Jumanne, 21 Aprili 2026

MENEJIMENTI YA MAHAKAMA KITUO JUMUISHI TEMEKE YAFANYA KIKAO

Na HIGHNESS TERRY-Kituo Jumuishi cha Masuala Familia,Temeke

Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, hivi karibuni ilifanya kikao cha menejimenti kujadili mambo mbalimbali ya kiuntendaji.  

Kikao hicho kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo hicho kilihusisha uongozi wa Mahakama pamoja na watumishi wa vitengo mbalimbali kwa lengo la kupokea na kujadili taarifa za utekelezaji wa majukumu, kupima mafanikio, kuchambua changamoto na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji wa mahakama.

Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Sarah Mwaipopo, aliongoza kikao hicho kusisitiza umuhimu wa uwajibikaji, ushirikiano na uadilifu katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku ya utoaji haki.

Katika kikao hicho, wajumbe walipokea taarifa ya kipindi cha Januari hadi Machi 2026 kutoka kwa Ofisa Utumishi wa Mahakama, Bi. Jennifer Malisa, aliyekuwa mjumbe wa kikao hicho.

Alieleza kuwa Mahakama katika Kituo Jumuishi Temeke imeendelea kufanya kazi kwa ufanisi katika maeneo mbalimbali ya utoaji huduma kwa wateja wanaofika mahakamani hapo, hivyo kuelezea mafanikio, changamoto na mikakati iliyofanywa katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita.

Moja ya mafanikio makubwa ni kuendelea kuboreshwa kwa huduma za usikilizaji wa mashauri kwa kutumia teknolojia na huduma za Mahakama Inayotembea zilizoanzishwa katika Wilaya zote kwa Dar es salaam, hali iliyosaidia kupunguza gharama na muda kwa wahusika walioko mbali na Kituo.

“Mifumo ni jjambo endelevu  na lenye tafsiri pana, ambapo bado tunaendelea kufanyia kazi katika kubuni ili kurahisisha ufanisi wa kazi,” aliongeza Bw. Fredrick Kachenje, katika kuelezea mafanikio na umuhimu wa TEHAMA katika jukumu zima la kutoa haki kwa Watanzania.

Pamoja na hayo, Mtendaji wa Mahakama Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samsoni Mashalla, alileza juhudi wanazozifanya katika kupeleka wataalamu wa TEHAMA kupata mafunzo kwa Mahakama nyingine, ikiwemo matumizi yasiyo na karatasi ili kuchukua ujuzi.

Aidha, Mahakama imefanikiwa kuimarisha mifumo ya kiutawala na usimamizi wa mashauri kwa kuongeza ufanisi katika utendaji wa kila siku. Watumishi wameendelea kupatiwa mafunzo mbalimbali ya kujenga uwezo na kuboresha utoaji huduma ndani nan je ya kituo.

Halikadhalika, Mtendaji alieleza juu ya mafunzo yanayotolewa kwa wateja nje na na ndani ya kituo kwa ajili ya kuogeza uelewa juu ya haki zao na upatikanaji wa haki unaotolewa kituoni hapo.

Katika upande wa miundombinu, baadhi ya marekebisho ya vitendea kazi na majengo yamefanyika, pamoja na ukarabati wa vyombo vya usafiri na vifaa vya ofisi, huku jitihada za kuboresha mazingira ya kazi zikiendelea.

Licha ya mafanikio yaliyopatikana, kikao kilibaini changamoto mbalimbali zinazoathiri ufanisi wa utoaji huduma za Mahakama. Changamoto kubwa ni upungufu wa Watumishi na vitendea kazi, hali inayoathiri mazingira ya kazi na ufanisi wa Watumishi.

Mtendaji alieleza pia ufinyu wa bajeti ambao umeathiri utekelezaji wa baadhi ya shughuli muhimu ikiwemo matengenezo ya vifaa, ununuzi wa vitendea kazi na kuboresha miundombinu ya ofisi.

Changamoto nyingine ni katika usimamizi wa mirathi ambapo baadhi ya mirathi hazifungwi kwa wakati, pamoja na changamoto za usimamizi wa fedha zake katika akaunti ya mirathi iliyoko mahakamani hapo kuendelea kupokea fedha.

Kaimu Jaji Mfawihidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo akiongoza kikao cha menejimenti.

 

Mtendaji wa Mahakama Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samson Mashalla, aliyekuwa Katibu katika kikao hicho akifafanua jambo.

Ofisa TEHAMA, Bw. Fredrick Kachenje, akifanya wasilisho juu ya mafanikio ya mifumo ya TEHAMA katika kipindi cha robo ya tatu ya mwaka katika kikao hicho.

 

Wajumbe wa menejiment wakisikiliza mawasilisho katika hicho.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni