Jumapili, 29 Machi 2026

TAWJA YANADI MATUMIZI YA TEHAMA NDANI YA MAHAKAMA NCHINI YANAVYOCHAGIZA UPATIKANAJI HAKI KWA JAMII

Na Mwandishi wetu, New York-Marekani

Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) hivi karibuni kilielezea ni kwa vipi kinachagiza matumizi ya teknolojia kwa lengo la kuhakikisha haki mahakamani kwa jamii hususan kwa wanawake na wasichana inapatikana kwa wakati.

Wakizungumza wakati wa kikao cha kando kwenye Mkutano wa 70 wa Kamisheni ya Hali ya Wanawake duniani, CSW70 jijini New York, Marekani, chama hicho kilisema kinafanya hivyo ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono mageuzi ya Mahakama nchini Tanzania.

Kikao hicho cha kando kilikuwa na maudhui Kutatua vikwazo vya kijinsia kwenye haki kupitia mahakama ya mtandao nchini Tanzania, ambapo walitaja mageuzi hayo kuwa ni pamoja na mifumo ya kidijitali na mahakama za mtandaoni.

Muda wa kusikiliza kesi umepungua

“Kupitia uwekezaji katika teknolojia na ubunifu wa mifumo ya TEHAMA, Mahakama nchini Tanzania zinaendelea kuwa jumuishi zaidi, zenye ufanisi, na rafiki kwa watumiaji—hasa wanawake na manusura wa ukatili wa kijinsia, (GBV),” amesema Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Barke Sehel ambaye pia ni Mwenyekiti wa TAWJA iliyoanzishwa mwaka 2000 na kusajiliwa rasmi mwaka 2022

“Hatua kubwa iliyopigwa ni pamoja na uhifadhi wa kidijitali wa zaidi ya mafaili 10,000 ya zamani jijini Dar es Salaam, jambo lililopunguza muda wa kutafuta mafaili kutoka wiki kadhaa hadi dakika chache. Maboresho haya yameongeza kasi ya upatikanaji wa haki na kupunguza ucheleweshaji wa kesi unaowaathiri zaidi wanawake na makundi yaliyo hatarini,” alisema Mwenyekiti huyo wa TAWJA.

Kiini cha mabadiliko ni nini?

Kiini cha mabadiliko haya ni Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (JoT e-CMS), unaorahisisha shughuli zote za mahakama kwa njia ya kidijitali.

“Mfumo huu unaruhusu ufungaji wa mashauri kwa njia ya mtandao (e-filing), ufuatiliaji wa kesi kwa wakati halisi, na upatikanaji wa kumbukumbu za kesi kwa urahisi.” Alieleza Jaji Sehel.

Hali kadhalika mfumo huo umewezesha kupanga kazi kiotomatiki ikiwa ni pamoja kugawa mashauri kwa MajajI, kupanga ratiba za usikilizwaji na utoaji wa taarifa kwa wahusika. “Faida zake ni pamoja na upatikanaji wa huduma saa 24, kupunguza gharama za uendeshaji, na kupunguza makosa ya kibinadamu katika usimamizi wa kesi,” alifafanua Mwenyekiti huyo wa TAWJA.

Faida za mahakama mtandao

Wakati wa kikao hicho iliwekwa bayana ni kwa kiasi gani TEHAMA inaboresha haki pamoja na matumizi ya akili unde (AI) katika kurekodi, kutafsiri na kushughulikia ushahidi.

“Hii imepunguza kwa kiasi kikubwa maumivu ya kisaikolojia kwa manusura wa GBV kwa kuepusha kurudia simulizi za matukio yanayowapatia kiwewe,” alisema Jaji Sehel.

Faida zingine za Mahakama Mtandao ni kuruhusu mashahidi kushiriki katika shauri wakiwa mbali, ndani na nje ya nchi. Aidha, katika Makao Makuu ya Mahakama yaliyopo Dodoma, kuna  chumba maalum cha Kanzi Data au Data Hub kinachowezesha uchambuzi wa taarifa za shauri kwa wakati halisi, ikiwemo mashauri ya GBV.

Jambo lingine lililozungumziwa ni mfumo wa “Sema na Mahakama” unaotoa fursa kwa wananchi kutoa maoni au malalamiko kupitia simu au mtandao, huku Programu ya Mahakama za Mwanzo ikitoa takwimu za moja kwa moja kwa ajili ya ufuatiliaji na maamuzi.

Kuwezesha Wanawake Kupitia Haki za Kidijitali

Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) kimesisitiza kuwa, matumizi ya teknolojia si tu kwa ajili ya kuboresha utendaji bali pia ni nyenzo muhimu ya kuhakikisha haki za wanawake zinazingatiwa. Kupitia mifumo hiyo, gharama zinapungua, faragha inaongezeka  na mazingira ya haki yanakuwa salama zaidi kwa wanawake.

Hata hivyo, Chama hicho kimeonya kuwa, matumizi ya teknolojia yanapaswa kuzingatia usawa ili kuepuka kuongeza changamoto mpya kwa makundi yaliyo pembezoni.

Teknolojia isijenge ukuta kati ya wa mijini na vijijini

Ni kwa mantiki hiyo Hakimu wa Mkoa, Zanzibar na pia Mratibu wa TAWJA huko Zanzibar, Sara Omar Hafidh alizungumzia umuhimu wa mafunzo endelevu kwa watendaji wa Mahakama.

“Sote tunajua kuwa kujifunza kubonyeza kitufe sahihi kwenye kompyuta ni jambo rahisi. Lakini sehemu ngumu ni kuendesha mahakama ya mtandaoni kwa huruma na uelewa. Tunawafundisha majaji na mahakimu wetu kushughulikia majeraha ya kisaikolojia kupitia skrini, kuhakikisha kwamba hata katika mazingira ya kidijitali kila mwananchi anahisi kuonekana, kusikilizwa, na kuheshimiwa,” alisema Mratibu huyo wa TAWJA, Zanzibar.

Jambo lingine ni kuhakikisha mifumo ya kidijitali ina ulinzi madhubuti wa taarifa.” Ni dhahiri kuwa mtu aliye katika hali ya hatari akihisi kuwa taarifa zake binafsi zinaweza kuvuja, ataogopa kujitokeza. Hivyo, dunia yetu ya kidijitali lazima iwe salama na isiyopenyeka. Teknolojia inapaswa kuwa ngao ya ulinzi—ngao inayowalinda walio dhaifu, si mwanga unaowaweka wazi,” alisema.

Mafunzo yanayotolewa na TAWJA

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) na Katibu Msaidizi wa TAWJA, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda alisema Chama hicho ndicho cha kwanza kuanzisha mafunzo kwa watendaji wa Mahakama nchini Tanzania miaka ya 2000.

“Mafunzo haya yanayotolewa kwa ushirikiano na Mahakama ya Tanzania yanalenga pamoja na mambo mengine kujenga uwezowa majaji, mahakimu, waendesha mashtaka,askari polisi, magereza na wachunguzi wa kesi,” alisema.

Kupitia mafunzo hayo, washiriki hupewa maarifa na ujuzi wa vitendo unaohitajika kushughulikia kesi zenye mwelekeo wa kijinsia, ikiwemo ukatili wa kijinsia, unyanyasaji wa kingono, talaka na migogoro ya ndoa, ukatili dhidi ya watoto na matunzo yao, pamoja na masuala ya mirathi, na ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.

Washiriki pia hufundishwa jinsi ya kuepuka kuongeza maumivu ya kisaikolojia kwa manusura wa unyanyasaji wa kingono na ukatili wa kijinsia, kwa kudhibiti mwenendo wa mahakama na kukusanya ushahidi kutoka kwa manusura kwa njia inayolinda utu wao, ili kufikia maamuzi ya haki.


Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dorothy Gwajima (wa tatu kulia) na wenzake wakiwa kwenye kikao cha kando cha CSW70 kilichofanyika hivi karibuni jijini New York nchini Marekani, kuhusu Kutatua Vikwazo vya Kijinsia kwenye haki kupitia Mahakama Mtandao. Wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel, wa tatu kushoto ni Mkurugenzi wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) na Katibu Msaidizi wa TAWJA, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda pamoja na washiriki wengine kutoka Tanzania.

Mkurugenzi wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) na Katibu Msaidizi wa TAWJA, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda akizungumza jambo kwenye kikao cha kando cha CSW70 kilichofanyika hivi karibuni jijini New York nchini Marekani kuhusu Kutatua Vikwazo vya Kijinsia kwenye haki kupitia Mahakama Mtandao.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni