Alhamisi, 30 Aprili 2026

MSAJILI MKUU ASISITIZA WATUMISHI KUILINDA HADHI YA MAHAKAMA

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, amewaasa Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Musoma kuilinda hadhi ya Mahakama kupitia utendaji wao wa kazi na hata katika maisha nje ya kazi.

Mhe. Nkya alitoa wito huo jana tarehe 29 Aprili, 2026 alipofanya kikao kazi na Watumishi hao pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma.

Awali akifungua kikao kazi hicho, Mhe Nkya alisema yuko Musoma kwa siku tatu kwa ajili ya ufuatiliaji na tathmini ya shughuli mbalimbali za kimahakama ambazo zimefanyika katika baadhi ya Mahakama za Masjala Ndogo Musoma.

Vilevile kupitia kikao hicho, Mhe. Nkya aliwasisitiza Watumishi kupenda kujisomea ili kujiongezea maarifa ya vitu tofauti vitakavyoboresha utendaji wao wa kazi, afya na maisha kwa ujumla.

Kupitia kikao kazi hicho, Watumishi mbalimbali walipata nafasi ya kuwasilisha hoja, changamoto na mapendekezo ya maboresho mbalimbali ili kuboresha mazingira ya kazi, maslahi na huduma kwa mteja.

Aidha, pamoja na ufuatiliaji na tathmini ya shughuli mbalimbali za kimahakama Mhe. Nkya alikabidhi vifaa vya kazi ambavyo ni kompyuta mpakato kwa Majaji wa Mahakama Kuu Musoma.

Katika ziara hiyo, Msajili Mkuu ametembelea Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, Mahakama ya Wilaya Musoma, Mahakama ya Wilaya Butiama, Mahakama za Mwanzo Musoma Mjini, Mukendo na Kukirango na kote alikopita ameongea na Watumishi wa maeneo hayo.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya (aliyesimama) akiwasalimia watumishi wa Mahakama Kuu Musoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakati wa kikao kazi hicho.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Omary Kingwele (aliyesimama) akimkaribisha Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya (aliyeketi mbele katikati) wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Mkurugenzi wa Ufuatiliaji, Ukaguzi na Mrejesho wa Huduma za Mahakama, Mhe. Maira Kasonde (wa pili kushoto) akichangia jambo wakati wa kikao kazi na watumishi wa Mahakama Musoma.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakifuatilia kwa makini kikao kazi cha Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe Eva Nkya (aliyeketi mbele katikati) wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Watumishi wa Mahakama Kuu Musoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakimsikiliza kwa makini Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya (aliyeketi mbele katikati) wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya, akizungumza wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Marlin Komba (kushoto) akipokea kompyuta mpakato kutoka kwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (kulia) alipokuwa katika ziara ya Mahakama Musoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Geita.

 

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni