Jumatatu, 25 Mei 2026

TMJA MANYARA WAFANYA ZIARA YA MAFUNZO NA UTALII SERENGETI

Na. CHRISTOPHER MSAGATI–Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Ilvin Claud Mugeta, amewaongoza wajumbe wa Chama Cha Mahakimu na Majaji Tanzania kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo hiyo katika Mafunzo yaliyofanyika kuanzia tarehe 20 mpaka 23 Mwezi Mei, 2026 katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyama Serengeti.

Akizungumza na wajumbe hao kwa nyakati tofauti wakati wa maandalizi na hitimisho la ziara hiyo, Mhe. Mugeta alieleleza lengo la ziara hiyo ni kuwawezesha Majaji na Mahakimu kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kuendelea kujinoa na kuongeza ujuzi katika utendaji kazi wa kila siku ili kuleta tija na ufanisi wa utoaji huduma ya Utoaji Haki kwa wananchi kwa wakati mapema ipasavyo.

“Suala zima la utoaji haki kwa wakati mapema ipasavyo, linaenda sambamba na utoaji wa mafunzo mbalimbali kwa wahusika wote ambao wanahusika katika mnyororo huu wa Utoaji Haki…

…Kwa sasa tumeanza na Waheshimiwa Majaji na Mahakimu kwa kupitia Chama chetu cha TMJA lakini baadae tutaona namna ya kufikisha mafunzo haya kwa watumishi wengine. Lengo la mafunzo haya ni kuendelea kunoa maarifa na ujuzi wetu tulio nao kwa ajili ya kuboresha utoaji huduma,” alisema Mhe. Mugeta.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora ambaye pia ni Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Manyara aliwapongeza watumishi wote waliofanikiwa kushiriki ziara hiyo ya mafunzo na kuwashauri watumishi kuendelea kujisomea na kujiongezea ujuzi na maarifa ili kuwa imara katika maamuzi na utendaji kazi wa kila Siku.

“Nawapongeza watumishi wote (Watalii wenzangu) mliofanikiwa kusafiri kwa ajili ya mafunzo haya na ninawashauri siku nyingine tuendelee kupenda kujisomea kwa ajili ya kuboresha maarifa yetu ya kila siku hususan uandishi wa Hukumu zenye tija na zinazoeleweka vizuri kwa jamii,” alisema Mhe. Kamuzora.

Baadhi ya mada zilizotolewa katika mafunzo hayo ni pamoja na Uendeshaji wa mashauri ya Mirathi katika Mahakama za Mwanzo, Utekelezaji wa Hukumu katika Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo na pia Usimamizi na Uondoshaji wa vielelezo vinavyopokelewa Mahakamani.

Katika hatua nyingine, Wanachama hao wa TMJA Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara walitumia muda wao wa baada ya mafunzo katika kufanya ziara ya Utalii wa kuona wanyama wa aina mbalimbali katika Hifadhi hiyo ya taifa ya Serengeti.

Akizungumza kwa niaba ya wanachama wengine wa TMJA Manyara, Hakimu Mkazi Mahakama ya Mwanzo Bassotu Mhe. Sabato Mwangwa, aliushukuru uongozi wa TMJA Manyara pamoja na Uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kwa kuwezesha mafunzo hayo kufanyika katika Hifadhi ya Serengeti kwa sababu pamoja na mafunzo, pia wanachama wamepata muda wa kuburudisha akili na miili yao kwa kuweza kufanya utalii huo wa ndani.

“Tunashukuru sana viongozi wetu kwa kutuwezesha kufanya mafunzo haya huku mbugani, Pamoja na maarifa tuliyoyapata tumeweza kuburudika kwa kuona Wanyama wa aina mbalimbali. Tunaomba uongozi uone uwezekano wa kufanya mafunzo zaidi na ikiwezekana yaratibiwe katika maeneo kama haya,” alisema Mhe. Mwangwa.

Jumla ya wanachama 47 wa TMJA Manyara wakiwemo Majaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Mahakimu Wakazi wafawidhi wa Wilaya zilizopo katika Masjala Ndogo hiyo na pia Mahakimu wengine waliweza kushiriki ziara hiyo ya mafunzo.

Wengine waliokuwa kwenye ziara hiyo ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Maafisa Rasilimaliwatu na Maafisa Tawala wa Mahakama wa Masjala Ndogo hiyo walishiriki ziara hiyo ikiwa ni muendelezo wa kuendelea kutambua vivutio vya asili vilivyo ndani na nje ya Mkoa wa Manyara.

Sehemu ya Wajumbe wa Tawi la TMJA Manyara wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikitolewa wakati wa mafunzo ya Wajumbe wa Tawi la TMJA Manyara yaliyofanyika katika Hifadhi ya Taifa Serengeti.

Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Dongobesh Mhe. Mgusi Masinde iliyopo wilayani Mbulu akitoa mada ya Uendeshaji wa mashauri ya Mirathi wakati wa mafunzo ya Wajumbe wa Tawi la TMJA Manyara yaliyofanyika katika Hifadhi ya Taifa Serengeti.

Wajumbe wa Tawi la TMJA Manyara wakiwa katika picha ya Pamoja kabla ya kuanza kwa ziara ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

Mnyama aina ya Nyati akiwa katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kama alivyoonekana na wajumbe wa TMJA-Manyara katika ziara ya mafunzo na Utalii iliyofanyika Hifadhini hapo.

Wanyama aina ya Swala wakiwa katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kama walivyoonekana na wajumbe wa TMJA-Manyara katika ziara ya mafunzo na Utalii iliyofanyika Hifadhini hapo.

Mnyama aina ya Twiga akiwa katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kama alivyoonekana na wajumbe wa TMJA-Manyara katika ziara ya mafunzo na Utalii iliyofanyika Hifadhini hapo.

Mnyama aina ya Fisi akiwa katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kama alivyoonekana na wajumbe wa TMJA-Manyara katika ziara ya mafunzo na Utalii iliyofanyika Hifadhini hapo.

Wanyama aina ya Pundamilia wakiwa katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kama walivyoonekana na wajumbe wa TMJA-Manyara katika ziara ya mafunzo na Utalii iliyofanyika Hifadhini hapo.

Wajumbe wa Tawi la TMJA Manyara wakiwa katika picha ya Pamoja kabla ya kuanza kwa mafunzo yaliyofanyika katika Hifadhi ya Taifa Serengeti.

Majaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta (mwenye fulana ya mistari ya rangi nyekundu na nyeupe) pamoja na Mhe. Devotha Kamuzora (mwenye kofia ya rangi nyeusi) wakiwaongoza wajumbe wa TMJA-Manyara kumsikiliza mmoja wapo wa watumishi wa Hifadhi ya Taifa Serengeti mara baada ya kuwasili Hifadhini hapo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo akitoa Neno la Salamu wakati wa mafunzo ya Wajumbe wa Tawi la TMJA Manyara yaliyofanyika katika Hifadhi ya Taifa Serengeti.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni