Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama Songwe
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe.
Gabriel Malata, ametoa elimu ya usuhuhishi kwa wadau mbalimbali wa Mahakama katika
ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe ikiwa ni siku ya kwanza ya kuadhimisha
Wiki ya Usuluhishi nchini.
Mhe. Malata alisema kuwa, katika pande mbili zenye
migogoro husuluhishwa na upande wa tatu wa mtu anayejulikana kama msuluhishi
ambapo msuluhishi huyo anaweza kuwa mtu yeyote, Mchungaji, Sheikh, Baraza la Wazee,
Baraza la Kata, au Chombo kingine chochote cha usuluhishi.
Mhe. Malata aliongeza kuwa, usuluhishi unapaswa
kutumika kama njia mbadala ili kutatua migogogoro katika familia, migogoro ya
kibiashara, migogoro mahali pa kazi na migogoro ya kijamii na pia njia hii
imerasimishwa kikatiba, kisheria kikanuni, kimila na desturi, na kwamba siyo
Tanzania pekee, usuluhishi pia hutumika kutatua migogoro mbalimbali ya
kimataifa.
Aidha, Mhe. Malata alieleza faida za kutatua migogoro
kwa njia ya usuluhishi na kusema kupitia usuluhishi unaokoa gharama na muda
kwani usuluhishi huchukua mda mfupi kuliko kesi mahakamani na pia gharama zake
ni ndogo ukilinganisha na ada za mahakamani na mawakili.
Vilevile, usuluhishi humaliza migogoro mapema bila
kuchelewa hivyo kupunguza msongamano wa kesi mahakamani na kupitia usuluhishi
wahusika huzungumza kwa amani na kuelewana hivyo husaidia kudumisha urafiki,
undugu na ushirikiano.
Mhe. Malata alisisitiza suala la msamaha kwani
kusamehe ni agizo kutoka kwa Mungu, kuto kufanya hivyo ni kwenda kinyume na agizo
la Mungu, kwani migogoro haipendezi katika jamii na sio lazima kila mgogoro
umalizwe na msuluhishi au kupelekwa kwenye vyombo vya sheria kwa kufanya hivyo
huongeza gharama zisizo na misingi.
Mhe. Malata aliwasisitiza viongozi wa Dini waendelee
kudumisha upendo, umoja na mshikamano baina ya waumini wao ili waishi kwa
upendo na pia aliwakumbusha viongozi hao kuwa wana wajibu wa kuchunga kondoo
wao vizuri kwani hilo ni jukumu lao walilopewa na Mungu ili kuepusha migogoro
ambayo inaweza kutokea katika jamii.
Aidha, aliwaasa wadau wa usuluhishi kuwa waipokee njia
ya usuluhishi na kutoa elimu kwa wanajamii wote kuhusu usuluhishi kama njia
mbadala ya kutatua migogoro baina ya pande mbili na pia jamii itambue kuwa
usuluhishi au upatanishi ni jambo ambalo lipo kwa mujibu wa dini zetu, Katiba
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kisheria na pia hata katika mila na desturi
zetu.
Mhe. Malata aliwashukuru wajumbe kwa kuhudhuria kikao
hicho na pia aliwashukuru kwa michango yao mizuri yenye kujenga amani, upendeo
na ushirikiano katika jamii.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata, akitoa elimu ya usuhuhishi kwa wadau mbalimbali wa Mahakama (hawapo pichani) ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha wiki ya usuluhishi nchini.
Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Bw. Sostenes
Mayoka (kulia) akiwa katika kikao hicho cha wiki ya usuluhishi nchini.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe
Mhe. Joyce Minde akifuatilia elimu ya Usuluhishi.
Sehemu ya Wadau waalikwa wakisikiliza kwa makini
wakati Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel
Malata (hayupo pichani) akitoa elimu ya usuluhishi.
Sehemu ya Wadau waalikwa wakisikiliza kwa makini
wakati Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel
Malata (hayupo pichani) akitoa elimu ya usuluhishi.
(Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni