Jumatano, 13 Mei 2026

JAJI MKUU ATAKA CHANGAMOTO ZA WATUMISHI KUTATULIWA BILA VIKWAZO

·       Awataka watumishi wa Mahakama kuendelea kutekeleza Kaulimbiu ya Siku ya Sheria, 2026

·       Ataka mashauri yasikilizwe mapema ipasavyo ili kuchangia ustawi na maendeleo ya Taifa

·       Asisitiza ushirikiano, amani na kuthaminiana kwa Watumishi

Na MARY GWERA-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama, amewataka Viongozi wa Mahakama kuwa wanyenyekevu sambamba na kufungua milango kwa ajili ya kuwasikiliza Watumishi walio chini yao ili kutatua changamoto wanazokabiliana nazo bila vikwazo.

Mhe. Masaju ametoa wito huo leo tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.

“Kadri unavyokuwa na Madaraka makubwa ni kwa kiwango hicho hicho unakuwa mtumishi wa wote, sisi Viongozi ni Watumishi wa watu, tuwe na tabia ya kufungua milango tuwasikilize walio chini yetu, tusifunge milango,” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu amesema Viongozi pia wanawategemea Watumishi walio chini yao ambapo ameeleza kuwa, kwa kadri Kiongozi anavyozidi kupanda kimadaraka ni kwa kiwango hicho hicho anazidi kuwa tegemezi kwa watu wengine, na kwamba kadri unavyokuwa na Madaraka makubwa ni kwa kiwango hicho hicho unapaswa kuwa mnyenyekevu ili uwafikie wanaokutegemea na wao wakufikie ili ujue changamoto zao na mafanikio yao.

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema kuwa, Viongozi wasiwazuie wajumbe wa Baraza kuzungumza yale yanayowasibu, badala yake wawaache huru kusema yale wanayokabiliana nayo katika utekelezaji wa majukumu yao ili kupata ufumbuzi wa utekelezaji mzuri wa majukumu ya Mahakama.

Ameongeza kuwa, hata Viongozi wanapotembelea Mahakama mikoani Viongozi wa Mahakama husika wanapaswa kuwaacha watumishi wazungumze na Viongozi ili wajue Mahakama imepiga hatua gani katika maendeleo, wajue changamoto  zilizopo ili tutatue changamoto hizo na kupiga hatua ili hatimaye vikao vya Baraza viwe vya furaha.

Aidha, Jaji Mkuu amewapongeza watumishi wa Mahakama wa Kada zote kwa utekelezaji mzuri wa majukumu ya Mhimili huo kwa ufanisi ipasavyo.

“Kwanza natambua mchango wenu, kila mmoja wetu katika utendaji wa Mahakama ya Tanzania, mmefanya kazi kubwa sana, miaka iliyopita na mimi tangu nimekuja kushirikiana na ninyi mmefanya kazi kubwa sana ya kutekeleza majukumu yenu na wakati fulani katika mazingira magumu mimi naelewa katika utumishi wangu mimi nimeanzia chini sana nikiwa Wakili wa Serikali Daraja la tatu, kwahiyo ninafahamu na wakati mwingine

Katika upande mwingine, Mhe. Masaju amewakumbusha Viongozi na watumishi wote wa Mahakama kwa ujumla kuendelea na utekelezaji wa Kaulimbiu ya Siku ya Sheria Nchini ya mwaka huu 2026 isemayo; ‘Mchango wa Mahakama ya Tanzania katika Maendeleo na Ustawi na Maendeleo ya Taifa.’

“Mahakama ina mchango mkubwa sana, mnaweza kurejea hotuba yangu ya Siku ya Sheria, nimeeleza yote, hii haiwezi kuwa ni Kaulimbiu ya Siku ya Sheria, hii tunaiishi mwaka huu wote wa 2026, kwahiyo tunapofanya kazi yatupasa tujue tuna mchango katika ustawi na maendeleo ya Taifa la Tanzania. Wajibu wetu Mahakama ni kuendelea kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi ipasavyo na tunapaswa kuendelea kuwa wabunifu,” amesema Jaji Mkuu.

“Kwenye Kanda mtaangalia mnapopanga mashauri mjue kuna kitu tunafanya, kwahiyo mnatakiwa kuangalia ustawi na maendeleo ya Taifa, tunahusika hata sisi katika maendeleo kwa sababu amani ni msingi mkubwa unaoleta ustawi na maendeleo ya Taifa,” amesema Mhe. Masaju.

Ameeleza kuwa, kwa msingi huo ndio maana wa mfano kuna mashauri ya jinai, mashauri ya madai, mashauri ya uchaguzi na kila aina ya mashauri yanashughulikiwa na kumalizika watu wanapiga hatua mapema.

“Mpaka sasa kwa mfano yale mashauri ya uchaguzi yaliyofunguliwa, limebaki shauri moja tu, mengine yote yameshaisha, kuna mashauri ya kila aina ya mirathi, ya ndoa, ya uhujumu uchumi. Sisi kama Mahakama wajibu wetu ni upi? najua tunazo changamoto pengine hatupati ushirikiano mzuri sana lakini sisi hatuwezi kukata tamaa ndio wajibu wetu, tukiharibu tunawajibishwa sisi, sisi ndio tunaosemwa na tunapaswa tuendelee kuwa wabunifu katika maeneo yetu ya kazi kuhakikisha kwamba mchango wa Mahakama ya Tanzania katika ustawi na maendeleo ya Taifa unazidi kuimarika,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Amesema, tunaishi katika nchi inayozingatia Utawala wa Sheria, hivyo, Mahakama ina nafasi kuwa katika ustawi na maendeleo ya Taifa na kwa sababu ni muhimu mashauri yanapopangwa yapangwe kimkakati na hayatakiwi kucheleweshwa bila sababu za msingi, lakini pia inabidi kuwa ni mikakati ya kubaini mashauri yenye kero yanayoleta sintofahamu katika jamii yashughulikiwe.

“Uchumi ni Ardhi wala hata sio kitu kingine, kwahiyo tuna mikakati ya kumaliza haya mashauri ya Ardhi tangu mwaka jana tumekuwa na hiyo mikakati, na Mahakama Kuu wamefanya vizuri sana kwa sababu mashauri ya ardhi kwa Mahakamani yanaanzia Mahakama Kuu, yanakwenda Mahakama Rufaa mengine kwenye ‘originial jurisdiction’ tunafanya vizuri japo bado ni mengi kwa sababu migogoro inazalishwa mingi na sehemu fulani tumeshauri kwa mfano ukisoma Sheria ya Usajili wa Ardhi (Land Registration Act) kuna mtu pale anaitwa ‘The Registrar of Titles) ana mamlaka makubwa sana  mashauri mengine hata yasingekuwa yanakuja mahakamani yangekuwa yanaenda pale kama kuna migogoro wakishindwa kutatua upande ambao hauridhiki unakuja Mahakama ya Rufani,” ameeleza.

Kwa upande wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Masaju amesema kuna mashauri mengi ya jinai, hivyo wameweka mkakati wa kushughulikia mashauri hayo ambayo walianza kusikiliza katika Vikao vya Mahakama ya Rufani (COA Session) ya mwezi Februari ambapo walichanganya na mashauri ya mirathi ili watu wawe na amani kwenye familia zao na wengine wajue hatma yao.

“Majaji hawa wa Mahakama ya Rufani wamefanya kazi nyuma, mashauri mengi yameenda, kama wengine hawasema sisi wenyewe tujisemee, mimi nawapongeza sana Mahakama ya Rufani,” amesema Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, Mwezi Aprili walipanga mashauri ya kazi na ndoa ambayo kikao chake kimekamilika tarehe 08 Mei, 2026 na wengine wanaendelea, jitihada hizo ni katika wajibu wa kutekeleza mchango wa Mahakama katika maendeleo na ustawi wa Taifa.

Kadhalika, amesema katika Vikao vinavyofanyika Juni na Agosti, 2026 mashauri ya ardhi yatashughulikiwa tena ili kuyapunguza. Ameeleza kuwa, katika vikao hivyo wataweka pia mashauri machache ya jinai na kabla ya Desemba pia watakuwa na mashauri ya jinai.

Amebainisha kuwa, ili Mahakama ifanikiwe inahitaji ushirikiano kutoka Mihimili mingine ili kutekeleza jukumu la utoaji haki kwa ufanisi ipasavyo.

Kwa upande wa Mahakama Kuu, Mhe. Masaju amesema, wamekamilisha vikao vya kusikiliza mashauri ya ardhi ikiwa ni mwendelezo wa zoezi ambalo lilianza mwaka jana, ambapo amesema kwa sasa hatatoa takwimu kwakuwa zinaandaliwa na Msajili wa Mahakama Kuu na zitatangazwa kwa wananchi kile ambacho Mahakama imefanya.

Amesema pia kulikuwa ni shida kubwa za mashauri ya baadhi ya waajiri kutowasilisha michango ya mafao ya watumishi wao katika mifuko ya hifadhi za jamii ambapo amesema wamefanya mabadiliko ya kanuni na kwamba katika usikilizaji wa mashauri hayo Majaji na Mahakimu wamefanya vizuri kwakuwa mashauri hayo mengi yameisha na yameisha kwa njia ya usuluhishi.

“Sisi Mahakama nia yetu ni kwamba wafanyakazi wapate stahili zao sio wanakatwa halafu mwisho wa siku hawapewi stahili zao,” ameeleza.

Kadhalika Jaji Mkuu amewataka watumishi wote wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano, umoja na kuthaminiana katika utekelezaji wa majukumu.

 Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Ezra Kyando akizungumza jambo wakati wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama lililofunguliwa leo tarehe 13 Mei, 2026 na Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha).


Wajumbe mbalimbali wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia hotuba ya Jaji Muu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) leo tarehe 13 Mei, 2026 alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama jijini Dodoma.

Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (wa kwanza kushoto) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (wa pili kushoto) wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama nchini ulioanza leo tarehe 13 Mei, 2026. Mkutano huo unatarajiwa kuhitimishwa kesho tarehe 14 Mei, 2026.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija (wa pili kushoto), Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kulia), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (wa kwanza kushoto) na Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama, Mhe. Christina Mlilwo.


Wajumbe mbalimbali wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia hotuba ya Jaji Muu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) leo tarehe 13 Mei, 2026 alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama jijini Dodoma.

Wimbo wa Mshikamano Daima (Solidarity Forever) ukiimbwa na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.


Meza kuu ikiwa katika picha za pamoja na Wajumbe wa Baraza Makao Makuu pamoja na Sekretarieti ya Maandalizi ya Mkutano huo.

(Picha na Mary Gwera-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni