- Ataka huduma kutolewa kwa haraka
Na FAUSTINE KAPAMA
na Noel Daud-Mahakama, Songea
Jaji Kiongozi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amewahimiza
Watumishi wa Mahakama ya Tanzania kwenda na kasi ya maendelea na kukua kwa
shughuli za kiuchumi katika maeneo mbalimbali nchini.
Mhe. Dkt. Siyani
ametoa wito huo leo tarehe 23 Juni, 2026 mjini Mbinga, alipokuwa anazungumza na
Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbinga katika siku ya pili ya ziara yake ya
kimahakama, kukagua Mahakama na Magereza mkoani Ruvuma.
“Shughuli za
kiuchumi zinapokuwa kubwa kama kwenye Mji wa Mbinga, mashauri kama ya mirathi,
ardhi ambayo ni mengi, shughuli za kibiashara na mikataba, yatakuja mahakamani.
Mahakama lazima iendane na kasi hiyo ya kukua kwa uchumi,” amesema.
Amewaambia
Watumishi hao kuwa ili kuendana na kasi ya maendeleo ambayo Wananchi
wanajifanyia na Serikali inawezesha, kuna mambo ambayo uongozi wa Mahakama
unaweza kufanya kama kuboresha maslahi na miundombinu, hivyo wao kama watoa
huduma hawatakiwi kuachwa nyuma.
“Kwa hiyo, ni
waombe inapowezekana, sisi tutagulie. Siyo tu tuende na kasi ya kukua kwa
uchumi na shughuli za watu, ikiwezekana sisi tutangulie mbele, tusiwe tunafukuza
maendeleo,” Jaji Kiongozi amesema.
Amesisitiza kuwa Mahakama
inatakiwa kuwa kinara wa kuonesha njia, ili watu wakifika mahakamani waone,
pamoja na uchakavu wa miundombinu iliyopo, wasiwakute Watumishi wakiwa wanyonge,
bali wapate huduma na waondoke wakiwa wameridhika.
“Huduma zitolewe haraka,
mashauri yasichukue muda mrefu mahakamani, kwa kadri inanyowezekana tutoe haki
mapema na tuweke mazingira ya kuwa na wepesi wa kupatikana huduma zenyewe,” Mhe.
Dkt. Siyani amesema.
Aidha, Jaji
Kiongozi amewataka Watumishi wa Mahakama kutokuwa kikwazo kwa watu kuja mahakamani
na pia wanapaswa kujiuliza ni kwa namna gani kila mmoja anapokea Wananchi
wanaokuja mahakamani na jinsi gani anavyotoa huduma bila kuwa na upendeleo.
Amebainisha kuwa Watumishi
wa Mahakama wanapaswa kutambua kuwa wao ni sehemu ya Mahakama, kwani wakitoa
huduma vizuri Mahakama na wao binafsi watapata sifa, tofauti na hivyo Mahakama itachafuka.
“Kila Mtumishi anatakiwa
kujua kuwa anao mchango anaopaswa kuutoa ili kuboresha huduma za Mahakama na hivyo
kujenga imani ya umma kwa Mahakama. Msipofanya hivyo, watu hawatawaheshimu na
Mahakama haitapewa hadhi inayostahiki,” amesisitiza.
Akizungumzia
matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Jaji Kiongozi
amewaeleza Watumishi hao kuwa pamoja na ugumu wa miundombinu na mazingira
yaliyopo, Mahakama haiwezi kurudi nyuma.
Mhe. Dkt. Siyani amewapongeza
Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbinga kwa kazi nzuri wanaoifanya, kwani
taarifa ya utendaji iliyowasilishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mhe. Lome
Mwapemela, imeonesha kutokuwa na mlundikano wa mashauri na Wananchi wa Mbinga
wanaendelea kupata huduma za haki.
Kwenye taarifa
yake, Mhe. Mwapemela ameeleza kuwa mashauri yaliyobaki Desemba, 2025 katika
ngazi ya Mahakama ya Wilaya yalikuwa 30, yaliyofunguliwa kati ya Januari 2026
hadi Juni 19, 2026, yalikuwa 77 na yaliyoamuriwa kwa kipindi hicho ni 84.
Kwa mujibu wa
taaarifa hiyo, hapakuwepo na mashauri yaliyovuka mwaka 2025 katika ngazi ya
Mahakama za Mwanzo na mashauri yaliyofunguliwa kati ya Januari na Juni 19, 2026
yalikuwa 425 na yaliyoamuriwa ni 376.
Hakimu Mfawidhi
ameeleza pia kuwa, kwa kipindi cha Januari hadi Juni 19, 2026, mashauri ya
mirathi sita yamefungwa kati ya mashauri 14 ambayo uteuzi wa msimamizi wa
mirathi umefanyika. Amebanisha kuwa kati ya mashauri hayo, mawili ni ya Mahakama
za Mwanzo na mashauri nne ni Mahakama ya Wilaya.
“Mashauri ambayo
hayajafungwa bado Wasimamizi wapo ndani ya muda wa kutekeleza majukumu yao. Tumekuwa
tukichukua namba za simu za Msimamizi wa Mirathi na za watu wao wa karibu ili kuhakikisha
wanapatikana baada ya kuteuliwa,” ameeleza.
Katika siku hiyo
ya pili ya ziara yake, Jaji Kiongozi pia ametembelea Magereza mawili ya Mkwaya na
Kitai, yote yakiwa katika Wilaya ya Mbinga. Akiwa kwenye Magereza hayo, Jaji
Kiongozi amepokea changamoto mbalimbali za Wafungwa, ambazo amezipatia ufunguzi
papo kwa papo.
Aidha, Jaji
Kiongozi ametumia fursa hiyo kuwaomba Wafungwa watakaobahatika kutoka wawe raia
wema, kwani kukaa kwao gerezni hakuna faida kwa nchi.
Katika ziara hiyo,
Jaji Kiongozi ameambatana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala
Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel
Kawishe, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa na Naibu
Wasajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele na Mhe. Asha Waziri.
Wengine ni Mtendaji
wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za
Wilaya ya Nyasa na Mbinga Songea na Watumishi wengine wa Mahakama Songea.
Kesho tarehe 24
Juni, 2026, Jaji kiongozi anatarajia kuendelea na ziara yake kwa kukutana na
Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mhe. Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, na baadaye
kufanya ukaguzi katika Gereza Kuu Songea na kisha kutembelea Mahakama Kuu
Songea na kuongea na Watumishi.














Hakuna maoni:
Chapisha Maoni