Jumanne, 21 Aprili 2026

JAJI MWAIPOPO AONGOZA KIKAO CHA KUSUKUMA MASHAURI IJC TEMEKE

  • Wajumbe wadhamiria mifumo ya Mahakama, Wadau kusomana kupunguza udanganyifu

Na HIGHNESS TERRY-Kituo Jumuishi cha Masuala Familia,Temeke

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo, hivi karibuni aliwaongoza Mahakimu na Wadau mbalimbali wa Mahakama katika kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai.

Kikao hicho (Bench Bar Meeting) kilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano katika kituo hicho na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbalimbali wa Mahakama, akiwemo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Frank Moshi, aliyekuwa Katibu wa Kikao.

Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Kituo Jumuisgi Temeke, Bw. Samson Mashalla, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Watoto, Mhe. Mwamini Kazema, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya, Mhe. John Msafiri na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo, Mhe. Upendo Kapama.

Walikuwepo pia Wajumbe wa Sekretarieti kutoka IJC Temeke pamoja na Wadau mbalimbali wa huduma za kimahakama kutoka PSSSF, RITA, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Msajili wa Hati, Mwakilishi kutoka Benki Kuu ya Tanzania, Mwakilishi kutoka Benki ya CRDB na wawakilishi kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC).

Akizungumza katika ufunguzi wa Kikao hicho, Mhe. Mwaipopo alisema kuwa ni jukumu la Mahakama kushirikiana kwa karibu na Wadau katika utekelezaji wa majukumu.

“Katika kusimamia mpango mkakati wake wa kumaliza mashauri ya mlundikano, Mahakama katika Kituo Jumuishi Temeke inatambua umuhimu mkubwa wa Wadau kwenye utekelezaji wa majukumu yetu. Tunawaalika Wahusika na Wadau wote ambao majukumu yao yanaathiri utendaji wa kazi tushirikiane ili kupunguza au kumaliza kabisa mashauri mlundikano,” aliongeza Mhe. Mwaipopo.

Aidha, katika kikao hicho, Wadau walipata taarifa katik ya robo ya tatu ya mwaka iliyowasilishwa na Katibu, ambaye pia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Frank Moshi, na kuona takwimu za hali ya mashauri kutoka Mahakama Kuu, Mahakama ya Watoto, Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo.

Wakati wa wasilisho hilo, wajumbe pia waliweza kufahamu sababu zilizochangia kutokumalizika kwa wakati mashauri katika Mahakama zote na walipata nafasi ya kutoa maoni yao.

Naibu Msajili alieleza changamoto kubwa upande wa mirathi kuwa na muda mrefu wa kufuatilia mashauri hayo pamoja na kuchelewa kufunga mirathi kwa wakati.

Aidha, alieleza changamoto kubwa ya utekelezaji kuwa ni muda mrefu wa upatikanaji wa wanunuzi wa mali za ndoa pamoja na utathimini wa thamani wa mali husika.

Wajumbe wa kikao walijadili mambo mbalimbali, ikiwemo tatizo la uhamishaji wa hati za umiliki kwenda kwa warithi pamoja na uhamishaji wa hisa na vipande kutoka kwenye Taasisi za Waadau.

Suluhisho lililotolewa ni kuomba uboreshaji wa mifumo ya Mahakama na Wadau wake kusomana, lakini pia kuongeza uelewa kwa wateja wanohudumiwa juu  ya ufuatiliaji wa stahiki hizo.

Pia kulikuwepo na majadiliano kuhusu kuchelewa kufunga mashauri kutoka Mahakama ya Watoto, ambapo sababu iliyobainishwa ni kuchelewa kwa majibu ya vinasaba (DNA) kutoka ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, huku upande wa Mahakama Kuu, sababu iliyotolewa ni kuwepo kwa amri ya Mahakama ya kufungua shauri upya baada ya makosa kufanyika.

Kulikuwepo pia na  changamoto ya suala la kubadilisha majina ya umiliki wa ardhi iliyobainishwa, jambo linalosababisha kupita muda wa kusikiliza mashauri uliowekwa kwenye kadi kipimo, ambayo ni siku 60 kwa Mahakama ya Mwanzo na Watoto, Siku 90 kwa Mahakama ya Wilaya na Siku 120 kwa Mahakama Kuu.

Ofisa Sheria kutoka RITA, Bi.Janeth Mandawa, aliongeza kuwa kuna changamoto ya wateja kuvutana juu ya nani kupata mali zisizohamishika na zinazoamishika kutokana na usheleweshaji katika uhamishaji wa umilik wa ardhi.

Alisisitiza kuwa ni muhimu ujumbe wa vikao kama hivyo kufika katika ofisi zote zinazohusika na taratibu za uhamishaji wa umiliki wa ardhi.

Hakukuwepo na mjumbe kutoka Ofisi ya Mkemia Mkuu ili kuleta majibu katika hoja ya miongozo inayohitajika kwa ajili ya upimaji wa vinasaba (DNA) kutokana na udhuru wa kuomba muda kwa ajili ya taratibu ya kuandaa orodha itakayotumika kwa nchi nzima.

 Akijibu hoja hiyo, Mjumbe wa Halmashauri ya Kigamboni alieleza kuwa ,“Sisi bado tupo kwenye majadiliano na pia tumeanzisha mradi wa kutengeneza hati miliki kwa awamu na kuendelea na zoezi la upimaji wa ardhi kwa maeneo ambayo hayajapimwa.

“…tumewasiliana na Ofisi ya Ardhi na tayari hoja hii imepelekwa katika Baraza la Madiwani ili kujadili namna bora ya kutoa uhakiki wa taarifa maalum za umiliki ili kutatua changamoto hii.”

Mjumbe huyo aliongeza kuwa ni muhimu kuwepo na mfumo unaosomana ili kuwezesha kesi zilizopo mahakamani na zenye kuhitaji uhamishaji wa umiliki ardhi zitumwe na Mahakama katika mfumo husika ili kufanyiwa kazi kwa haraka na kuepusha mashauri kukaa muda mrefu bila kumalizika.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo, akitoa neno la ufunguzi wa Kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai kilichofanyika hivi karibuni. Kulia ni Katibu wa Kikao na Naibu Msajili, Mhe. Frank Moshi na kushoto ni Mtendaji, Bw. Samson Mashalla.

Katibu wa Kikao na Naibu Msajili, Mhe. Frank Moshi, akitoo ufafanuzi katika kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai.

Ofisa kutoka Banki Kuu ya Tanzania akitoa ufafanunuzi juu ya orodha ya mahitaji ili kuhamisha umiliki wa hisa au vipande kutoka kwa marehemu kuja kwa warithi.

Wajumbe wa Kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai ambao ni wadau wa Mahakama kutoka Taasisi mbalimbali wakisikiliza kwa makini wasilisho kutoka kwa Naibu Msajili na Katibu wa Kikao, Mhe. Frank Moshi (hayupo pichani).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni