Jumanne, 21 Aprili 2026

KIKAO CHA BARAZA LA WANYAKAZI KITUO JUMUISHI TEMEKE CHAFANYIKA

Na HIGHNESS TERRY-Kituo Jumuishi cha Masuala Familia,Temeke

Kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke limefanyika hivi karibuni kujadili ustawi wa Watumishi, tathmini ya utekelezaji wa maazimio yaliyopita, pamoja na kupanga mikakati ya kuboresha utendaji kazi wa Taasisi.

Kikao hicho kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo hicho kilikuwa jukwaa muhimu la majadiliano ya wazi kati ya uongozi na Watumishi, kikilenga kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ushirikishwaji katika masuala ya kiutumishi.

Kikao hicho kiliongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Sarah Mwaipopo. Katika hotuba yake ya ufunguzi, alisisitiza umuhimu wa Baraza kama chombo cha kushauri na kuimarisha mahusiano kazini.

Mhe. Mwaipopo alieleza kuwa, “Baraza hili ni jukwaa la kujenga Taasisi yetu kwa pamoja, hivyo mawazo yenu ni msingi wa maboresho tunayoyahitaji.

Katika kikao hicho, kulikuwepo pia na ajenda ya uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza. Hivyo aliwashukuru na kuwaaga Viongozi wa Baraza waliopita, Bi. Fatuma Jumbe, aliyekuwa Katibu na Bw. David Mbago, aliyekuwa Katibu Msaidizi.

Zoezi la uchaguzi lilisimamiwa na Ofisa Kazi, Bw. Hussein Mwamba, ambaye alisisitiza taratibu za uchaguzi kuwa wazi na shirikishi kwa wajumbe kwa mujibu wa Mkataba. 

Baada ya wajumbe kupiga kura, Bw. David Mbago alichaguliwa kuwa Katibu mpya wa Baraza, huku Bi. Fatuma Jumbe akawa Katibu Msaidizi. Bi.Doroth Ndunguru alichaguliwa kuwa Mwakilishi TUGHE.

Katika tathmini ya utekelezaji wa maazimio ya kikao kilichopita, Baraza liliridhishwa kubaini kuwepo kwa hatua kadhaa chanya zinazoonesha juhudi za uongozi katika kuboresha ustawi wa Watumishi na ufanisi wa utendaji kazi.

Pamoja na mafanikio yaliyopatikana, Baraza lilibaini kuwepo kwa changamoto kadhaa zinazoendelea kuathiri utekelezaji wa maazimio na ufanisi wa kazi kwa ujumla. Changamoto hizo zinahitaji kushughulikiwa kwa umakini ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Watumishi waliibua hoja ya kuchelewa kupandishwa madaraja, hususan kwa wale walio kwenye ajira za muda mrefu. Katika mjadala, ilisisitizwa kuwa Watumishi wanapaswa pia kujitahidi kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo. Aidha, wajumbe walisisitiza umuhimu wa kutoa elimu kuhusu Miundo ya Utumishi ili kuondoa mkanganyiko.

Baraza linasisitiza umuhimu wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana huku likichukua hatua za haraka na za kimkakati kushughulikia changamoto zilizobainika.

Katikati ni Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo, aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi. Kushoto ni aliyekua Katibu wa Baraza, Bi. Fatuma Jumbe na kulia ni aliyekua Katibu Msaidizi, Bw. David Mbago.

 Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi, Bw. Hamisi Some, akichangia Hoja katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi.

Bw. David Mbago aliyekuwa Katibu Msaidizi akiwashukuru wajumbe kwa nafasi ya kuwatumikia.

Katibu na Katibu Msaidizi wakiwashukuru wajumbe kwa kuwapigia kura za kuwachagua katika awamu nyingine ya uongozi.

Bwana Hussein Mwamba, mjumbe kutoka Baraza Kuu la Wafanyakazi katika kusimamia zoezi la uchaguzi wa Katibu, Katibu Msaidizi na Mjumbe Mwakilishi katika Baraza la TUGHE.

Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi waliohudhuria.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni