WATUMISHI IJC DODOMA WANUFAIKA NA MAFUNZO YA USULUHISHI
Na
ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu, Dodoma
Watumishi
wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma wamepatiwa mafunzo maalum
yanayohusu matumizi ya usuluhishi katika kushughulikia migogoro ya kiutawala na
kikazi, ikiwa ni sehemu ya hitimisho la Wiki ya Usuluhishi kwenye Mahakama hiyo.
Mafunzo
hayo yamefanyika leo tarehe 17 Aprili, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano, kuhitimisha
Maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi. Mafunzo hayo yalilenga kuimarisha ufanisi
kazini na kujenga utamaduni wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya mazungumzo.
Mafunzo
hayo yalisimamiwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma na Mratibu wa Wiki
ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, ambaye ametoa elimu ya kina kuhusu
dhana nzima ya usuluhishi na matumizi yake katika mazingira ya kazi.
Amesisitiza
kuwa usuluhishi ni nyenzo muhimu katika kuongeza tija, kuimarisha mahusiano ya
kikazi na kupunguza migogoro isiyo ya lazima katika Taasisi za umma.
Mafunzo
hayo yaliwashirikisha pia Viongozi wa Dini ambao walitoa mchango mkubwa katika
kuelezea nafasi ya usuluhishi kwa mtazamo wa kidini.
Kwa
upande wa dini ya Kikristo, Bw. Ford Saileni
alitoa mafundisho yaliyolenga kuhimiza amani, msamaha na maridhiano kama msingi
wa kutatua migogoro.
Aidha,
kwa upande wa dini ya Kiislamu, Ustadh Bwana Haji kutoka Masjid Sunni Nunge
Dodoma alieleza umuhimu wa suluhu (usuluhishi) kama sehemu ya mafundisho ya
dini, akisisitiza haki, uvumilivu na maelewano katika jamii.
Mafunzo
hayo hayakuwa ya kawaida, bali yalipambwa na shamrashamra mbalimbali
zilizoongeza hamasa kwa washiriki. Vipengele vya maigizo vilivyowasilishwa na
baadhi ya Watumishi pamoja na Wasanii walioalikwa vilionyesha kwa vitendo namna
usuluhishi unavyoweza kutumika katika kutatua migogoro kwa njia ya kirafiki na
yenye tija.
Watumishi
walioshiriki walionesha kufurahishwa na mafunzo hayo, wakieleza kuwa
yamewajengea uelewa mpana zaidi na kuwapa mbinu bora za kushughulikia
changamoto za kikazi. Walibainisha kuwa elimu hiyo ina manufaa makubwa katika
kuboresha utendaji wao pamoja na kuimarisha mshikamano kazini.
Kwa
ujumla, mafunzo hayo yameacha alama chanya kwa Watumishi wa IJC Dodoma,
yakionesha wazi umuhimu wa usuluhishi katika kujenga mazingira bora ya kazi na
utoaji haki wenye ufanisi zaidi.
Ikumbukwe kuwa Wiki ya Usuluhishi nchini yalizinduliwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, tarehe 13 Aprili, 2026. Maadhimisho hayo yalienda sambamba na kaulimbiu isemayo, “Kutumia Njia Mbadala ya Utatuzi wa Migogoro kama Mbinu Inayopendelewa ya Kutatua Migogoro nchini Tanzania.”
Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma,
ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (aliyesimama)
akizungumza wakati wa kutoa mafunzo ya usuluhishi kwa Watumishi wa Mahakama IJC
Dodoma.
Mchungaji Ford Saileni (aliyesimama) akiwasilisha mada ya usuluhishi kwa upande wa dini ya kikristo katika mafunzo ya watumishi wa IJC Dodoma.
Ustadhi Mbwana Haji akiwasilisha mada ya usuluhishi kwa upande wa Kiislamu wakati wa mafunzo ya usuluhishi kwa watumishi wa Mahakama wa IJC Dodoma.
Meza
Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu
wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya
pamoja na washiriki wa mafunzo hayo kutoka Wizara ya Katiba na Sheria. Waliokaa
kushoto kwake ni Ustadh Mbwana Haji kutoka Masjid Sunni Nunge Dodoma na kulia
kwake ni Mchungaji Ford Saileni.
Meza
Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu
wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya
pamoja na washiriki na wakufunzi wa mafunzo hayo ambao ni Mahakimu, Mawakili
pamoja na Watumishi (waigizaji) waliopamba mafunzo hayo ya usuluhishi kwa
watumishi.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.






Hakuna maoni:
Chapisha Maoni