Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel leo tarehe 12 Mei, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania.
Kikao hicho kimefanyika kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma na kuhudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick pamoja na Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule.
Lengo la kikao hicho ambacho hufanyika kila mwaka kabla ya Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ni kujadili pamoja kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu watumishi wa Mahakama sambamba na kujadili hoja za Mabaraza ya Kanda na Divisheni za Mahakama Kuu kwa upana zaidi kabla ya kufanyika kwa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.
Aidha, Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania kinatarajiwa kufanyika kesho tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma chini ya Mwenyekiti wake ambaye ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.
Yafuatayo ni matukio katika picha ya Kikao kati ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.
Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule akizungumza jambo wakati wa kikao hicho.
Meza kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel ikisikiliza na kurekodi hoja mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na Viongozi wa TUGHE-Mahakama ya Tanzania leo tarehe 12 Mei, 2026 jijini Dodoma.



















Hakuna maoni:
Chapisha Maoni