Wananchi wa Mkoa wa Geita wamenufaika na mpango wa utoaji elimu kwa Umma ulioratibiwa na Mahakama Kuu Masjala ya Geita.
Utoaji huo wa
elimu ulifanyika tarehe 03 Machi, 2026 katika Ukumbi wa Elimu kwa Umma, Kituo
Jumuishi (IJC) Geita.
Mada
iliyowasilishwa ilikuwa ‘Utekelezaji wa Amri za Mahakama,’
ikiwa na lengo la kuwajengea wananchi uelewa kuhusu taratibu za kisheria baada
ya hukumu kutolewa.
Elimu hiyo
ilitolewa na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Geita, Mhe.
Mujuni Muchunguzi, ambaye alieleza kwa kina hatua
zinazofuatwa katika utekelezaji wa amri za Mahakama mara baada ya hukumu
kutolewa.
Katika mafunzo
hayo, Mhe. Muchunguzi alifafanua kuwa utekelezaji wa amri za Mahakama
hufanyika kwa njia mbalimbali, ikiwemo kukamata na kuuza mali za mdaiwa,
kuamrisha jambo fulani litendeke ili kumpatia mdai haki yake, au utekelezaji wa
kifungo cha madai pale inapobidi. Alieleza kuwa taratibu zote hufuata misingi
ya kisheria ili kuhakikisha haki inatendeka kwa pande zote zinazohusika.
Aidha, wananchi
walipata fursa ya kuuliza maswali kuhusu migogoro ya ardhi, zuio litolewalo na Mahakama
na masuala ya dhamana katika mikopo ya benki.
Akijibu hoja hizo,
Mhe. Muchunguzi alisisitiza kuwa endapo mali itauzwa kwa
thamani kubwa kuliko deni, kiasi kinachozidi hurudishwa kwa mdaiwa.
Aliongeza kuwa
migogoro ya ardhi inapaswa kuanzia Baraza la Ardhi la Kata kwa usuluhishi na
baadaye kama hawajaelewana kupeleka mgogoro wa ardhi kwenye Baraza la Ardhi
Nyumba na Makazi Wilaya kwa mujibu wa sheria.
Alisema
kwamba ni kosa la kukaidi amri ya Mahakama, ambapo anayekiuka zuio halali
anaweza kuchukuliwa hatua za kisheria.
Wananchi walieleza kufurahishwa na elimu hiyo, wakisema imewasaidia kuelewa haki na wajibu wao katika masuala ya kisheria. Mahakama imeueleza Umma huo kuwa itaendelea kutoa elimu kama hiyo mara kwa mara ili kuongeza uelewa wa sheria na kuimarisha upatikanaji wa haki kwa jamii.
Jaji Mfawidhi
wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, akiwahutubia na kuwasalimia
wananchi, huku akiwaalika wale wote wenye changamoto au wanaohitaji msaada wa
kisheria kujitokeza ili wasikilizwe na kupatiwa msaada stahiki.
Hakimu Mfawidhi wa
Mahakama ya Wilayya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi
akiendelea kutoa elimu kwa wananchi Mkoa wa Geita.
Wananchi Mkoa wa
Geita wakiendelea kupata mafunzo katika ukumbi
wa mafunzo wa Mahakama Kuu Geita.
Hakimu Mfawidhi,
Mhe. Mujuni Muchunguzi akiwa katika picha
ya pamoja na Wananchi baada ya
mafunzo.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni