Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita
Jaji wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Griffin
Mwakapeje, ameipongeza Mahakama Kuu Njombe kwa kufanya ziara ya mafunzo katika Mahakama ya Geita yenye lengo la
kubadilishana uzoefu wa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
(TEHAMA) katika utoaji wa haki kwa wananchi.
Mhe.
Mwakapeje alitoa pongezi hizo juzi tarehe 18 Mei, 2026 katika Ukumbi wa Mafunzo wa
Mahakama Kuu Geita wakati akiwakaribisha wajumbe kutoka Mahakama Kuu Njombe. Alisema kuwa Geita imeendelea kuwa mfano bora katika matumizi ya
TEHAMA ndani ya Mhimili
wa Mahakama.
“Mmefanya uamuzi sahihi
sana kuichagua Mahakama Kuu Geita kama sehemu ya kujifunza matumizi ya TEHAMA,
hivyo natarajia mafunzo haya yawe na mafanikio chanya katika kuongeza kasi ya
utoaji haki kwa wakati,” alisema Jaji Mwakapeje.
Aidha, aliwashukuru Viongozi wa Mahakama Masjala Ndogo Njombe kwa kujipanga
kujifunza kwa vitengo
mbalimbali vya Mahakama
ili kuongeza ufanisi wa kazi na kuondoa changamoto zinazoweza kujitokeza katika
utoaji wa huduma kwa wananchi.
Katika ziara hiyo, mada
mbalimbali ziliwasilishwa na menejimenti ya Mahakama Kuu Geita, zikieleza namna mifumo ya TEHAMA
inavyotumika kurahisisha utoaji wa haki kwa wakati pamoja na kuongeza uwazi
katika utendaji kazi wa Mahakama.
Naibu Msajili wa Mahakama
ya Tanzania Masjala Ndogo
Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, aliwasilisha mada kuhusu matumizi ya mfumo wa
kielektroniki wa usimamizi wa mashauri
na namna Mahakama
hiyo inavyoendesha shughuli zake bila matumizi ya karatasi.
Alieleza kuwa mfumo huo
umeongeza ufanisi, uwazi na urahisi wa usimamizi wa shughuli za Mahakama, huku Viongozi wakipata uwezo wa kukagua
mwenendo wa kazi kupitia mfumo huo bila kufika moja kwa moja katika maeneo
husika.
Kwa upande wake, Hakimu
Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi,
alifafanua jinsi Mahakama za Wilaya zinavyotumia mifumo ya kidijitali katika
usimamizi wa mashauri
na shughuli za kiutawala.
Naye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo
Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, alieleza namna Mahakama za Mwanzo zilivyoondokana
na matumizi ya karatasi kupitia mfumo maalum uliobuniwa na unaotumika katika Mahakama
zote za Mwanzo Masjala Ndogo
Geita.
Mada nyingine
iliwasilishwa na Winifrida Nghumbu, ambaye alieleza namna huduma ya KIOSK
inavyowasaidia wananchi kupata taarifa za kesi, kusajili kesi na kufuatilia
mwenendo wa mashauri yao kwa urahisi, hata kwa wale wasio na uelewa wa mifumo
ya Mahakama.
Pia, Kaimu Mtendaji wa
Mahakama Kuu Geita, Happiness Mushi, alieleza namna utawala wa Mahakama hiyo
ulivyoachana na matumizi ya karatasi kwa kutumia mifumo ya e-Office pamoja na mawasiliano ya
barua pepe.
Akitoa neno la shukrani
baada ya mawasilisho hayo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Joseph
Luambano, alisema ziara hiyo imekuwa na manufaa makubwa kwao kutokana na
mafunzo waliopata kuhusu matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa haki.
“Kufuatia ziara hii ya
kubadilishana uzoefu, tumejifunza mambo mengi yenye kujenga na kutuonesha
maeneo tunayopaswa kuboresha katika matumizi ya TEHAMA. Tunaahidi kuwa walimu
kwa wengine na kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati kwa kuzingatia taratibu bila
kumuathiri mtu yeyote,” alisema Mhe. Luambano.
Ziara hiyo iliongozwa na Mhe. Luambano, pamoja na Mtendaji wa Mahakama, Liad Chamshama, na watumishi wawakilishi kutoka kada mbalimbali za Mahakama ya Njombe.
Jaji
wa Mahakama ya Tanzania, Masjala Ndogo
Geita,
Mhe. Griffin Mwakapeje,
akifungua mafunzo.
Naibu
Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala
Ndogo Geita, Mhe. Fredrick Lukuna,
akitoa ufafanuzi juu ya ushirikiano biana ya Viongozi
na Watumishi unavyoleta mafanikio katika
kuongeza ufanisi wa matimizi ya Tekinolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).
Naibu
Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo
Njombe, Mhe. Joseph Luambano, akitoa neno la shukrani kwa uongozi wa Mahakama Geita.
Hakimu
Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Geita,
Mhe. Mujuni Muchunguzi, akielezea namna Mahakama za Wilaya
zilivyoachana na matumizi ya karatasi katika uendeshaji wa kesi na shughuli za
kiutawala.
Hakimu
Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo
Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, akilekeza jinsi Mahakama za Mwanzo
zilivyoachana na matumizi ya karatasi.
Kaimu
Mtendaji wa Mahakama Geita,
Bi. Happines Mushi,
akielezea namna utawala
ulivyoachana na matumizi ya karatasi.
Ofisa
Kumbukumbu, Bi. Winifrida Warsha, akiekelezea huduma ya KIOSK
inavyowasaidia wananchi
kusajili kesi na kuelewa mienendo ya kesi.
Picha
ya pamoja ya Watumishi wa Mahakama Kuu Geita na
watumishi wa Mahakama Kuu Njombe katika jengo
la Kituo Jumuishi
cha Utoaji Haki Geita.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni