Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Kaimu
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma amewaasa Madalali
wa Mahakama na Wasambaza Nyaraka kufanya kazi zao kwa kuzingatia Uadilifu wa
hali ya juu na Sheria.
Mhe.
Mruma ametoa rai hiyo leo tarehe 30 Juni, 2026 alipokuwa akitoa neno kwa niaba
ya Jaji Kiongozi, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani wakati wa ufunguzi wa Mkutano
Mkuu wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania uliofanyika
kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
"Mkikosa
uadilifu katika hilo, mnatengeneza mazingira rahisi kwa watu wa Mihimili
mingine kuingilia Mhimili wa Mahakama na kuhalalisha uingiliaji wao," amesema
Jaji Mruma.
Akizungumza
kwa niaba ya Jaji Kiongozi ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Uteuzi na Nidhamu
ya Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama, Mhe. Mruma amebainisha kuwa,
utekelezaji wa hukumu za madai unategemea kwa kiasi kikubwa utendaji wa Madalali
hao, na kwamba bila wao, mnyororo wa utoaji haki unakuwa haujakamilika.
Jaji
Mruma amesema, katika miaka ya karibuni, kumeonekana kuwepo kwa changamoto
kubwa ya Viongozi wa Kisiasa—hasa wanaotumia nyadhifa zao kama Wenyeviti wa Kamati
za Ulinzi na Usalama—kuingilia utekelezaji wa amri za Mahakama.
Akieleza
jinsi ya kukabiliana na hali hiyo, amewataka Madalali kujiamini na kutumia
sheria kuchukua hatua dhidi ya yeyote anayewakwamisha.
"Sheria
inawaruhusu kuwachukulia hatua watu wanaoingilia utendaji wenu kwa njia ya
dharau kwa Mahakama (contempt of court). Kumzuia Ofisa yeyote wa Mahakama
kutekeleza amri halali ni kosa, na tunategemea mchukue hatua za kisheria ili
kukomesha hali hii mara moja na kwa mara zote," amesisitiza.
Pamoja
na kuwataka Madalali hao kuwa wajasiri, Mhe. Mruma ameeleza kuwa, uhuru wao wa
kufanya kazi na ulinzi wa kisheria unaweza tu kulindwa ikiwa wao wenyewe wataonesha
uadilifu wa hali ya juu.
Ametaja
maeneo yanayolalamikiwa zaidi kuwa ni pamoja na: Ukamataji na Uhifadhi wa Mali
ambapo Mali kukamatwa na kutofikishwa kwenye yadi za Madalali, na wakati
mwingine kupotea.
Kaimu
Jaji Kiongozi huyo ametaja eneo lingine linalolalamikiwa kuwa ni Uuzaji wa Mali
chini ya Kiwango: Mali kuuzwa kwa bei isiyo ya soko au isiyozingatia tathmini
halisi.
“Ukiukwaji
wa Taratibu za Uondoaji, baadhi ya madalali wasio waadilifu kufunga nyumba au
kutoa watu nje bila kuwa na amri maalum ya uondoaji badala ya kuweka tu tangazo
la zuio la Mahakama,” amesema.
Ameongeza
kuwa, ili kuimarisha usalama na hadhi ya Madalali hao, Mahakama inaangalia
uwezekano wa Kisheria wa kuwatambua rasmi watendaji hao kama Maofisa kamili wa Mahakama
ili wapate ulinzi thabiti wa kisheria wakati wa kutekeleza majukumu yao.
Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma akitoa neno wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania uliofanyika leo tarehe 30 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.



Hakuna maoni:
Chapisha Maoni