Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma
Mbunge
wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake, Prof. Joyce Ndalichako
amewaeleza Majaji na Mahakimu Wanawake wa Tanzania kuwa, weledi na uadilifu ndizo
nguzo kuu na muhimu za utendaji hivyo hawana budi kuzizingatia wakati
wanapotimiza wajibu wao.
Prof.
Ndalichako aliyasema hayo jana tarehe 10 Machi, 2026 alipokuwa akifunga
Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu
Wanawake, lililofanyika katika ukumbi wa New Generation Hall Kisasa jijini
Dodoma.
Akizungumza
wakati wa kufunga Kongamano hilo, Prof. Ndalichako amesema kuwa, ameridhishwa
na mjadala wenye afya na nia ya dhati ya kujenga na kuimarisha haki na usawa wa
kijinsia, pamoja na maazimio yaliyowekwa ambayo watakwenda kuyatekeleza.
Aliongeza
kuwa, lengo la kuanzishwa kwa TAWJA ni kutambua mchango wa Majaji Wanawake
duniani na kuhimiza usawa wa kijinsia katika Mhimili wa Mahakama, hivyo
kongamano hilo ni tukio muhimu la kubadilishana maarifa kuonesha uongozi, ujasiri
na dira ya mabadiliko pia ni mwanga unaoangaza nuru na kazi kubwa wanayoifanya
ambayo inaakisiwa hadi nje na si ndani ya kumbi za Mahakama pekee bali katika
jamii nzima.
Prof.
Ndalichako amesisitiza kuwa uadilifu ni nguzo kuu ya utendaji, hivyo ni vema
Majaji na Mahakimu Wanawake kuendelea kuzingatia uadilifu katika masuala ya
haki, huku akinukuu maneno ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.
Samia Suluhu Hassan wakati alipokuwa akiwaapisha Majaji ambapo alisema, “uzoefu
umeonesha kuwa Majaji wanawake huwazidi wenzao wa kiume katika utendaji
unaozingatia masuala ya uadilifu.”
Aliongeza
kuwa, anavutiwa na weledi, mshikamano na kujitoa kwa Majaji na Mahakimu
wanawake hali inayoleta mabadiliko ya kijamii kwa kuzingatia utawala wa haki
unaoleta usawa wa kijinsia.
Aidha,
amesema kuwa haki haitoshi kutolewa bali inapaswa ieleweke na iguse mioyo ya
watu pamoja na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama, hivyo Majaji na Mahakimu
Wanawake wana nafasi muhimu katika kuhakikisha sheria inazungumza kwa haki na
uadilifu.
Katika
hatua nyingine, Prof. Ndalichako alizungumzia kuhusu umuhimu wa kuimarisha
mifumo ya Taasisii ili kulinda afya ya kisaikolojia ya Mahakimu ambapo ameeleza
kuwa mtu hawezi kuponya wengine ikiwa yeye mwenyewe ana maumivu, hivyo ni vema
kulinda afya ya akili ili kuimarisha utendaji.
“Mmesisitizwa
pia kuhusu umuhimu wa kulinda mifumo ya Taasisi ili kulinda afya ya
kisaikolojia ya Mahakimu, huwezi kuponya jamii wakati wewe mwenyewe unaumia
kimyakimya, ni vema kuendelea kuhakikisha kwamba tunalinda afya za akili ndani
ya Makahama ili iendelee kutoa haki endelevu,” alisisitiza Mwenyekiti huyo.
Kadhalika,
alisema kuwa, ni vema kuepuka kuwajeruhi upya wahanga na manusura wa ukatili wa
kijinsia na kusisitiza kuwa, manusura wanastahili kujisikia salama na
kuheshimiwa, hivyo haki lazima irejeshe utu na si kufungua tena majeraha.
Alieleza
kwamba, teknolojia inakua kwa kasi hivyo ni vema itumike katika kuwalinda
waathirika wa masuala ya ukatili wa kijinsia hasa ukatili wa mitandaoni, hivyo ubunifu
ni lazima uendelee kutumika ili kuimarisha ulinzi wa waathirika na kuongeza
uwajibikaji kwa kutumia Mahakama mtandao.
Alisema
kuwa, yeye kama Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake anawahakikishia kuwa, Bunge
pamoja na Wabunge wengine wataendelea kushirikiana katika kuimarisha sheria
zinazolinda wanawake na watoto, hivyo ujumbe alioubeba katika mijadala ya leo
utatumika ili kuendelea kukuza usawa wa kijinsia.
Katika
hatua nyingine, Prof. Ndalichako ameeleza kuwa mojawapo ya mafanikio makubwa
kwa Mahakama na Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA) ni kufikia usawa
wa asilimia 50 kwa 50 kwa Majaji jambo ambalo ni la msingi katika kukuza imani
kwa wananchi.
Kama
Kaulimbiu ya mwaka huu inavyokumbusha, amewataka Majaji na Mahakimu hao
wanawake kutoka mahakamani na kwenda kwenye jamii wakitoa haki kwa uadilifu
huku wakijihusisha kikamilifu katika shughuli za uelimishaji hususan kupitia
vyombo vya habari, kuzalisha maarifa na kujengeana uwezo jambo litalaojenga
uaminifu kwa jamii ya watoto wa kike kuwa ndoto zao ni halali na matarajio yanawezekana
na mustakabali wa maisha yake hauna mashaka.
Kauli
mbiu ya Kongamano hilo kwa mwaka huu ni “Kutoka mahakamani kuifikia jamii: Majaji
na Mahakimu wanawake mstari wa mbele kuongoza mapambano dhidi ya ukatili wa
kijinsia.
Awali,
kongamano hilo lilifunguliwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Juma Homera, ambaye
alikuwa mgeni rasmi katika ufunguzi. Kongamano hilo lilihudhuriwa na Mtendaji
Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, UN Women, Mwakilishi
kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mwakilishi kutoka Ofisi ya
Mkurugenzi wa Mashtaka na wageni wengine waalikwa.
Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako akizungumza alipokuwa mgeni rasmi wakati wa kufunga Kongamano maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma.
Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) baada ya kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma. Aliyekaa kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Winifrida Korosso.
Mgeni rasmi Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (kushoto) akifuatilia kinachojiri wakati wa kufunga Kongamano maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake. Kushoto kwake ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Kongamano hilo, Mhe. Winifrida Korosso.
Mgeni rasmi wakati wa kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake, Prof. Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Majaji Wanaume waliohudhuria katika Kongamano hilo.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni