Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya
Mahakama
Kuu Kituo cha Usuluhishi jijini Dar es Salaam kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi
wa Mahakama Lushoto (IJA) imeendesha mafunzo maalum ya Usihi na Usuluhishi kwa Naibu
Wasajili na Mahakimu Wakazi toka katika Mahakama mbalimbali za mikoa ya Nyanda
za Juu Kusini ikiwemo Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Iringa, Njombe, Sumbawanga,
Songwe, Songea na Katavi.
Mafunzo
hayo ya siku tatu yalianza tarehe 24 Machi, 2026 hadi tarehe 26 Machi 2026
katika ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya yakiongozwa na Jaji
Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga ambaye pia ni
alikuwa mwezeshaji akishirikiana na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya
Momba Mhe. Raymond Kaswaga pamoja na Mhe. Gloria Shuma kutoka Chuo cha Uongozi
wa Mahakama (IJA).
Akizungumza
wakati wa kufunga mafunzo hayo Mhe. Tiganga alitoa shukrani zake za dhati kwa
Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi Dar Es Salaam, Mhe. Zahara
Maruma kwa kuandaa na kuratibu Mafunzo hayo. Vilevile, aliwaasa washiriki kuwa
chachu ya mabadiliko katika kutatua migogoro mingi kwa njia ya usuluhishi.
“Kwa
mafunzo haya mliyoyapata mkawe sababu ya mabadiliko katika kutatua migogoro
mingi kwa njia ya usuluhishi na kuwa walimu wazuri kwa kuwapa wengine kile mlichojifunza
kwa ambao hawakupata bahati ya kuwa sehemu ya mafunzo haya. Natamani mashauri
mengi katika masjala zetu yaishe kwa njia ya Usuluhishi” alisema Mhe. Tiganga.’’
alisema Mhe. Tiganga.
Mafunzo
hayo yanaendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na Mpango Mkakati wa
Mahakama unaosisitiza umuhimu wa kutumia njia mbadala ya utatuzi wa migogoro
(usuluhishi) ili kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.
Na
pia ni utekelezaji wa Ibara ya 107 A (2) (d) ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ya 1977. Mafunzo hayo yalilenga pia maandalizi ya Wiki ya Usulujishi
itakayozinduliwa tarehe 9 Aprili 2026 katika Ukumbi wa Golden Jubilee PSSSF
Tower Dar Es Salaam na kufuatiwa na Wiki ya Usuluhishi itakayofanyika Nchi
nzima kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili, 2026.
Akizungumza
kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya
Mbeya Mhe. Tedy Mlimba alitoa shukurani kwa waandaaji na wawezeshaji wa mafunzo
hayo kwa kufanikisha mafunzo hayo na kuahidi kuwa watayafanyia kazi yale
waliyofundishwa na watakuwa walimu wazuri kwa wengine ambao hawakupata bahati
ya kuwa sehemu ya mafunzo hayo.
Sehemu
ya mada zilizofundishwa ni pamoja na dhana ya Usuluhishi, sheria na kanuni za
usuluhishi, mambo muhimu ya kuzingatia wakati wa usuluhishi, nafasi ya sheria
na mawakili katika usuluhishi, vikwazo na changamoto katika usuluhishi na pia
mafunzo hayo yaliambatana na mazoezi ya vitendo (Practical sessions)
yaliyowasaidia washiriki kuelewa kwa kina namna ya kuendesha vikao vya
usuluhishi kwa ufanisi.
Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim
Tiganga, akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo.
Viongozi wa Mahakama Kuu Mbeya wakiwa Meza Kuu wakati wa kufunga mafunzo ya Usuluhishi Nyanda za Juu Kusini katikati ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (kushoto) na Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo (kulia)
Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.
Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.
Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya
Mhe. Aziza Temu akikabidhiwa cheti na Jaji Mfawidhi Mahakama kuu kanda ya Mbeya
Mhe. Joachim Tiganga kwa kuwa sehemu ya mafunzo hayo.
Mhe. Raimond Kaswaga akikabidhiwa cheti na Jaji
Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga kwa kuwa sehemu ya
wawezeshaji katika mafunzo hayo.
Washiriki katika mafunzo hayo wakiwa katika mazoezi ya
vitendo (Practical session) ya namna ya kuendesha vikao vya usuluhishi.
Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim
Tiganga akikabidhiwa cheti na Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya
Songea Mhe. Elizabeth Nyembele kwa kuwa sehemu ya wawezeshaji katika mafunzo
hayo.
Mwezeshaji katika mafunzo hayo ambaye ni Jaji Mfawidhi
Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, akimwaga madini wakati wa
mafunzo hayo.
Mwezeshaji katika mafunzo hayo ambaye ni Hakimu mkazi
Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba Mhe. Raimond Kaswaga akifundisha wakati wa
mafunzo hayo
Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe.
Tedy Mlimba akitoa neno la shukurani kwa waandaaji na wawezeshaji wa mafunzo
hayo kwa niaba ya washiriki wa mafunzo.
Mhe. Gloria Shuma kutoka Chuo Cha Uongozi wa mahakama
(IJA) akitoa neno la shukurani katika Ufungaji wa mafunzo hayo
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni