Jumanne, 30 Juni 2026

CHAMA CHA MADALALI NA WASAMBAZA NYARAKA ZA MAHAKAMA CHAOMBA KULINDWA KISHERIA

  •    Chawasilisha Mapendekezo Saba kwa Jaji Mkuu

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Chama cha Madalali wa Mahakama na Wasambaza Nyaraka za Mahakama Tanzania kimeiomba Mahakama kusimamia ipasavyo Sheria na taratibu ili kulinda usalama wao, heshima ya amri za Mahakama na kuboresha mfumo wa utoaji haki nchini.

Akizungumza mbele ya Mgeni Rasmi, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 30 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mwenyekiti wa Chama hicho, Bi. Mwamvua Kigulu amesema kuwa, Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama ni nguzo muhimu kwani hukumu haiwezi kufikia lengo lake bila utekelezaji, na mashauri hayawezi kusonga mbele bila usambazaji sahihi wa nyaraka.

Bi. Mwamvua ametaja Changamoto na Mapendekezo saba kwa Mahakama ili kuimarisha utendaji kazi na kulinda hadhi ya Mhimili huo, ambayo ni pamoja na kuomba Ulinzi wa Polisi Wakati wa Utekelezaji.

Chama hicho kimeomba Mahakama isimamie utekelezaji wa amri zake kwa kutoa ulinzi wa Polisi kwa Madalali, kwani katika baadhi ya maeneo amri hizo hazitekelezwi ipasavyo, jambo linalohatarisha usalama wao.

“Kuingiliwa na Viongozi wa Kisiasa na Serikali; kufuatia matukio ya kuingiliwa kwa amri halali za Mahakama kabla na baada ya kutekelezwa, Chama kinaomba Mahakama kutoa Mwongozo thabiti kuwa hakuna mamlaka inayoruhusiwa kuzuia utekelezaji huo isipokuwa kwa mujibu wa sheria,” amesema Mwenyekiti huyo.

Kadhalika, Chama hicho kimeomba kudhibiti Wavamizi wa Kazi ya Usambazaji Nyaraka: ambapo kimesikitishwa na tabia ya baadhi ya Mawakili na Makarani wa Mahakama kufanya kazi ya usambazaji nyaraka wakati hawajateuliwa kisheria hivyo wameomba sheria isimamiwe ipasavyo ili kazi hiyo ifanywe na Wasambaza Nyaraka waliosajiliwa pekee.

Aidha, Bi. Mwamvua ametaja pendekezo lingine la kuomba kuongezeka kwa Muda wa Kuhuisha Leseni ambapo Chama hicho kimeomba muda wa kuhuisha leseni zao uongezwe na kuwa miaka mitatu (3) kwa nyaraka zinazoisha muda wake ili kupunguza gharama, kwa kuwa wote wapo chini ya sheria moja.

Kuhusu Gharama za Uhifadhi (Storage), wamependekeza gharama za uhifadhi zilipwe kuanzia siku ya kwanza mali inapokamatwa, kwa kuwa gharama za maghala, ulinzi na bima hulipiwa mwaka mzima na usimamizi ukiacha hapo hapo.

Kadhalika, Mwenyekiti huyo amebainisha juu ya changamoto ya Gharama za Utekelezaji (GN Na. 363 ya 2017) ambapo Chama hicho kimeomba malipo ya utekelezaji yaendelee kulipwa bila kuwekewa ukomo wa asilimia, bali yalipwe kwa uwazi na haki kama yalivyoainishwa kwenye Kanuni za Serikali (GN Na. 363 za Mwaka 2017).

Aidha, Bi. Mwamvua ameishukuru Mahakama ya Tanzania kupitia Chuo cha Uongozi wa Mahakama kwa kuwapatia mafunzo ya mara kwa mara na kuomba mafunzo hayo kuwa endelevu ili kuendelea kuongeza weledi, uwajibikaji na ubora wa huduma kwa wananchi.

Chama hicho kupitia Mwenyekiti huyo kimemshukuru Jaji Mkuu, Mhe. Masaju kwa kuwasikiliza na kuahidi kuendelea kushirikiana bega kwa bega na Mahakama katika kusimamia utawala wa sheria nchini Tanzania.

Mwenyekiti wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania, Bi. Mwamvua Kigulu akitoa neno la utangulizi wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama hicho leo tarehe 30 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akisikiliza neno kutoka kwa Mwenyekiti wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania, Bi. Mwamvua Kigulu (hayupo katika picha) alipokuwa akitoa neno la utangulizi wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama hicho leo tarehe 30 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma.


Sehemu ya Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania wakifuatilia kinachojiri wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu leo tarehe 30 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

(Picha na MAY GWERA, Mahakama-Dodoma)








 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni