Jumapili, 19 Aprili 2026

BARAZA ELIMU YA SHERIA LAKAGUA MAZINGIRA UTOAJI ELIMU YA SHERIA VYUO VIKUU

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Dar es Salaam na REHEMA AWET-Mahakama, Mwanza

Baraza la Elimu ya Sheria nchini, chini ya Mwenyekiti, ambaye pia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, hivi karibuni lilifanya ziara maalum, kukagua Vyuo Vikuu vitatu, kama sehemu ya juhudi za kuimarisha ubora wa elimu ya sheria nchini.

Wajumbe wa Baraza hilo walifanya ukaguzi katika Chuo cha Kimataifa Kampala, Chuo Kikuu Huria Tanzania na Chuo cha St. Augustine Mwanza.

Ziara hiyo ni sehemu ya mpango mpana wa Baraza la Elimu ya Sheria wa kutembelea na kukagua mazingira ya vyuo mbalimbali nchini ili kuhakikisha elimu ya sheria inatolewa kwa viwango vinavyokubalika na vinavyoendana na mahitaji ya jamii

Akizungumza wakati wa ziara hizo, Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria alisema kuwa lengo kuu ni kukagua na kuboresha mifumo ya ufundishaji, mitaala, pamoja na miundombinu inayotumika kufundishia sheria ili kuhakikisha wahitimu wanakidhi viwango vinavyotakiwa kitaifa na kimataifa.

Alisema kuwa Baraza la Elimu ya Sheria lina jukumu la kusimamia na kudhibiti ubora wa elimu hiyo nchini, hivyo ziara kama hizo ni muhimu katika kubaini changamoto na kuweka mikakati ya kuzitatua kwa kushirikiana na Taasisi husika.

Wakuu wa vyuo hivyo walipongeza ziara hiyo, wakieleza ni fursa muhimu kwao ya kubadilishana mawazo na kupokea ushauri utakaosaidia kuboresha utoaji wa elimu ya sheria.

Katika ziara hizo, Baraza pia lilipata nafasi ya kukutana na Wanafunzi wa kitivo cha sheria vyuoni hapo na kusikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili, pamoja na kupokea mapendekezo yao ya namna ya kuboresha mazingira bora ya kujifunzia ili kuweza kupatikana wanasheria bora.

Baraza pia lilipata wasaa wa kutembelea baadhi ya maeneo katika vyuo vikuu hivyo, ikiwemo Moot Court, Maktaba, Mabweni ya Wanavyuo, Ofisi za Viongozi pamoja na Walimu.

Aidha, Baraza hilo lilifanya mazungumzo na uongozi wa vyuo hivyo na kupokea taarifa ili kuona namna wanavyoweza kuboresha mitaala ili kuendana na soko la ajira.

Pamoja na hayo, Mwenyekiti wa Baraza alishauri namna bora ambayo inaweza kusaidia uhusiano mzuri kati ya vyuo hivyo, Mahakama na Taasisi mbalimbali za elimu katika kuandaa Wanafunzi bora na wenye tija katika soko la ajira.

Mapokezi ya Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini katika Chuo Kikuu cha Kimataifa Kampala.

Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria pamoja na Wanafunzi wa Chuo Kikuu Kampala.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini, Mhe. Dkt Mustapher Mohamed Siyani (katikati), Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kimataifa Kampala, Prof. Honoratha Mushi (tatu kushoto) pamoja na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini.

Mapokezi ya Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini katika Chuo Kikuu Huria Tanzania.

Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria pamoja na Uongozi wa Chuo Kikuu Huria Tanzania.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini akitembelea Maktaba ya Chuo Kikuu cha St. Augustine.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini, Mhe. Dkt Mustapher Mohamed Siyani (katikati), Mkuu wa Chuo cha St. Augustine, Padre. Prof. Juvenalis Asantemungu (tatu kushoto) pamoja na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni