Jumatano, 25 Machi 2026

TMJA TAWI LA KILIMAJARO YANOGESHA MASHINDANO YA KILIMANJARO MARATHON 2026

  • Watumia jukwaa hilo kutoa elimu ya sheria kwa umma
  • Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo awapongeza

Na PAUL MUSHI- Mahakama, Moshi

Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Tawi la Kilimanajaro, wakiongozwa na Mlezi wao, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lilian Mongella, hivi karibuni walishiriki kikamilifu kwenye mbio za urefu wa Kilomita 42, 21 na 5 katika kwenye tamasha kubwa la michezo la International Kilimanjaro Marathon.

Tamasha hilo lililofanyika kuanzia tarehe 19 hadi tarehe 22 Machi, 2026 liliongozwa na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda na kushirikisha Wadau wa michezo wa ndani ya nchi na mataifa mbalimbali duniani. Mhe. Makonda pia alitoa zawadi kwa washindi katika mbio za aina tofauti.

Baada ya kutoa zawadi hizo, Waziri Makonda alitembelea na kukagua mabanda yaliyokuwa yanatoa huduma mbalimbali, likiwemo la TMJA lililokuwa linatoa elimu ya masuala ya kisheria kwa Wananchi.

Akiwa kwenye banda hilo, Mhe. Makonda aliwapongeza Majaji na Mahakimu  kwa kutumia jukwaa hilo kuimarisha afya zao na kutoa elimu kuhusu masuala mbalimbali ya kisheria.

“Nilipata taarifa ya uwepo wenu katika tamasha hili, kwakweli sikutegemea kama mngekuwepo. Nawapongeza sana kwa kazi kubwa mliyoifanya, hasa ya kutoa elimu katika siku hizi zote toka siku ya ufunguzi. Niwaombe muendelee na awamu zijazo ili muwafikie watu wengi zaidi kwa elimu hii mnayotoa,” alisema Waziri Makonda.

Naye Mhe. Dkt. Mongella aliwapongeza washiriki kwa kujitoa kwao katika hali na mali kushiriki katika tamasha hilo kwa lengo la kuimarisha afya zao na kutoa elimu kwa watu wenye uhitaji kwenye masuala ya kisheria.

“Nawapongeza sana viongozi wa Tawi letu la TMJA Kilimanjaro kwa kuona umuhimu kwa kushiriki tamasha hili kubwa. Hili si tu kwamba ni muhimu katika kujenga afya zetu, bali pia jambo la kutoa elimu ni kubwa zaidi, hasa kwa kuzingatia uwingi wa watu katika tamasha,” alisema.

Katika hatua nyingine, Rais wa TMJA, Mhe, Elimo Massawe, aliyeambatana na Katibu wa Chama hicho, alipata fursa ya kutembelea na kuona shughuli zilizofanyika wakati wa tamasha hilo.

Mhe. Masawe naye aliwapongeza wanachama wa Tawi hilo kwa kazi kubwa waliyofanya na kuwapa shime ya kuendelea kuwa wabunifu na kufanya zaidi kwa siku zijazo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lilian Mongella akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kutembelea banda la maonyesho katika viwanja vya ushirika Moshi yalipofanyikia mashindano ya Kilimanjaro Marathon 2026.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda, (wa kwanza kushoto mwenye fulana ya njano) akikabidhiwa zawadi na Mjumbe wa Baraza Tendaji Taifa wa Chama cha Majaji na Mahakimu, Mhe. James Kapele, kwa niaba ya mlezi wa Tawi, baada ya kutembelea banda la chama hicho.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi wakitoa elimu kwa Wananchi waliofika katika banda la Mahakama katika viwanja vya ushirika Moshi yalipofanyikia mashindano ya Kill Marathon 2026.

Rais wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania, Mhe. Elimo Massawe, alipotembelea banda la TMJA Tawi la Kilimanjaro wakati wa tamasha la Kilimanjaro Marathon 2026.

Baadhi ya Watumishi wa Mahakama walioshiriki mbio wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kumaliza mbio za Kill marathon 2026.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni