Jumanne, 12 Mei 2026

JAJI SEHEL, MWENYEKITI KAMATI YA JAJI MKUU UFUATILIAJI NA TATHMINI AFANYA ZIARA MAHAKAMA NJOMBE

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

 Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na  Tathmini, Mhe. Barke Sehel hivi karibuni alifanya ziara ya kikazi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe lengo likiwa ni kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa shughuli za Mahakama.

 

Mhe. Sehel ambaye pia ni na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) alianza ziara yake tarehe 07 Mei, 2026 ambapo alipokelewa na mwenyeji wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa TAWJA pamoja na Viongozi na watumishi watumishi wa Mahakama Njombe.

 

Jaji Sehel alipata wasaa wa kuzungumza na watumishi wa Mahakama Njombe ambapo alisikiliza changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo ikiwemo ukosefu wa huduma ya usafiri wa basi la Mahakama linaloweza kuwapeleka ofisini kutokana na umbali mkubwa wa kutoka maeneo wanayoishi mpaka mahali pa kazi.

 

Aidha, Mwenyekiti huyo alipata fursa ya kutembelea jengo la Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Njombe (IJC) ambalo lipo kwenye hatua za mwisho kwa asilimia 97 na baadhi ya viongozi na watumishi tayari wameanza kuhamia kwenye jengo hilo.

 

Katika ziara hiyo Mwenyekiti alifanya ukaguzi wa shughuli za kimahakama katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mahakama ya Wilaya ya Njombe na Makete pamoja na Mahakama ya Mwanzo Njombe.

 

 Vilevile, katika ziara hiyo Mhe. Sehel alipata fursa ya kuzungumza mambo mbalimbali ya TAWJA Njombe katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wake pamoja na kuhuisha uanachama  wa TAWJA na IAWJ.

 

 

Akiendelea na kikao hicho huku wanachama wengine wakishiriki kwa njia ya mkutano mtandao (Video Conference) walio nje ya Wilaya ya Njombe, Mhe. Sehel  alisisitiza mshikamano pamoja na kushirikiana kikamilifu katika shughuli za Chama hicho, Tawi la Njombe ikiwa ni pamoja na kujitolea katika majukumu mbalimbali bila kujali malipo pamoja na kutoa elimu na kuhudhuria mikutano ya ndani.

 

 

Mwenyekiti huyo wa TAWJA alisisitiza kuwa Chama hicho ni jukwaa linalowawezesha kung’ara kitaifa na kimataifa kwa kazi zinazofanyika, ambapo aliwatakia wanachama wa TAWJA Njombe majukumu mema ya ujenzi wa Taifa huku akisisitiza uadilifu, weledi na uwajibikaji kama ambavyo Kaulimbiu ya Mahakama inasema.

 

Mhe, Sehel pamoja na wanachama wa TAWJA Njombe walipata fursa ya kukata keki na kufungua champeni pamoja na Makamu Mwenyekiti Mhe. Victoria Nongwa kama ishara ya mwanzo mpya wa TAWJA mkoani Njombe.

 


Jaji wa Mahakama ya Rufani  ambaye pia ni Mwenyekiti wa  Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (aliyeketi mbele katikati) akizungumza na Watumishi wa Mahakama Njombe alipotembelea Masjala hiyo hivi karibuni. Kushoto ni  Jaji Mfawidhi wa  Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndono ya Njombe ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Victoria Nongwa na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge. Aliyesimama upande wa kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama.  

 


Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa  Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Njombe mbele ya jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe wakati walipofanya ziara hivi karibuni. 


 Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na  Tathmini, Mhe. Barke Sehel akipatiwa maelezo na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Bw. Richard Mbambe (wa kwanza kushoto). Wa kwanza kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA akizungumza hivi karibuni na baadhi ya Wanachama wa Chama hicho wa mkoani Njombe.

Jaji Sehel akiwa katika maandalizi ya kukata keki maalum ikiwa ni ishara ya kuanza kwa Tawi mpya la TAWJA Mahakama Njombe.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa  TAWJA, Mhe.  Victoria Nongwa (kulia) akimpatia zawadi Jaji Sehel.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)




 

 

 

 

 

 

 

 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni