Jumamosi, 23 Mei 2026

MAHAKAMA KUU NJOMBE YAJIANDAA USIKILIZAJI MASHAURI YA MAUAJI, UHUJUMU UCHUMI

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge ameongoza Kikao cha awali cha usikilizaji wa mashauri ya mauaji na uhujumu uchumi lengo likiwa ni kuharakisha uendeshaji wa mashauri kwa makosa yanayoweza kusikilizwa na Mahakama Kuu.

Kikao hicho kilifanyika tarehe 22 Mei, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu Njombe ambapo, Mhe. Bwegoge alikutana na Wadau wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe wakiwemo wa upande wa Mashtaka na upande wa Utetezi na kukubaliana mambo mbalimbali yunayohusu mashauri ya mauaji na uhujumu uchumi.

Awali, Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Isack Mlowe alifungua kikao hicho na kumkaribisha Jaji Bwegoge ili aweze kuzungumza na wadau wa Mahakama Njombe na kuwaeleza lengo la kikao hicho.

Aliwaeleza kuwa, kikao hicho kilikuwa kinahusiana na maandalizi ya usikilizwaji wa mashauri ya kikao cha usikilizaji wa mashauri ya mauaji na uhujumu uchumi kitakachoanza   tarehe 15 Juni, 2026 mpaka tarehe 12 Julai, 2026 Mahakama ya Mwanzo Makambako iliyopo katika Halmashauri ya Mji Mdogo wa Makambako.

Mhe. Bwegoge alijadiliana na wadau wa Mahakama mkoani Njombe kuhusu mambo mbalimbali pamoja na kupeana ushauri wa changamoto ambazo huwa zinajitokeza katika usikilizwaji wa mashauri.

Katika kikao hicho, alisema vikao vya mashauri hasa yanayosikilizwa  mfululizo huwa kunakuwa na changamoto kama vile uchelewaji wa mahabusu kufika Mahakamani, kupatikana kwa mashahidi ambao hutoa ushahidi wa shauri zaidi ya moja.

Aidha, Jaji Bwegoge alitoa ushauri wa hoja mbalimbali ambazo ziliibuka ikiwemo adha ya usafiri kutoka Njombe Mjini mpaka Halmashauri ya Mji Mdogo wa Makambako.

Nao upande wa Gereza Njombe na Polisi Njombe, walitoa   ombi la mahabusu ambao mashauri yao yatasikilizwa kwa siku zaidi ya moja mfululizo waweze kukaa Mahabusu zilizopo Mji wa Makambako wakae huko na siyo kurudi mkoani Njombe ili kupunguza gharama kutokana na aza ya mafuta kupanda bei ambapo Mhe. Bwegoge aliridhia ombi hilo.

Kwa upande wa mashtaka pamoja na upande wa utetezi walibaini mambo ya msingi katika usikilizwaji wa mashauri ambapo Mhe. Bwegoge aliwakumbusha Wadau Mahakama kuwa uendeshaji wa vikao hivyo hufuata Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA) na Kanuni za Makosa ya Uhujumu Uchumi.

Wakati wa kufunga kikao hicho, Mhe. Mlowe aliwashukuru wadau waliohudhuria kwenye kikao hicho ambao ni wadau wa Mahakama Njombe  wakiwemo upande wa Mashtaka (NPS), Ofisi ya Upelelezi Polisi Mkoa (RCO), Magereza Njombe na Mawakili wa Kujitegemea upande wa Utetezi pamoja na Ustawi wa Jamii Mkoa wa Njombe.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge (aliyeketi katikati) akiongoza 
Kikao cha awali cha usikilizaji wa mashauri ya mauaji na uhujumu uchumi. Aliyeketi kushoto Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Isack Mlowe na kulia ni Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, Bi. Lucia Mpepo wakiwa katika kikao hicho kilichofanyika tarehe 22 Mei, 2026 mahakamani hapo.


 Wadau mbalimbali wa Mahakama Kuu Njombe  wakifuatilia yaliyokuwa yakijiri katika Kikao cha awali cha usikilizaji wa mashauri ya mauaji na uhujumu uchumi. Aliyesimama ni  Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Isack Mlowe akisisitiza jambo wakati wa kikao hicho.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge akizungumza na Wadau wa Mahakama (hawapo katika picha) tarehe 22 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama hiyo.



Wadau mbalimbali wa Mahakama Njombe walioshiriki katika kikao hicho wakichangia jambo wakati wa majadiliano.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni