.Awasisitiza kuzingatia maadili, kuimarisha weledi na kutumia TEHAMA katika utoaji wa haki
Na. James Busanya & Halima Mnete
– Mahakama, Dodoma
Msajili Mkuu wa Mahakama ya
Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, amewasisitiza Mahakimu Wakazi wapya kuzingatia
maadili ya kazi, kuongeza weledi wa kitaaluma na kulinda taswira ya Mhimili wa
Mahakama katika utoaji wa haki kwa wananchi.
Mhe. Nkya ametoa wito huo jana
tarehe 6 Machi 2026 katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini
Dodoma, wakati akifunga rasmi mafunzo elekezi ya siku kumi kwa Mahakimu Wakazi
wapya 92, mafunzo yaliyoandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA)
kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe.
Nkya amesema ana furaha kushiriki hitimisho la mafunzo hayo na kueleza
matumaini kuwa siku kumi za mafunzo zimewajengea washiriki uwezo mpana kuhusu
majukumu ya uhakimu na misingi ya utoaji wa haki kwa kuzingatia sheria, kanuni
na taratibu zilizopo.
Amesema kazi ya uhakimu ni wito
unaohitaji umakini mkubwa kwa kuwa sehemu kubwa ya majukumu yake inahusiana
moja kwa moja na utoaji wa haki kwa jamii, hivyo Mahakimu wanapaswa kutambua
uzito wa dhamana waliyopewa na kuitumikia kwa uadilifu na weledi wa hali ya
juu.
Katika kusisitiza hilo, alimnukuu
Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, aliyewahi kusema kuwa zipo kazi
nyingi zinazoweza kufanywa na mtu yeyote, lakini kazi ya uhakimu si mojawapo
kutokana na uzito wake na mahitaji ya juu ya kitaaluma pamoja na kimaadili.
Aidha, Mhe. Nkya aliwakumbusha
Mahakimu hao kuwa uhuru wa Mahakama upo pale Hakimu anapozingatia kiapo chake
cha kazi na kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sheria bila kuingiliwa na
mtu au chombo chochote.
Msajili Mkuu huyo, aliwataka
kushirikiana na wadau wa sekta ya haki pamoja na viongozi wengine katika maeneo
watakayopangiwa kazi, akieleza kuwa ushirikiano huo utasaidia kuboresha
utendaji kazi na kuongeza ufanisi wa huduma ya utoaji haki kwa wananchi.
Vilevile, Mhe. Nkya aliwataka Mahakimu
hao kuzingatia Kanuni za Maadili ya Mahakama za mwaka 2020 ndani na nje ya Mahakama
kwa kusoma, kuelewa na kuzifuata kikamilifu, akibainisha kuwa Mahakama imara
hujengwa na watumishi wenye uadilifu.
“Mahakama imara hujengwa na
watumishi wenye uadilifu na kosa la Hakimu mmoja linaweza kuchafua taswira ya
Mhimili mzima wa Mahakama,” alisisitiza Mhe Nkya.
Kwa upande wa maendeleo ya kitaaluma,
Msajili Mkuu aliwahimiza Mahakimu hao kuendelea kujifunza na kujielimisha ili
kuongeza weledi wao katika utoaji wa haki na kuepuka makosa yanayoweza
kuepukika katika utendaji wao wa kazi.
Pia aliwataka kujiepusha na vitendo
vya rushwa, upendeleo na ubaguzi, kuzingatia nidhamu ya kazi, kutumia lugha ya
staha kwa wadau wa Mahakama pamoja na kutumia rasilimali za ofisi kwa ufanisi.
Katika hatua ya kuimarisha utendaji
kazi wao, Mahakimu hao walikabidhiwa vitendea kazi ikiwemo kompyuta mpakato
zitakazowasaidia katika uandishi wa hukumu na uendeshaji wa mashauri mbalimbali
kwa njia ya kidijitali.
Mhe. Nkya pia aliwahimiza
kuwakilisha ipasavyo matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA)
katika kazi zao za kila siku ili kuongeza ufanisi na kasi ya utoaji wa haki.
Aidha, Mhe. Nkya aliwataka Mahakimu
hao kulinda taswira ya Mahakama wakati wote na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa
kuwawezesha kukutana katika mafunzo hayo, huku akiwaombea mafanikio mema katika
utekelezaji wa majukumu yao mapya ya kuhudumia jamii kupitia Mhimili wa Mahakama.
Msajili
Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Kiaki Nkya, akifunga rasmi mafunzo
elekezi ya siku 10 kwa Mahakimu Wakazi wapya 92, yalioandaliwa na Chuo cha
Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania jana
tarehe 6 Machi, 2026 katika Ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama jijini
Dodoma.
Sehemu ya Mahakimu Wakazi wapya waliomaliza mafunzo ya siku 10 wakisikiliza hotuba ya Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (hayupo pichani)
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Kiaki Nkya (Katikati) akiwa Meza Kuu na Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo Bi. Patricia Ngungulu (wa kwanza kulia) wakati wa kufunga mafunzo hayo elekezi kwa Mahakimu Wakazi Wapya 92.
Sehemu
ya Mahakimu Wakazi wapya waliomaliza mafunzo ya siku 10 wakisikiliza hotuba ya
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (hayupo pichani)
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni