Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo
ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka wajumbe wa Baraza la
Wafanyakazi kutumia kikao hicho kama jukwaa muhimu la majadiliano ya wazi ili kuimarisha
uwajibikaji, uwazi na ushirikishwaji wa waatumishi katika masuala ya kiutumishi.
Mhe. Rwizile aliyasema hayo hivi karibuni kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma wakati akiongoza kikao
cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu Kigoma kilicholenga kujadili
ustawi wa Watumishi, tathmini ya utekelezaji wa maazimio yaliyopita na kuweka
mikakati ya kuboresha utendaji kazi wa Taasisi.
Katika hotuba yake ya ufunguzi, Jaji
Rwizile alisisitiza umuhimu wa Baraza kama chombo cha kushauri na kuimarisha
mahusiano kazini kwa kuzingatia mkataba mpya unaolenga kuboresha maslahi ya
mwajiri na watumishi wake.
Jaji Mfawidhi huyo alieleza kuwa, “Baraza
hili lipo kisheria na mkataba mpya umejikita katika kujenga Taasisi yetu
kwa pamoja, hivyo mawazo yenu ni msingi wa maboresho
tunayoyahitaji katika usimamizi wa shughuli za usimamizi wa usikilizwaji mashauri
katika Mahakama zetu.”
Hata hivyo, aliwajulisha wajumbe kuwa,
kupitia kikao hicho kulikuwa na ajenda ya uchaguzi wa Viongozi
wapya wa Baraza kwa mujibu wa mkataba mpya wa Baraza la Wafanyakazi, hivyo
aliwashukuru na kuwaaga Viongozi wa Baraza waliopita amba oni Mhe. Victor
Kagina, aliyekuwa Katibu na Bi. Naomi Chawe aliyekuwa Katibu Msaidizi wa Baraza
hilo.
Zoezi la uchaguzi liliongozwa na Ofisa
Kazi, Bw. Frank Kimaro ambaye alisisitiza taratibu za uchaguzi kuwa wazi
na shirikishi kwa wajumbe wote kwa mujibu wa Mkataba.
Baada ya zoezi la kupiga kura
kukamilia, Msaidizi wa Kumbukumbu, Bw. Julius Manyanya alichaguliwa kuwa
Katibu mpya wa Baraza hilo na Msaidizi
wa Sheria wa Jaji, Mhe. Mburalina Maira aliteuliwa kuwa Katibu Msaidizi na
Bi. Naomi Chawe alichaguliwa kuwa Mwakilishi TUGHE Baraza la Wafanyakazi Taifa.
Katika tathmini ya utekelezaji wa maazimio
ya kikao kilichopita, Baraza liliridhishwa kubaini kuwepo kwa hatua kadhaa
zenye tija zinazoonesha juhudi za uongozi katika kuboresha ustawi wa watumishi
na ufanisi wa utendaji kazi.
Aidha, Watumishi waliibua hoja ya kuchelewa
kupandishwa madaraja, hususan kwa wale walio kwenye ajira za muda mrefu. Katika
mjadala, ilisisitizwa kuwa, watumishi wanapaswa pia kujitahidi kujiendeleza
kielimu ili kukidhi vigezo.
Wajumbe wa Baraza hilo wamesisitiza umuhimu wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2025/2026, huku wakichukua hatua za haraka na za kimkakati kushughulikia mara tu changamoto zilizobainika ili kutatuliwa.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (kulia) akimkabidhi Mkataba wa Baraza la Wafanyakazi Katibu wa Baraza mpya, Bw. Julius Manyanya mara baada ya kuibuka mshindi katika nafasi hiyo kwa kupata kura nyingi za kishindo kutoka kwa wajumbe.
Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kigoma wakifuatilia kwa makini mjadala ulikuwa ukiendelea wakati wa kikao cha Baraza hilo.
Ofisa Kazi, Bw. Frank Kimaro akitoa ufafanuzi juu ya utaratibu wa uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kigoma.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


Hakuna maoni:
Chapisha Maoni