Jumanne, 10 Machi 2026

WATUMISHI WANAWAKE KIGOMA WASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI

  • Wanawake mkoani humo waaswa kuchangamkia fursa zilizopo kuboresha uchumi wa familia na taifa letu

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo aliwaongoza wanawake wa Mahakama Kanda ya Kigoma kujumuika na wanawake wenzao waliojitokeza wilayani Kakonko kwenye sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo kimkoa ilifanyika katika Wilaya hiyo. 

Mgeni Rasmi katika sherehe hizo zilizofanyika tarehe 08 Machi, 2026 alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mhe. Dinah Mathamani aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Balozi Simon Sirro.

Akizungumza na wanawake waliofika katika viwanja hivyo, Mhe. Mathamani, alisema kuwa, kupitia Kauli mbiu yam waka huu ya Siku ya Wanawake Duniani isemayo, "Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050," Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira rafiki yanayowawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo, uchumi na uongozi kupitia sera, programu na fursa mbalimbali za uwezeshaji.

Amewahimiza wanawake kwamba, wanao wajibu mkubwa wa kusimamia maadili ya familia na kulea kizazi kijacho na kwamba Serikali inaendelea kufungua fursa za kiuchumi na kuboresha miundombinu muhimu ya Afya, Elimu, Kilimo, Biashara na Uchukuzi katika kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

Alieleza kuwa, uboreshaji wa huduma ya afya kutoka Hospitali za Wilaya na Halmashauri tatu, na kufikia tarehe 08 Machi zilikuwa nane sawa na asilimia 166.6, na Vituo vya Afya kutoka 34 mpaka kufikia 53 sawa asilimia 55.8, na kwa upande Shule za Sekondari awali zilikuwa 194 na sasa zipo 256 sawa na asilimia 31.9, ambapo shule za msingi awali zilikuwa 664 na sasa zimejengwa na kufikia 742 sawa asilimia 11.7.

“Hatua zote hizo zimeenda sambamba na ujenzi wa madarasa ya Shule za Sekondari kutoka 1,900 mpaka 3288 sawa na asilimia 70 na kwa Shule za Msingi vyumba vilikuwa 5401 na sasa tunaongea vyumba 6057 sawa na asilimia 12.1,” alisema Mkuu wa Wilaya huyo.

Aidha, aliongeza kwamba, kupitia Sera ya Taifa ya haki kwa wanawake na watoto wa kike inasisitiza umuhimu wa kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kama njia ya kukuza usawa wa kijinsia na haki za wanawake hivyo maadhimisho hayo yanalenga kuongeza uelewa kuhusu changamoto zinazowakuta wanawake na wasichana kama vile unyanyasaji wa maneno, ukatili wa kijinsia, na ukosefu wa usawa wa kiuchumi.

Kadhalika maadhimisho hayo yanatambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya jamii na kukuza ushirikiano kati ya wanawake na wanaume katika kufikia usawa wa kijinsia na Wanawake wametakiwa kusimama imara katika kutetea haki na usawa wao na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kukuza haki za wanawake na wasichana.

Naye, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Bi. Zainabu Buyogela alisema kuwa, wanawake wanatakiwa kuchangamka na asiwepo hata mmoja anayekosa shughuli inayompatia kipato ili watoe mchango wao katika uongozi na ujasiriamali unaojitokeza katika maeneo yao, na kuwaonya wasichana wasiache kazi kwa ajili ya kulinda ndoa au mahusiano.

Bi. Zainabu alitumia fursa hiyo kumshukuru mwanamke nambari moja Tanzania ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuongoza nchi kwa haki na usawa wa kijinsia.

Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Hassan Abbas Rugwa, alisema kuwa, Mkoa huo unaendelea kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo inayolenga kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuhakikisha wanapata fursa sawa katika uongozi, uamuzi na kushiriki shughuli za maendeleo.

Hata hivyo, Bw. Rugwa aliwahimiza wanawake kuwa wabunifu, kujiamini na kutumia maarifa waliyonayo ili kunufaika na fursa za mikopo, mafunzo ya ujasiriamali pamoja na nafasi za uongozi zinazopatikana katika jamii wanazotoka ili nao kuwa sehemu ya mafanikio katika nafasi hizo.

Aidha, aliwapongeza wanawake na kuishukuru Serikali kuendelea kuweka sera na mikakati mbalimbali inayolenga kuwainua wanawake kiuchumi, kijamii na kisiasa hatua inayochangia kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya Taifa.


Watumishi Wanawake  wa Mahakama Kanda ya Kigoma wakiwa katika picha ya pamoja tayari kwa ajili ya kusherehekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika tarehe 08 Machi, 2026 katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda Wilayani Kakonko.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Valerian Tarimo (aliyevaa sare ya kitenge) akiwa pamoja na Viongozi mbalimbali wa Mkoa wa Kigoma katika sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Wanamke Duniani iliyofanyika Wilaya ya Kakonko katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda.

Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mhe. Dinah Mathamani akitoa hotuba yake wakati wa Sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani zilizofanyika tarehe 08 Machi, 2026 katika viwanja vya ofisi ya kata ya Kasanda.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Abbas Rungwe akitoa neno katika  hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda Wilaya ya Kakonko.

Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania Mkoani Kigoma (UWT), Bi. Zainabu Buyogela akitoa neno wakati wa hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani iliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda  Wilaya ya Kakonko.

Wanafunzi wa Kidato cha Tano wa Shule ya Sekondari Mtendeli iliyopo Kata ya Kasanda wakitumbuiza mbele ya Mgeni Rasmi Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mhe. Dinah Mathamani (hayupo katika picha) wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda Wilaya ya Kakonko.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni