Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala
Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa amewataka washiriki wa mafunzo ya
Usuluhishi ambao ni Mahakimu kutoka Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza kutumia
ujuzi walioupata kuisaidia jamii kumaliza migogoro yao kwa amani na utengamano.
Mhe. Mbelwa aliyasema hayo hivi karibuni
mkoani Kigoma wakati akifunga mafunzo ya Usuluhishi yaliyoendeshwa kwa siku
tano na kuhudhuriwa na washiriki 16.
“Tumieni ujuzi huu wa usuluhishi kuisaidia
jamii kutatua migogoro kwa njia ya amani ili kuleta utengamano wa kijamii ili
kupunguza utitiri wa migogoro katika Mahakama zetu na hii itaboresha
upatikanaji haki kwa wananchi,” alisema Mbelwa.
Alibainisha kuwa, mafunzo hayo yamefanikiwa
kwani washiriki wamepewa mbinu zote muhimu za usuluhishi, hivyo ni matarajio ya
Mahakama na Jamii kwa ujumla wake kuona wanatumia vema ujuzi na weledi
walioupata kuleta tija katika utatuzi wa migogoro Mahakamani ili kupunguza
mashauri.
Aidha, alifafanua kuwa, mafunzo hayo
yamefanyika sambamba na Wiki ya Usuluhishi Kitaifa, huku akitoa pongezi kwa washiriki
ambavyo wameshiriki vema Wiki ya Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya Usuluhishi,
ambapo wametumia weledi walioupata kufanya usuluhishi na umeleta tija kwa Mahakama
Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma kwa mashauri waliyosimamia ambayo usuluhishi wake
umefanikiwa.
Aidha, alimshukuru Jaji Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju kukubali mafunzo hayo yafanyike Kigoma
na washiriki kutoka maeneo tajwa walioshiriki katika mafunzo hayo.
Vilevile alimshukuru Jaji wa Mahakama ya
Rufani Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe.
Dkt. Paul Kihwelo kwa kuridhia Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kigoma, Mhe.
Augustine Rwizile na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa
kuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo ya Usuluhishi.
Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama
ya Wilaya Nyamagana, Mhe. Ramla Shehagilo alitoa shukrani kwa niaba ya
washiriki, ambapo aliwashukuru Wakufunzi wa Mafunzo hayo sambamba na Waandaaji
wa mafunzo hayo ambao ni Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) pamoja na Mahakama
ya Tanzania kwa kuwachagua wao kuwa washiriki wa mafunzo ya usuluhishi katika Wiki
ya Kitaifa ya Usuluhishi.
Naye, Hakimu Mkazi na Mratibu wa
Mafunzo kutoka Chuo Cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Husna
Rweikiza akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Chuo IJA, Mhe. Dkt. Kihwelo alibainisha
kuwa washiriki wamejifunza mbinu zote za usuluhishi hivyo, malengo ya mafunzo
hayo yamefikiwa, na kubainisha kuwa wasuluhishi hao watakuwa na tija katika
kuongeza juhudi za kuimarisha ufanisi na upatikanaji wa haki Mahakamani.
Mafunzo hayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ Tanzania).
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni