Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama Mbeya
Mahakama
Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya imefanya kikao cha kusukuma mashauri ya jinai
kilichoongozwa na Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe.
Aziza Temu kwa lengo la kuimarisha usimamizi na ufanisi wa utoaji haki kwa
wakati mapema ipasavyo.
Akizungumza
katika kikao hicho Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, alibainisha
kuwa azimio la kuhakikisha mashauri ya mlundikano hayavuki Desemba 2025
limefanikiwa kwa kiasi kikubwa, huku juhudi za kupunguza vielelezo mahakamani
hasa dawa za kulevya, zikiendelea kwa kushirikiana na vyombo husika ili
kuharakisha uteketezaji wake.
Akiwasilisha
taarifa ya Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Aziza Temu alieleza kuwa, kwa sasa
hakuna mashauri ya mlundikano kwa Mahakama Kuu Mbeya na kwa Mahakama za chini
ni machache ambayo yamebaki kwa sababu maalumu ambapo mengine yanasubiri
maamuzi ya Mahakama ya Rufani. Aliongeza kuwa, Mahakama Kuu imeweka rekodi mpya
kwa kumaliza mashauri yote ya mlundikano.
Kikao
pia kilipokea taarifa ya ujio wa Wahe. Majaji na watumishi wengine wa Mahakama
ya Rufani mwezi Aprili 2026, pamoja na kuanza kwa vikao vya kesi za mauaji
Mahakama Kuu Mbeya kuanzia tarehe 13 Aprili 2026.
Aidha,
ilibainishwa kuwa, kutokana na kujitenga kwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mkoa
wa Songwe, kutasaidia kupunguza mzigo wa mashauri katika Kanda ya Mbeya na
idadi ya wafungwa na mahabusu katika Gereza Kuu la Ruanda Mbeya.
Kwa
upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe.
Zawadi Laizer, akiwasilisha taarifa ya Mahakama Mkoa wa Mbeya, alizungumzia
kuhusu jitihada za Mahakama kusimamia utoaji wa haki mapema ipasavyo:
“Kufuatia
maelekezo ya Jaji Mkuu, mashauri yanapaswa kumalizika ndani ya miezi sita kwa
Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya na miezi mitatu kwa Mahakama za Mwanzo. Sote
tushirikiane kuhakikisha kwamba ukomo huu unazingatiwa” alisema Mhe. Laizer
Vilevile,
Mhe. Laizer alisisitiza umuhimu wa taarifa za Wafungwa na Mahabusu hususan
utoro wa Mahabusu na wafungwa walio chini ya ulinzi halali, kufikishwa mapema
mahakamani ili kuisaidia Mahakama katika kuandaa usikilizwaji wa mashauri
mbalimbali.
Katika
maazimio ya kikao hicho ilikubaliwa kuwa, taarifa muhimu za wafungwa, ikiwemo
utoro, vifo, msamaha wa Rais au kumaliza kifungo, ziwasilishwe kwa wakati mahakamani
ili kusaidia katika upangaji wa Vikao vya kusikiliza mashauri, ili mashauri
yote yamalizika ndani ya miezi sita tangu kusajiliwa kwake na yaliyovuka muda
huo yapewe kipaumbele yakamilike kabla au ifikapo Juni 2026.
Kikao
hicho kilihudhuriwa na wadau wa mnyororo ya haki jinai wakiwemo Wahe. Mahakimu
Mkoa wa Mbeya, Magereza, Polisi, Ofisi ya Upelelezi, Ofisi ya Mdhibiti Mali za
Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Mbeya (NPS), Ustawi wa Jamii,
Mawakili wa Serikali, Mawakili wa Kujitengemea (TLS), Idara ya Marekebisho ya
Tabia na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Mwenyekiti wa kikao hicho ambaye pia ni Naibu Msajili
Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (kushoto), akiendesha
kikao hicho wakati wa kuwasilisha taarifa ya Mahakama Kuu Mbeya.
Mwakilishi wa Mkuu wa Gereza Kuu Ruanda Afisa Magereza
akizungumza jambo katika kikao hicho.
Sehemu ya wadau walioshiriki kikao hicho.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi
Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, akiwakilisha taarifa ya Mkoa wa Mbeya ikijumuisha
Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mahakama za Wilaya na Mahakama zake za Mwanzo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni