Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma
Wanafunzi wapatao 19 wa kidato cha sita kutoka Shule ya
Sekondari Bulonge mkoani Kigoma wametembelea Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya
Kigoma ili kupata fursa ya kujifunza masuala mbalimbali ya kisheria, mchango wa
Mahakama katika kukuza siasa na Utawala wa Sheria nchini.
Akitoa elimu kuhusu namna Mahakama nchini inavyofanya kazi tarehe
13 Machi, 2026 kwenye ukumbi Mahakama ya wazi wa Mahakama Kuu Kigoma, Msaidizi
wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola aliwaeleza
wanafunzi hao kuhusu majukumu ya Mahakama katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na namna Mhimili huo unavyoshiriki kutoa haki katika mashauri
mbalimbali ya uchaguzi na kutoa haki na amri mbalimbali zinazolinda na kuleta
amani na ustawi wa Nchi.
Aidha, wanafunzi hao walisisitizwa kufuatilia hotuba mbalimbali
za Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, hususani ya tarehe 31 Julai, 2025
jijini Dodoma wakati akitoa salamu kwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania
waliokuwa wakishiriki katika Mafunzo ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi
yaliyofanyika kwa njia ya Mahakama Mtandao (Virtual Court).
Kadhalika, Mhe. Msola aliwafundisha ni kwa jinsi gani Mahakama
inatoa fursa kwa mgombea wa chama chochote ambaye hajaridhika na matokeo ya
uchaguzi kuja Mahakama ya Wilaya husika kufungua shauri katika ngazi fulani ya
uchaguzi, hata hivyo anaweza kukata
rufaa kwenda Mahakama Kuu au ya Mahakama
ya Rufani asiporidhishwa na hukumu ya Mahakama ya chini.
Alisema kuwa, kwa Mahakama za Mwanzo zote, rufaa zake hupelekwa
Mahakama za Wilaya na Mahakama za Wilaya rufaa zake hupelekwa Mahakama Kuu ya
Tanzania na vilevile Mahakama Kuu rufaa zake huwasilishwa Mahakama ya Rufani
ili kutoa haki iliyokosekana kutolewa kwa Mahakama za chini.
“Kupitia mlolongo huo, mwananchi/wanasiasa wanayo fursa kubwa ya
kutafuta haki aliyonyimwa na Tume ya Uchaguzi, kwa namna hiyo Mahakama
inashiriki kikamilifu katika kukuza siasa na haki nchini,” alisisitiza Mhe.
Msola.
Aidha, aliwaasa wanafunzi hao kusoma kwa bidii na kujituma huku
wakikua katika maadili ya kuwa viongozi wasomi katika kada mbalimbali
wanazopenda kusomea.
Hata hivyo, aliwakaribisha katika tasnia ya sheria kwani ni
miongoni mwa tasnia mahsusi katika kulinda na kutetea haki za kisiasa na
masuala mbalimbali ya kijamii na kiuchumi, na kuwasisitiza kusoma na kufaulu
vizuri ili kuweza kupata fursa ya kufika elimu ya juu katika masomo yao ili
kuja kuwa viongozi wenye tija kwa jamii na Taifa kwa ujumla.
Akizungumza juu ya nia yao ya kujifunza kupitia Kazi Mradi
(School Project), Kiongozi wa Wanafunzi hao, Bw. Sefu Hamis alibainisha kiu
waliyokuwa nayo kujifunza masuala ya kisheria hususani sheria za siasa ambapo alisema, “tunapenda kufahamu mchango wa
Mahakama kukuza siasa na taratibu za kusikiliza mashauri hayo ili kulinda haki za
wanasiasa.”
Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola akisisitiza jambo fulani alipokuwa akitoa elimu kwa wanafunzi wa kidato cha sita Shule ya Sekondari Bulonge juu ya utaratibu wa usikilizwaji wa mashauri ya uchaguzi.
Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola akifundisha kwa vitendo wanafunzi wa kidato cha Sita Shule ya Sekondari Buronge namna ambavyo Mahakama huketi kusikiliza mashauri mbalimbali ikiwemo ya uchaguzi.
Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Bulonge Kidato cha Sita, Bi. Elizabeth Elifasi akisoma Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 107 inayoainisha uanzishwaji wa Mahakama ya Tanzania wakati wakipatiwa elimu na Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola (hayupo katika picha).
Wanafunzi wapatao 19 wa Kidato cha Sita kutoka Shule ya Sekondari Bulonge wakisikiliza kwa makini mtoa elimu Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola alipokuwa akitoa mada wakati walipotembelea Mahakama Kuu Kigoma.
Picha ya pamoja ya Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wanafunzi wapatao 19 wa kidato cha sita Shule ya Sekondari Bulonge mara baada ya kupatiwa elimu.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mwanza)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni