Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.
Mahakama
Dodoma tarehe 17 Aprili, 2026 iliendesha mafunzo ya taratibu za uchukuaji wa
maelezo ya ungamo, yakihusisha Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kutoka Dodoma na
Singida.
Mafunzo
hayo yaliyoendeshwa kwa mfumo mseto, yalifanyika katika ukumbi wa Mahakama
uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.
Baadhi
ya washiriki walihudhuria ana kwa ana ukumbini, huku wengine wakishiriki kwa
njia ya mtandao kupitia kiunganishi maalumu. Hatua hiyo iliwezesha ushiriki
mpana zaidi wa Mahakimu, wakiwemo wale ambao hawakuweza kufika eneo la mafunzo.
Akifungua
mafunzo hayo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt.
Juliana Masabo, alisisitiza umuhimu wa Mahakimu kuzingatia kikamilifu taratibu
za kisheria katika uchukuaji wa maelezo ya ungamo ili kulinda haki na kuhakikisha
ushahidi unaokubalika mahakamani.
“Ubora
wa uamuzi wa Mahakama huanza na ubora wa ushahidi unaowasilishwa, ni wajibu
wetu kuhakikisha kuwa maelezo ya ungamo yanachukuliwa kwa kuzingatia kikamilifu
sheria, miongozo na kanuni zilizowekwa,” alisema Dkt. Masabo.
Katika
hotuba yake, aliwashukuru kwa dhati wawezeshaji wa mafunzo hayo kwa kujitoa
kwao, hususan wale waliowezesha mafunzo kwa njia ya mtandao, akiwemo Naibu
Msajili na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Huduma za Mahakama, Ukaguzi, Mrejesho kwa
Umma na Maadili, Mhe. Maira Kasonde, pamoja na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya
Wilaya ya Mombo, ambaye pia ni mwezeshaji wa mafunzo hayo.
Aidha,
alitambua na kushukuru ushiriki wa Viongozi wa juu wa Mahakama waliohudhuria
kwa njia ya mtandao, akiwemo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Singida,
Mhe. Ayubu Mwenda, ambaye alifuatilia mafunzo hayo kama sehemu ya kuimarisha
utoaji haki katika maeneo yao.
Mafunzo
hayo yalilenga kuwajengea Mahakimu uelewa wa kina kuhusu taratibu sahihi za
kisheria katika uchukuaji wa maelezo ya ungamo, pamoja na kuwapa mbinu bora za
vitendo zitakazosaidia kuepuka makosa ya kiutaratibu yanayoweza kuathiri
ushahidi na uamuzi wa Mahakama.
Kupitia
mafunzo hayo, Mahakimu wamekumbushwa umuhimu wa kufuata miongozo ya sheria
katika kila hatua ya uchukuaji wa maelezo ya ungamo, ikiwemo kuhakikisha
mtuhumiwa anafahamishwa haki zake, kurekodi maelezo kwa usahihi, na
kuthibitisha uhalali wa maelezo hayo kwa mujibu wa sheria.
Mafunzo
hayo yameacha alama muhimu kwa washiriki, yakiwakumbusha wajibu wao mkubwa
katika kulinda haki za Wananchi kupitia uzingatiaji sahihi wa sheria na
taratibu.
Kwa
kuzingatia mabadiliko ya mifumo ya utoaji haki na changamoto zinazoendelea
kujitokeza, utoaji wa mafunzo hayo kwa njia ya ana kwa ana pamoja na mtandao
unaonesha dhamira ya Mahakama ya Tanzania katika kuhakikisha Mahakimu wanakuwa
na uelewa wa kisasa unaokidhi mahitaji ya wakati.
Hatua
hiyo si tu inalenga kuboresha utendaji kazi wa Mahakimu, bali pia inalenga
kuimarisha imani ya jamii kwa Mhimili wa Mahakama, ambapo haki haitolewi tu
bali inaonekana ikitendeka kwa uwazi, weledi na uadilifu.
Akimhitimisha mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Mhe. Zabibu Mpangule, amewashukuru washiriki kwa ushiriki wao mzuri, akisisitiza kuwa mafunzo hayo yatachangia kuleta mabadiliko chanya katika utoaji wa haki na kuongeza ufanisi katika utendaji kazi wa Mahakama.
Meza
kuu ikiongoza na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt.
Juliana Masabo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama
za Mwanzo Dodoma Mjini waliohudhuria mafunzo hayo. Kulia kwake ni Hakimu Mkazi
Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Mhe. Zabibu Mpangule na kushoto kwake
ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Dodoma, Mhe Thurstone Kombe.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni