Jumatatu, 30 Machi 2026

WATUMISHI WANAWAKE WA MAHAKAMA KANDA GEITA WAFANYA MATENDO YA HURUMA

Na DOTTO NKAJA – Mahakama Kuu, Geita

Wanawake wa Mahakama Kanda ya Geita kutoka Mahakama Kuu Geita, Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, Mahakama ya Wilaya ya Geita na Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, tarehe 28 Machi  2026 walitembelea Wodi ya Wajawazito na Wazazi katika Kituo cha Afya Kasamwa.

Lengo la ziara hiyo ni kufanya matendo ya huruma ikiwa ni utaratibu waliojiwekea kila mwaka wanapoadhimisha kilele cha Siku ya Wanawake Duniani.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kasamwa, Dkt. Emmanuel Zillagera, pamoja na Watumishi wengine wa Kituo hicho waliwaongoza Wanawake wa Mahakama katika wodi hizo na kutoa zawadi mbalimbali.

Watumishi hao wa Mahakama walitoa vifaa na mahitaji kwa Wajawazito na Wazazi ambavyo ni sukari, sabuni za unga, mafuta ya kujipaka, pampers na vingine.

Akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo, Dkt. Zillagera aliwashukuru Wanawake wa Mahakama kwa matendo ya huruma waliyotoa. Pia aliwaomba kurudi kipindi kingine kwa ajili ya hiyo mara watakapopata nafasi.

Naye Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Bi. Masalu Kisasila, aliwashukuru Viongozi pamoja na Watumishi wa Kituo hicho kwa kuwakubalia kufika na kufanya matendo ya huruma.

"Kila mwaka Wanawake wa Kanda ya Geita wanapokuwa wanaelekea kilele cha Siku ya Wanawake Duniani, hufanya matendo ya huruma kwa kupeleka vifaa ambavyo ni mahitaji mbalimbali. Kitendo hiki ni sadaka yetu kama Wanawake kwa Wazazi pamoja na Wajawazito,” alisema.

Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Masalu Kisasila, akikabidhi sabuni, pampers na vitu vingine kwa Muuguzi Mkunga Sr. Joyce wa Kituo cha Afya Kasamwa.

Watumishi wa Mahakama Kanda ya Geita wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kufika katika Kituo cha Afya Kasamwa.

Watumishi wa Mahakama Kanda ya Geita wakiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Kituo cha Afya Kasamwa (juu na chini).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni