Alhamisi, 2 Aprili 2026

JAJI NONGWA ATETA NA WADAU WA MAHAKAMA NJOMBE

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa amekutana na wadau wa Mahakama Taasisi mbalimbali zinazotoa huduma kwa wananchi ndani ya Kanda hiyo ili kuteta nao juu ya uanzishwaji wa shughuli za Mahakama Kuu Njombe

Akizungumza na wadau hao tarehe 30 Machi, 2026 aliwaeleza kuwa, Mahakama Kuu Kanda ya Njombe imeanza kufanya kazi Jumatatu tarehe 30 Machi, 2026.

Aidha, Mhe. Nongwa alisema kuwa, kuanza kazi kwa Mahakama hiyo kulianza kwa kufunguliwa kwa dirisha la kusajili mashauri. Hivyo, aliwaeleza Wadau wa Mahakama kuwa, lengo la kikao hicho ni kuzungumza kwa pamoja na kupeana ushauri katika kukabiliana na changamoto mbalimbali.

Pamoja na kushauriana na kufafanua zaidi pale penye changamoto za usikilizwaji mashauri kwa njia ya kieletroniki wakati yanapokatiwa rufaa, Jaji Nongwa ameomba ushirikiano wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) hasa kwa mashauri ya mauaji.

Kuhusu Baraza la Kata la Nyumba na Ardhi, Mhe. Nongwa amewasisitiza kuhusu mfumo wao ambao bado haujaungana na Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) hivyo, Baraza hilo litatakiwa kuwa na nakala laini pindi zinapohitajika mahakamani.

Kwa upande wa Madalali wa Mahakama, Jaji Mfawidhi huyo amewataka kufuata sheria kwenye mashauri yanayokaziwa hukumu kwa kuwa mashauri hayo yana hatua mbalimbali.

Alielezea jinsi ya ufunguaji wa mashauri kwa njia ya kieletroniki ya kutotumia karatasi (paperless) kwenye dirisha dogo la ufunguaji wa mashauri kupitia Mfumo wa Kieletroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) la Masjala ndogo ya Mahakama Kuu Kanda ya Njombe iliyoanza kutoa huduma zake kuanzia Siku ya Jumatatu tarehe 30 Machi, 2026.

Kwa upande mwingine Jaji Nongwa alisisitiza umoja na mshikamano kwa Mawakili na kwa  Taasisi nyingine za Haki Jinai ili waweze kutoa huduma kwa wateja ambao ni wananchi kwa weledi na ufanisi hasa kwa kutoa kipaumbele kwa wateja walio kwenye makundi maalum mfano kwa akinamama wajawazito, wazee na akina Mama wenye watoto wadogo.                                                                                     

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Bw. Richard Mbambe kwa pamoja waliwashukuru Wadau wa Mahakama Kwa utayari wa kufika kwa ajili ya kumsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa na kuhaidi kuendeleza ushirikiano.

Wadau  walioshirikiki katika kikao  hicho ni  Ofisi ya  Mwendesha Mashtaka Mkoa wa Njombe, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa Njombe (RCO), Baraza La Nyumba na Ardhi, Mawakili wa Kujitegemea pamoja na Wawakilishi wa Taasisi mbalimbali kutoka Mkoa wa Njombe ambao walichangia hoja mbalimbali kwa pamoja juu ya uendeshaji wa Masjala ndogo ya Mahakama Kuu Njombe.

 Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania  Kanda ya Njombe,  Mhe. Victoria Nongwa akizungumza na Wadau wa mkoani Njombe. (hawapo katika picha) tarehe 30 Machi, 2026.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano  akizungumza na Wadau na Mawakili wa Mkoa wa Njombe (hawapo katika picha).

       Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu mkazi Mkoa Njombe Mhe. Liadi Chamshamu akitoa neno la shukrani kwa Wadau (hawapo katika picha) walioshiriki katika kikao.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Njombe, Bw. Richard Mbambe  akitoa neno la shukrani kwa wadau wa Mkoa wa Njombe. Nyuma yake ni Ofisa Utumishi, Bi. Happy Merere pamoja na wadau wengine waliohudhuria katika kikao hicho.

Wadau wa Mahakama pamoja wakifuatilia kinachojiri katika kikao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama mkoani humo. Aliyeketi kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano na kulia ni Mtendaji Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Bw. Richard Mbambe.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)

 

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni