Jumanne, 23 Juni 2026

JAJI MFAWIDHI DODOMA AFUNGUA MAFUNZO YA UKATILI WA KIJINSIA

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, jana tarehe 22 Juni, 2026, amefungua mafunzo yanayowakutanisha Maafisa wa Mahakama na Ustawi wa Jamii kwa lengo la kuimarisha uwezo wa kushughulikia kesi za unyanyasaji wa kingono na ukatili wa kijinsia kwa kuzingatia hali na mahitaji ya manusura.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo ya siku tatu katika Ukumbi wa Mikutano uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki, Jaji Tiganga alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu katika kuimarisha utoaji wa haki wenye kuzingatia utu, heshima na ustawi wa manusura wa ukatili wa kijinsia.

Alisisitiza kuwa Watumishi wa Mahakama na Maafisa Ustawi wa Jamii wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha wahanga wanapata huduma za haki katika mazingira salama na yenye huruma.

Alieleza kuwa Mahakama ya Tanzania inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha upatikanaji wa haki kwa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi, ikiwa ni pamoja na kuimarisha uwezo wa Watumishi wake kupitia mafunzo ya mara kwa mara.

Jaji Tiganga aliwataka washiriki kutumia vyema fursa hiyo kwa kushiriki kikamilifu katika mijadala na kubadilishana uzoefu utakaosaidia kuboresha utendaji kazi wao wa kila siku.

Aidha, aliwahimiza kuyafikisha maarifa watakayopata kwa Watumishi wenzao katika vituo vyao vya kazi ili kuongeza manufaa ya mafunzo hayo kwa sekta nzima ya utoaji haki.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Irish Rule of Law International (IRLI) na yanalenga kuwajengea washiriki uelewa wa mbinu zinazosaidia kuepusha kuamsha upya maumivu ya kisaikolojia kwa manusura wa ukatili wa kingono na kijinsia wanapopitia mchakato wa utoaji haki.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga akizungumza wakati akifungua mafunzo ya ukatili wa kijinsia Dodoma.

 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (wa katikati waliokaa).  Kulia kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe Victoria Nongwa, ambaye pia ni Mkufunzi wa mafunzo hayo. Aliyeketi kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri wakiwa kwenye picha ya pamoja na Wakufunzi wa mafunzo hayo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (wa katikati waliokaa).  Kulia kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe Victoria Nongwa, ambaye pia ni Mkufunzi wa mafunzo hayo. Aliyeketi kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri wakiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo.


 

Baadhi ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo ya ukatili wa kijinsia.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni