Na. HALIMA MNETE & INNOCENT KANSHA - Mahakama
●
Toyota Hilux mpya
kuongeza ufanisi wa ufuatiliaji, tathmini na usimamizi wa shughuli za
kimahakama nchini
Mahakama ya Tanzania imepokea rasmi gari jipya aina ya
Toyota Hilux 2.4 GD Pick Up Double Cabin kutoka Mradi wa Building Sustainable Anti-Corruption
Action Programme (BSAAT) katika hatua inayotarajiwa kuongeza ufanisi wa
ufuatiliaji wa shughuli za mapambano dhidi ya rushwa na kuimarisha utoaji wa
haki nchini.
Makabidhiano hayo yamefanyika tarehe 22 Juni, 2026, katika
ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma,
yakihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Mahakama, menejimenti ya Mahakama na
waratibu wa programu au mradi wa BSAAT pamoja na watumishi wa Mahakama Makao
Makuu.
Akizungumza katika hafla hiyo, Msajili Mkuu wa Mahakama ya
Tanzania Mhe. Eva Nkya alisema kuwa gari hilo ni nyenzo muhimu itakayosaidia
Mahakama kutekeleza kwa ufanisi shughuli za ufuatiliaji na tathmini (Monitoring
and Evaluation), hususan katika maeneo ya mbali ambayo awali yalikuwa na
changamoto za kufikika.
Mhe. Nkya alisema kuwa, uwezeshaji huo unaonesha dhamira ya
dhati ya Serikali ya Tanzania ya kuendelea kuimarisha mifumo ya utoaji haki kwa
kuhakikisha taasisi za kisheria zinapata rasilimali muhimu za kuboresha
utendaji wake.
“Kupatikana kwa gari hili kutaongeza kwa kiasi kikubwa uwezo
wa Mahakama kufanya ziara za ufuatiliaji, usimamizi wa shughuli za mradi,
uhakiki wa taarifa pamoja na tathmini ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za
BSAAT katika maeneo tofauti nchini,” alisema Msajili Mkuu.
Aidha, alibainisha kuwa mchango wa BSAAT ndani ya Mahakama
umeleta mageuzi makubwa katika kuimarisha uwezo wa taasisi kushughulikia
mashauri ya rushwa kubwa na uhalifu wa kiuchumi kwa ufanisi zaidi.
Mhe. Nkya aliongeza kuwa, miongoni mwa mafanikio yaliyotajwa
ni kuimarishwa kwa Programu ya Ulezi na Ushauri wa Kitaaluma kwa Majaji na
Mahakimu (Judicial Mentorship Programme), ambayo imeongeza ubadilishanaji wa
maarifa, kuimarisha maadili ya kazi na kuboresha usimamizi wa mashauri magumu
ya rushwa.
Mbali na hilo, Msajili Mkuu ameeleza kuwa, mradi wa BSAAT
umechangia pia kukuza matumizi ya teknolojia kupitia Mfumo wa Tafsiri na
Unukuzi wa Kesi (Translation and Transcription System – TTS), ambao umeongeza
usahihi wa kumbukumbu za mashauri na kuharakisha mwenendo wa usikilizwaji wa
kesi.
Mhe. Nkya alisisitiza kuwa gari hilo si tu chombo cha
usafiri, bali ni sehemu ya uwekezaji wa kimkakati unaolenga kuhakikisha
mafanikio yaliyopatikana kupitia BSAAT yanaendelea kudumu hata baada ya mradi
huo kufungwa rasmi mwezi Septemba 2026.
“Zaidi ya kuwa nyenzo ya usafiri, gari hili ni uwekezaji wa
kimkakati unaolenga kuhakikisha uendelevu wa mafanikio ya BSAAT ndani ya
Mahakama,” ameongeza Mhe. Nkya.
Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi wa BSAAT Tanzania, Dkt.
Boneventure Baya, amesema ushirikiano kati ya mradi huo na Mahakama umeendelea
kuzaa matokeo chanya katika juhudi za kujenga taasisi zenye uwajibikaji, uwazi
na uadilifu.
Dkt. Baya alisema ni jambo la busara kwa taasisi
zinazonufaika na miradi ya maendeleo kuweka mikakati ya uendelevu na
uwajibikaji, akisisitiza kuwa Mahakama imekuwa mfano bora kwa kuwa tayari
imeandaa mpango mahsusi wa kuhakikisha mafanikio yaliyopatikana kupitia BSAAT
yanabaki kuwa sehemu ya mfumo wa kawaida wa utendaji wake.
“Itakuwa busara zaidi kwa taasisi zinazonufaika na miradi
kama huu kuweka utaratibu mzuri wa sustainability na accountability. Mahakama
ya Tanzania imeonesha mfano mzuri kwa kuwa tayari imeandaa mpango wa uendelevu
na kuhakikisha mafanikio haya yanabaki na kuendelezwa hata baada ya mradi
kufungwa,” amesema Dkt. Baya.
Aidha, ameongeza kuwa, Mahakama ya Tanzania imekuwa taasisi
ya kipekee katika utekelezaji wa mradi huo, jambo lililopelekea kuwa taasisi
pekee iliyoidhinishwa kunufaika na gari hilo kutokana na kiwango chake cha
maandalizi, usimamizi mzuri wa rasilimali na dhamira ya kuendeleza matokeo ya
mradi.
“Mahakama iko mbele, imejipanga na imeonesha utayari wa
kulinda na kuendeleza mafanikio haya. Hii ndiyo sababu imekuwa taasisi pekee
iliyokubalika katika mpango huu wa kupata gari,” amesema Dkt. Baya
Makabidhiano hayo yanaendelea kuthibitisha dhamira ya
Mahakama ya Tanzania ya kuimarisha uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika utoaji
wa haki, huku ikiendelea kujenga mifumo imara ya kupambana na rushwa na kuimarisha
imani ya wananchi kwa Mhimili huo muhimu wa Dola.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya akitoa hotuba fupi ya kuushukuru mradi wa BSSAT kwa kutoa gari jipya aina ya Toyota Hilux 2.4 GD Pick Up Double Cabin kwa ajili ya kuendeleza mapambano dhidi ya rushwa nchini.
(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni