Alhamisi, 16 Aprili 2026

WANANCHI SUMBAWANGA WAHAMASISHWA KUTUMIA UPATANISHI KUTATUA MIGOGORO

Na. SHARIFU MOKIWA-Mahakama, Sumbawanga

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga imeungana na Masjala nyingine nchini kuadhimisha Wiki ya Usuluhishi iliyoanza tarehe 13 Aprili, 2026 kwa kutoa elimu kwa wananchi wanaotembelea mabanda yaliyowekwa Mahakama Kuu Sumbawanga na Ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi  Sumbawanga ili kupata elimu ya utatuzi   wa migogoro kwa njia ya upatanishi ikiwa ni sehemu ya kuimarisha utoaji wa haki.

Aidha, wiki usuluhishi inatumia kaulimbiu isemayo “kutumia njia mbadala ya utatuzi wa migogoro kama mbinu inayo pendelewa ya kutatua migogoro nchini Tanzania” kaulimbiu hiyo inasisitiza dhamira ya Mahakama kuhamasisha jamii kutumia njia za usuluhishi katika kutatua migogoro kwa amani.

Akitoa elimu ya usuluhishi Jaji Mfawidhi wa Mahakama wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe.Frederick Manyanda akizungumzia umuhimu wa usuluhishi alisisitiza kuwa ni vyema kufanya usuluhishi kwa sababu unaweza kupoteza kila kitu kwa hoja za kiutaratibu na kisheria lakini ni faida zaidi pale unapokubali kumaliza mgogoro nje ya Mahakama kwa upatanishi.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo aliwahakikishia wananchi kuhusu nguvu ya kisheria ya makubaliano ya usuluhishi baina ya pande zenye mgogoro.

“Tuwatoe hofu kuwa, makubaliano ya usuluhishi yana nguvu ya kisheria na yanaweza kutekelezwa kama ilivyo kwa uamuzi wa Mahakama hivyo yale mtakayokubaliana yana thamani na uhalali wa kisheria,” alisisitiza Mhe. Mazengo

Naye, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa Mhe. Kisasila Saguda akitoa elimu hiyo alisema kuwa, usuluhishi hutoa fursa ya kumaliza mgogoro kwa amani bila kuwepo mshindi au mshindwa, “usuluhishi husaidia kumaliza jambo kwa amani bila kuwa na mshindi wala mshindwa wote mnakuwa washindi kwasababu mmemaliza mgogoro wenu kwa maelewano,” alisema.

Akifafanua sehemu ya mambo Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Sumbawanga Mhe. Yusuph Sakara alisisitiza umuhimu wa usuluhishi katika kujenga maendeleo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii ili kuboresha ustawi wa wananchi.

“Tunataka jamii ipige hatua kimaendeleo, hatuwezi kupiga hatua hiyo kama tunahudhuria mahakamani siku nzima, hatuwezi kuwa na maendeleo tukiwaza tumerundika mashauri mahakamani. Usuluhishi ni jambo jema ukifanyika kwa haraka watu wanapata muda wa kwenda kufanya shughuli nyingine za kimaendeleo,” amesema Mhe. Sankara

Hivyo Mahakama inawahimiza wananchi kujitokeza kushiriki katika wiki ya usuluhishi ili kutatua migogoro kwa njia ya upatanishi, amani na kwa wakati hali itayakayo chochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Katika zoezi hilo Wasuluhishi na Wapatanishi walioteuliwa walipata wasaa wa kushughulikia sehemu ya migogoro iliyowasilishwa na wadau baada ya kupata elimu miongoni mwa migogoro iliyoshughulikiwa ni pamoja na migogoro ya kifamilia, kama vile ndoa ambapo pande husika zilipata fursa ya kusikilizana na kuelekezwa namna ya kufikia makubaliano bila ya kuendelea na mchakato wa kesi mahakamani.

Vilevile zoezi la kutoa elimu ya usuluhishi linaendelea katika Mahakama ya Wilaya Kalambo na Mahakama ya Wilaya Nkasi zilizopo Mkoa wa Rukwa.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Manyanda akieleza umuhimu wa usuluhishi wakati akitoa elimu kwa wananchi wakati wa kuadhimisha wiki ya usuluhishi nchini.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo akizungumza na wananchi waliojitokeza kupata elimu ya usuluhishi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa Mhe. Kisasila Saguda akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi.

Wananchi wakisikiliza kwa makini elimu ya usuluhishi iliyokuwa inatolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Rukwa Mhe. Kisasila Saguda (hayupo pichani)

Msaidizi wa Kumbukumbu Bw. Fredrick Mushi akisulusha wananchi walioamua kumaliza mgogoro wao kwa njia ya usuluhishi.

Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Sumbawanga Mjini Mhe.Yusuph Sakara akitoa elimu kuhusu umuhimu wa usuluhishi katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa


Wananchi wakisikiliza kwa makini elimu ya usuluhishi iliyokuwa inatolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Rukwa Mhe. Kisasila Saguda







 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni