Jumatano, 1 Aprili 2026

MAHAKAMA MUSOMA YAFANYA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama Musoma.

Mahakama Kanda ya Musoma hivi karibuni, imefanya mkutano wa Baraza la Wafanayaka kwa mwaka 2026 na kujadili masuala mbalimbali ya kiutendaji.

Akifungua Baraza hilo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. Fahamu Mtulya, aliwasisitiza wajumbe wote kuwa huru kueleza changamoto zao.

Mhe. Mtulya alisema kuwa sehemu ya kutatua changamoto zilizo ndani ya uwezo wa Kanda ni katika Baraza hilo na zile zilizo nje ya uwezo wa Kanda zichukuliwe na kuwasilishwa kwa Mwajiri.

Alisema Baraza la Wafanyakazi ndio sehemu muhimu ambayo Watumishi wanapata nafasi ya kuongea na Mwajiri pamoja na Wawakilishi wa Chama cha Wafanyakazi, yaani TUGHE, ili kupata ufumbuzi wa changamoto wanazokutana nazo lakini pia kujua nini Mwajiri na Serikali kwa pamoja wanafanya ili kuboresha mazingira ya kazi.

Naye katibu wa TUGHE Mkoa wa Mara, Bw. Hamis Mwisa, alipata wasaa wa kuelezea na kutoa elimu juu ya mkataba mpya wa Baraza la Wafanyakazi na kutoa pongezi kwa namna ulivyoweza kuainisha wajumbe ambao wanabeba uwakilishi mzuri wa Watumishi, jambo litakaloongeza ufanisi na uwazi katika Mabaraza ya Wafanyakazi.

Aidha, Mjumbe wa Baraza Kuu Serikalini anayeteuliwa na TUGHE Makao Makuu, Dkt. John Bomani, alimpongeza Mwenyekiti wa Baraza kwa namna anavyoliendesha kwa kuzingatia kanuni za demokrasia na kuruhusu uhuru wa maoni.

Alisema kuwa mwenendo huo wa uwazi ni kiashiria cha mahusiano mazuri kati ya Viongozi na Watumishi, jambo ambalo linasaidia katika kuweka mazingira bora na rafiki ya kazi.

Katika mkutano wa Baraza hilo, wajumbe walipata nafasi ya kuelezwa kilichojiri katika Baraza la mwaka 2025 pamoja na matokeo ya hoja zilizowasilishwa. Pia walieleza hoja mbalimbali ambazo zilikubalika zichukuliwe na kuwasilishwa kwa Mwajiri katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.

Pamoja na hayo, katika Baraza hilo wajumbe walipitishwa katika taarifa mbalimbali za kiutendaji, ikiwemo taarifa ya bajeti inayoendelea ya mwaka wa fedha 2025/2026 pamoja na makisio ya bajeti ijayo ya mwaka 2026/2027, huku majukumu yaliyopangwa kutekelezwa kwa kila ngazi ya Mahakama ndani ya Kanda yakianishwa.

Vilevile, wajumbe wa Baraza hilo walipata nafasi ya kupendekeza na kuchagua mtumishi hodari wa Mahakama Kanda ya Musoma, zoezi lililosimamiwa na Mwenyekiti wa Baraza hilo.

Akihitimisha Baraza hilo, Mwenyekiti aliwashukuru na kuwapongeza Watumishi kwa namna walivyowasilisha hoja zao, pamoja na Viongozi wa TUGHE Mkoa wa Mara, hususan Katibu, Bw. Hamis Mwisa, kwa namna anavyojitoa kushiriki katika vikao na kutoa elimu kwa wajumbe juu ya masuala mbalimbali, ikiwemo elimu ya Mabaraza ya Wafanyakazi.

Viongozi na wajumbe wa mkutano wa Baraza la Wafanyakazi, Kanda ya Musoma, wakiimba kwa pamoja wimbo wa mshikamano daima wakati wa ufunguzi.

Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Musoma, Bw. Kandana Lucas, akisema neno wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika hivi karibuni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, akisisitiza jambo wakati wa mkutano huo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati), Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Musoma, Bw. Kandana Lucas (kushoto) pamoja na Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi Musoma, Bi. Teckla Patrick, wakihesabu kura za wajumbe wakati wa zoezi la kuchagua mtumishi hodari wa Kanda ya Musoma.

Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi, Bw. Simo Lubili (aliyesimama) akiwasilisha taarifa ya kikao cha Baraza la Wafanyakazi la mwaka 2025 pamoja na majibu ya hoja zilizowasilishwa mwaka huo.

Katibu wa TUGHE Mkoa wa Mara, Bw. Hamis Mwisa (aliyesimama) akifafanua mkataba mpya wa Baraza la Wafanyakazi wakati wa mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma.

Mjumbe wa Baraza Kuu Serikalini, Dkt. John Bomani, akitoa ufafanuzi wa jambo wakati wa mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni