Makao Makuu ya
Mahakama ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuwasili katika Hospitali
ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma tarehe 06 Machi, 2026.
Watumishi wanawake wa Makao Makuu ya
Mahakama ya Tanzania wakielekea wodini kuona watoto katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH).
Afisa Rasilimaliwatu Mwandamizi wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Gladness Massawe akizungumza jambo mara baada ya kupokelewa katika Hospitali ya Benjamin Mkapa.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto kutoka Hospitali ya Benjamin Mkapa, Dkt. Rehema Yona akitoa shukrani mara baada ya kupokea wageni hao.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni