Na MUSSA MWINJUMA-Mahakama, Tanga
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya
Tanga, Mhe. Katarina Mteule, jana tarehe 13 Aprili, 2026 aliongoza kikao cha Baraza
la Wafanyakazi lililofanyika katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Tanga.
Kikao hicho kilihudhuriwa na wajumbe wawakilishi
kutoka sehemu mbalimbali ndani ya Kanda pamoja na wajumbe wengine waalikwa,
wakiwemo Majaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Messe Chaba na Mhe. Happiness Ndesamburo.
Akifungua kikao hicho, Mhe. Mteule aliwashukuru
wajumbe wote kwa kufika pamoja na changamoto za mvua na kuharibika kwa
mindombinu ya barabara. Aidha alisisitiza umuhimu wa kuwepo kwenye kikao na
kila Wilaya kupata uwakilishi.
“Baraza hili lipo kwa mujibu wa sheria na ni maelekezo
ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Baraza ni sauti na ni lazima Watumishi
wapate eneo au vikao rasmi kama hivi ili kutoa maoni ,ushauri na hata
mapendekezo ya namna gani Taasisi yao inaweza kuendeshwa ili kuleta tija na
matokeo Chanya,” alisema.
Aidha, Jaji Mfawidhi alisisitiza umuhimu wa Baraza kuwa
ni kikao mahsusi kinachotoa fursa kwa Watumishi kujenga hoja za kiutendaji, kujua
sera na mipango kupitia taarifa mbalimbali zitakazowasilishwa.
“Nawasihi sana kutoa maoni yenu kwa uhuru na maoni ya
mnaowawakilisha hapa; usitoe maoni yako binafsi ukaacha ya wale
unaowawakilisha, na ni vyema baada ya kikao hiki twende tukawape mrejesho wale
wenzetu ambao hawapo hapa, hii itatusaidia kujenga mshikamano ,” alisisistiza Jaji
Mteule.
Akizungumza Katika Baraza hilo, Ofisa Kazi Mwandamizi
kutoka Idara ya Kazi jijini Tanga, Bi Diana Chacha, aliwaasa wajumbe juu ya
usiri wa taarifa za Baraza na taarifa binafsi ndani ya kikao.
“Usiri wa Baraza ni muhimu sana kwa taarifa za Taasisi
na taarifa binafsi, usitoe siri za Baraza kwani kinachoamuliwa kinabaki kuwa
maazimo ya kikao,” alisema.
Taarifa mbalimbai za mashauri na kiutendaji
ziliwasilishwa na wajumbe walipata fursa ya kujua hali ya mashauri pamoja na
mipango ya baadaye ya Kanda kwenye masuala ya miundombinu, maslahi, afya za Watumishi
na michezo.
Akifunga kikao hicho, Mhe. Mteule aliwashukuru wajumbe
kwa michango yao mizuri yenye kujenga, lakini alitoa rai juu ya kujenga
utamaduni wa kusikiliza hotuba za Viongozi wa Taasisi. Alisema kuwa ndani ya hotuba
hizo kuna majibu ya maswali mengi ambayo huwa wanajiuliza bila kupata majibu.
“Najua mambo ni mengi, lakini nawaomba Watumishi
tujenge utamaduni wa kusikiliza hotuba za Viongozi wetu ili kujua maboresho
mbalimbali yanayofanywa kwa maslahi yetu kama Taasisi,” alisema.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni