Jumatano, 1 Aprili 2026

MAHAKAMA ZA MWANZO TATU KANDA YA MTWARA ZAZINDULIWA

Na SOJO STEPHEN-Mahakama, Mtwara

Mahakama za Mwanzo tatu zilizokuwa zinajengwa ndani ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, zimezinduliwa katika jitihada za kusogeza huduma za haki karibu zaidi na Wananchi, hasa waliopo katika maeneo ya vijijini.

Uzinduzi huo wa pamoja ulifanyika tarehe 27 Machi, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Chikundi kwa niaba ya Mahakama nyingine za Mwanzo Kitangari na Newala Mjini na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali pamoja na Wadau wa sekta ya sheria.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, akiwa ameambatana na Naibu Msajili, Mhe. Seraphine Nsana na Mtendaji wa Mahakama ya Mtwara, Bw. Yusuph Msawana.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Kakolaki alisema kuwa kuanzishwa kwa Mahakama hizo kutasaidia kupunguza msongamano wa mashauri na kuharakisha utoaji wa haki kwa Wananchi.

Alisisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Mahakama na Serikali kuhakikisha kila Mwananchi anapata haki kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Aidha, aliwahimiza Wananchi kutumia Mahakama kama njia sahihi ya kutafuta haki, badala ya kutumia mbinu au sheria zisizo sahihi ambazo zinaweza kusababisha migogoro zaidi.

Vilevile, aliwasihi Wananchi na Watendaji wa Mahakama kutumia mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha shughuli za Mahakama, kuharakisha utoaji wa huduma na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mashauri.

Mhe. Kakolaki aliwashukuru Wananchi, Viongozi wa Serikali pamoja na Wadau mbalimbali wa kijamii kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki uzinduzi wa Mahakama hizo zilizozinduliwa katika maeneo ya Chikundi, Kitangari na Newala Mjini.

“Napenda kuwashukuru Wananchi, Viongozi na Wadau wote kwa kushiriki uzinduzi huu wa Mahakama za Mwanzo za Chikundi, Kitangari na Newala Mjini. Ushiriki wenu unaonesha namna ambavyo jamii inathamini uwepo wa huduma za haki karibu na Wananchi,” alisema.

Alieleza kuwa Mahakama ya Tanzania ina mikakati madhubuti ya kuhakikisha Wananchi wanapata haki bila kucheleweshwa wala kubaguliwa, na kwamba moja ya mikakati hiyo ni ujenzi wa Mahakama za Mwanzo katika maeneo mbalimbali nchini.

“Mahakama ya Tanzania imejipanga kuhakikisha kila Mwananchi anapata huduma ya kisheria kwa wakati na kwa usawa. Ndiyo maana tunaendelea kujenga Mahakama za Mwanzo ili kusogeza huduma hizi karibu zaidi na Wananchi,” aliongeza.

Naye Mtendaji wa Mahakama Mtwara alieleza kuwa Mahakama ina mkakati wa kuendelea kujenga majengo mapya na bora kwa ajili ya Mahakama mbalimbali nchini ili kuwezesha shughuli zote za utoaji wa haki kufanyika katika mazingira mazuri na yenye ufanisi.

“Ujenzi wa majengo haya ni sehemu ya mkakati wa kuboresha mazingira ya kazi kwa Watumishi wa Mahakama na kuhakikisha Wananchi wanapata huduma za haki katika maeneo yaliyo karibu nao na yenye miundombinu bora,” alisema.

Aidha, aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa juhudi zake za kuboresha miundombinu ya utoaji wa huduma za kisheria katika jamii, akisema hatua hiyo itaongeza ufanisi na kuimarisha imani ya Wananchi kwa Taasisi hiyo.

Vilevile, aliwasisitiza watumishi wa Mahakama kuyatunza majengo hayo na miundombinu mingine iliyojengwa ili yaweze kudumu na kuendelea kutoa manufaa kwa jamii pamoja na watumishi kwa ujumla.

Kwa upande wao, baadhi ya Wananchi waliohudhuria hafla hiyo walieleza kufurahishwa na hatua hiyo, wakisema itapunguza umbali waliokuwa wakisafiri kufuata huduma za Mahakama.

Mbali na viongozi hao, hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi, Fatima Saidi Kubenea. Katika hotuba yake, alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwepo kwa ushirikiano mzuri kati ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na Mahakama ili kuhakikisha huduma za haki zinawafikia wananchi kwa ufanisi zaidi.

Mahakama za mwanzo zitakuwa na jukumu la kusikiliza na kuamua kesi ya ngazi ya kwanza, madai kulingana na mamlaka yao kisheria. Wananchi wamehimizwa kutumia vyema fursa hiyo kwa kufuata taratibu za kisheria na kuepuka kujichukulia sheria mkononi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, akiwasili katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Chikundi.

Wageni waalikwa walioshiriki kwenye uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Mtwra, Mhe. Said Ding’ohi (kulia) na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi Fatima Saidi Kubenea pamoja wasikiliza taarifa ya ujenzi wa majengo ya Mahakama.

Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Mtwara akitoa hotuba yake katika uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo iliyofanyika Chikundi.

Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi Fatima Saidi Kubenea akihutubia katika uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akitoa hutuba katika uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo eneo la Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akikata utepe katika shughuli ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto,) Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya (katikati) na Jaji wa Mahakama ya Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara (kulia) kwa pamoja wakikagua ukumbumbi wa wazi wa Mahakama ya Mwanzo Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Said Ding’ohi (wa pili kushoto), Naibu Msajili, Mhe. Seraphine Nsana (wa kwanza kushoto), Naibu Msajili, Mhe. Elia Mrema (wa kwanza kulia) na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi Fatima Saidi Kubenea (wa pili kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Kanda ya Mtwara.

Habari hii imehaririwa na FAUSSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni