Jumatatu, 13 Aprili 2026

WATUMISHI MANYARA WAFANYA UTALII HIFADHI YA TAIFA TARANGIRE

Na. CHRISTOPHER MSAGATI–Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. Ilvin Claud Mugeta, amewaongoza watumishi wa Mahakama Kanda hiyo, kufanya ziara ya utalii wa ndani iliyofanyika mnamo tarehe 10, Aprili 2026 katika Hifadhi ya Taifa Tarangire mkoani Manyara.

Akizungumza na watumishi kwa nyakati tofauti wakati wa maandalizi na hitimisho la ziara hiyo, Mhe. Mugeta alieleleza lengo la ziara hiyo ni kutambua maeneo mapya ambayo watumishi wengi hawajawahi kuyafikia, kupata furaha na kuimarisha afya ya akili.

“Muda mrefu tunakaa ofisini tukiwa tunashughulika na majukumu ya usikilizwaji wa mashauri bila kupata fursa ya kufahamu masuala mengine mengi ambayo tunapaswa kuyafahamu. Hili jambo linaweza kupunguza ufanisi wa utendaji kazi kama tunakosa muda wa kuwaza masuala mengine nje ya kazi, ziara hii ya Tarangire ituwezeshe kuwa na mtazamo mpya lakini pia kuyafahamu maeneo ambayo yanatuzunguka,” alisema Mhe Mugeta.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora aliwapongeza watumishi wote waliofanikiwa kushiriki ziara hiyo na kuwashauri watumishi kuendelea kushirikiana katika masuala kama hayo yanapojitokeza kwa kuwa pia yanaongeza upeo wa ufahamu ambao unaimarisha utendaji kazi.

“Nawapongeza watumishi wote ambao no watalii wenzangu waliofanikiwa kusafiri kwa ajili ya utalii wa ndani, nawashauri siku nyingine ziara kama hii ikitokea tuungane sote kwa pamoja kwa kuwa tutakuwa tumeongeza kitu kikubwa sana katika upeo na ufahamu wetu na kuboresha ufanisi wa kazi,” alisema Mhe. Jaji Kamuzora.

Katika hatua nyingine, watumishi ambao walikuwa wamepanda basi walikwama kwenye matope ambayo yamesababishwa na mvua ambazo zinaendelea kunyesha nchi nzima jambo liliwafanya watumishi hao kushuka kwenye basi na kuanza kulisukuma. Hata hivyo walijulishwa na waongoza watalii kuwa hayo ni mambo ya kawaida kutokea katika mbuga na pia ni sehemu ya masuala ambayo yanafanya ziara ipendeze zaidi.

Watumishi 112 wa kada mbalimbali kutoka Mahakama za ngazi mbalimbali wakiwemo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Mahakimu Wakazi wafawidhi wa Wilaya zilizopo katika Kanda ya Manyara, Mahakimu na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara walishiriki ziara hiyo ikiwa ni muendelezo wa kutambua vivutio vya asili vilivyo ndani na nje ya Mkoa wa Manyara pamoja na kuwafanya watumishi kuendelea kuishi kwa umoja na ushirikiano.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara wakati wa ziara ya kuona Wanyama katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyama Tarangire.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta (wa nne kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi ambao wameajiriwa siku za hivi karibuni katika ziara ya kuona Wanyama Tarangire.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara wakiwa wanasukuma basi lililokwama kwenye matope wakati wa Ziara ya kuona Wanyama katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyama Tarangire.

Kundi la Swala wakiwa wanaonekana wakila majani katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyama Tarangire.

Tembo akiwa anaonekana akila majani katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyama Tarangire.

Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora (aliyesimama) mbele, akitoa neno kwa watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara kabla ya kuanza safari ya kuelekea Tarangire.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara wakiwa katika picha ya pamoja mbele ya jengo la Mahakama Kuu Manyara wakati wakijiandaa kuelekea Tarangire.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni