Jumapili, 12 Aprili 2026

SUMBAWANGA YAFANYA KIKAO CHA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na. SHARIFU MOKIWA - Mahakama, Sumbawanga

Mahakama Kuu, Kanda ya Sumbawanga imefanya kikao cha Baraza la Wafanyakazi tarehe 10 Aprili, 2026 kwa lengo la kuimarisha ushirikiano kati ya Uongozi na watumishi, kuboresha utendaji kazi na utoaji wa huduma za kimahakama.

Kikao cha Baraza hilo kilifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Frederick Manyanda na kuhimiza mshikamano na uwajibikaji miongoni mwa watumishi kwa kutumia kaulimbiu ikiwemo, Mshikamano Daima (Solidarity Forever) Kazi na Utu Tunasonga Mbele pamoja ile ya Mahakama ya Tanzania ya Uadilifu, Uweledi na Uwajibikaji.

Baraza hilo, lilitumia kikao hicho kufanya uchaguzi wa Katibu na Katibu Msaidizi wa Baraza la wafanyakazi ambao watachukua nafasi zilizoachwa wazi na viongozi waliopita ambao mmoja alihama na mwengine alikuwa anatokea Mkoa wa Katavi ambako kumeanzishwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo.

Katika uchaguzi huo, kuliwasilishwa majina mawili ya wajumbe yaliyopendekezwa na Menejimenti ili yaweze kupigiwa kura na wajumbe wa kikao na baada ya zoezi la uchaguzi Bw. Fredrick Mahava alichaguliwa kuwa Katibu wa Baraza la wafanyakazi huku Bi. Bupe John akichaguliwa kuwa Katibu Msaidizi wa Baraza la wafanyakazi.

 

Akizungumza baada ya kuchaguliwa Katibu wa Baraza la wafanyakazi Bw. Fredrick Mahava aliwashukuru wajumbe kwa imani waliyoionesha kwake. “Asanteni kwa kutuchagua kuwa Katibu na Katibu Msaidizi. Tunaahidi kushirikiana na Mwenyekiti katika kutekeleza majukumu yetu na kuhakikisha tunatimiza majukumu tuliyopewa,” alisema.

Katika hatua nyingine, Katibu huyo alikabidhiwa Mkataba wa Baraza la wafanyakzi kati ya Mahakama ya Tanzania na Chama cha wafanyakazi Serikalini na afya Tanzania (TUGHE) mbele ya wajumbe wa kikao hicho.

Aidha, zoezi hilo lilienda sambamba na uteuzi wa Kamati Tendaji ya Baraza la wafanyakazi ambayo inaundwa na Menejimenti yote, Mwenyekiti wa TUGHE, Katibu wa TUGHE na wajumbe kutoka kwa wawakilishi wa wafanyakazi ambapo wajumbe hao walichaguliwa kwa kupigiwa kura ambao walikuwa ni Bi. Veronika Garikunga kutoka Mahakama ya Wilaya Sumbawanga, Bw. Damian Mlowezi Kutoka Mahakama ya Wilaya Kalambo, Bi. Jenifeva Mwakanema kutoka Wilaya ya Nkasi na Bi. Atupelile Konga kutoka Mahakama Kuu, Kanda ya Sumbawanga.

Akitolea ufafanuzi kuhusu Baraza hilo, Afisa kazi Mkoa wa Rukwa Bw. Curthbelth Kumburu alisema kuwa, Baraza la wafanyakazi ni chombo cha ushirikishwaji kinachomkutanisha mwajiri na mwajiliwa kwa lengo la kupanga mipango mbalimbali na kushughulikia changamoto zinazojitokeza mahali pa kazi.

Bw. Kumburu aliongeza kuwa, lengo Kuu la Baraza hilo ni kuhakikisha Taasisi inasonga mbele kwa kuwashirikisha watumishi katika kutoa maoni chanya yanayochangia maendeleo ya Taasisi.

Aidha, alibainisha kuwa, Baraza hilo linaendeshwa kwa mujibu wa sheria mbalimbali ikiwemo sheria ya utumishi wa umma, sheria ya ajira na mahusiano kazini pamoja na sheria ya taasisi ya kazi namba 7 ya mwaka 2024 na mkataba wa kuanzishwa kwa Baraza husika.

Vilevile, Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Sumbawanga Bw. Machumu Essaba aliwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu 2025/2026 kwa wajumbe ikionyesha hali ya raslimali watu, maendeleo ya kiutendaji pamoja na utekelezaji wa majukumu mbalimbali

Baraza hilo, liliwasilisha hoja mbalimbali za wafanyakazi na kujadiliwa kwa pamoja, zile ambazo zilikuwa ndani ya uwezo wa Viongozi wa Kanda zilipata majibu papopapo na zile zilizo nje ya uwezo wa viongozi wa Kanda zilipokelewa kwa ajili ya kuwasilishwa kwenye Baraza Kuu litakalofanyika Makao Makuu ya Mahakama hivi karibuni.

Kikao hicho cha Baraza la wafanyakazi kilihitimishwa kwa msisitizo wa kuendelea kudumisha mshikamano, ushirikiano na uwajibikaji miongoni mwa watumishi ili kuhakikisha Mahakama inatekeleza majukumu yake kwa ufanisi. 

Jaji Mfawidhi Mahakama ya Sumbawanga Mhe, Frederick Manyanda akifungua kikao cha Baraza la wafanyakazi Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga 



Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga Bw. Machumu Essaba akiwasilisha taarifa ya utekelezaji 2025/2026 majukumu ya Mahakama.

Katibu wa Baraza la wafanyakazi Bw. Fredrick Mahava (kulia) akikabidhiwa Mkataba wa Baraza la Wafanyakazi baada kuchaguliwa kuwa Katibu wa Baraza hilo na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Bw. Machumu Essaba (kushoto)

Wajumbe wa kikao cha Baraza la Wafanyakazi wakiimba wimbo kuonesha umoja na mshikamno.

Afisa kazi  kutoka Mkoa wa Rukwa  Bw. Curthbelth Kumburu akitoa ufafanuzi kuhusu Baraza la Wafanyakazi.

Wajumbe wa kikao cha Baraza la Wafanyakazi wakiimba wimbo kuonesha umoja na mshikamno.




 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni