Jumanne, 21 Aprili 2026

SERIKALI YAENDELEA KUBORESHA MAJENGO YA MAHAKAMA NCHINI

  • Ujenzi, ukarabati kufanyika kwa awamu kusogeza huduma za haki karibu na wananchi

Na HALIMA MNETE- MAHAKAMA DODOMA.

Serikali imesema inaendelea kutekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama nchini ili kuboresha utoaji wa huduma za haki kwa Wananchi.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 21 Aprili, 2025 jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba, wakati akijibu maswali ya Wabunge katika kikao cha Bunge la Kumi na Tatu jijini Dodoma kuhusu hali ya miundombinu ya Mahakama.

Amesema kuwa Mahakama ya Tanzania inaendelea kutekeleza ujenzi na ukarabati wa majengo kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi 2025/2026, kufuatia kuwepo kwa uhaba wa majeng,o hususan Mahakama za Mwanzo katika maeneo mbalimbali nchini.

Naibu Waziri ameeleza kuwa utekelezaji huo unafanyika kwa awamu, ambapo kwa sasa Serikali inakamilisha maandalizi ya awamu ya tatu ya mpango huo wa ujenzi na ukarabati wa majengo ya mahakama.

Katika swali la msingi, Mbunge wa Nanyamba, Abdallah Chikota, alihoji kuhusu mpango wa Serikali kujenga Mahakama ya Mwanzo katika Wilaya hiyo, huku akishauri pia kujengwa kwa nyumba za Watumishi wa Mahakama ili kuboresha mazingira ya kazi.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri alisema kuwa ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo wilayani Nanyamba utazingatiwa katika mpango wa awamu ya tatu.

Aidha, Mbunge wa Tunduru Kaskazini, Ado Shaibu Ado, aliuliza swali la nyongeza akitaka kufahamu sababu za kusimama kwa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya hiyo kwa takribani miezi mitano na ni lini utakamilika.

Katika majibu yake, Mhe. Katimba alisema kuwa mradi huo upo katika awamu ya pili ya utekelezaji na tayari mkandarasi yupo eneo la kazi akiendelea na ujenzi, huku Serikali ikiwa na dhamira ya kuhakikisha Wananchi wanapata majengo ya kisasa yatakayowezesha upatikanaji bora wa haki.

Kwa upande wake, Mbunge wa Muleba Kaskazini, Mhe. Adonis Alfred Bitegeko, alihoji lini jengo la Mahakama ya Wilaya hiyo litaboreshwa kutokana na changamoto ya uchakavu na ufinyu wa nafasi.

Akijibu, Naibu Waziri alisema kuwa Serikali ina mpango wa kuboresha jengo hilo ili Wananchi wa Muleba waweze kupata huduma za mahakama katika mazingira bora zaidi.

Naye Mbunge wa Kiteto, Mhe. Edward Ole Lekaita, aliitaka Serikali kueleza lini ujenzi wa Mahakama ya kisasa katika Wilaya hiyo utaanza.

Katika majibu yake, Mhe. Katimba alisema kuwa tayari mchakato wa kumpata mkandarasi umeanza baada ya kutangazwa kwa zabuni, na hatua zilizopo sasa ni za majadiliano ya mkataba ili kuruhusu kuanza kwa ujenzi huo.

Serikali imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuhakikisha inaboresha miundombinu ya Mahakama nchini ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki na kupunguza changamoto zinazowakabili Wananchi katika kupata huduma hiyo muhimu.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba, akisisitiza jambo wakati anajibu maswali ya Wabunge katika kikao cha Bunge la Kumi na Tatu jijini Dodoma.



Bunge la Kumi na Tatu likiendelea na shughuli zake jijini Dodoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni