Alhamisi, 25 Juni 2026

JAJI KIONGOZI ATAKA MIUNDOMBINU MIPYA IENDANE NA HUDUMA BORA ZINAZOTOLEWA

  • Awataka Watumishi kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu, kuwajibika kwa weledi

Na FAUSTINE KAPAMA na Noel Daud-Mahakama, Songea

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amewataka Watumishi wa Mahakama ya Tanzania kutoa huduma zinazoendana na ubora wa miundombinu ambayo imejengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Mhe. Dkt. Siyani ametoa wito huo leo tarehe 24 Juni, 2026 mjini Songea, alipokuwa anazungumza na Watumishi wa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo mjini Songea katika ziara yake ya kimahakama, kukagua Mahakama na Magereza mkoani Ruvuma.

“Miundombinu hii mipya michache tutakatoipata, itakayotutoa katika majengo ya zamani inatokana na fedha ambazo Serikali inaiwezesha Mahakama kupitia mikopo kutoka Benki ya Dunia na fedha za maendeleo ambazo Serikali inazileta. Miundombinu hii iendane na ubora wa huduma zitakazokuwa zinatolewa,” amesema.

Jaji Kiongozi ameagiza kuwa wale wote wanaokwenda kufanya kazi katika miunombinu hiyo, iwe Songea au sehemu yoyote nchini, huduma wanazozitoa ziendane na ubora wa majengo hayo.

Mhe. Dkt. Siyani amebainisha kuwa fedha nyingi zimewekezwa kwenye miradi hiyo, hivyo haitakuwa sawa kwa Watumishi kuchuku changamoto zao walizokuwa nazo miaka yote na kuzihamishia kwenye majengo hayo.

“Uwekezaji mkubwa uliofanyika Songea na maeneo mengine nchini hautakuwa na maana yoyote kama huduma zetu zitakuwa za kiwango cha chini, kwa hiyo, nawakumbusha kuwa tutaendelea kufanya kila linalowezekana kuboresha miundombinu,” Jaji Kiongozi amesema.

Amewahimiza Watumishi wa Mahakama Songea kwenda kujifunza kwa wenzao waliotangulia kama Geita na Simiyu, ambao wameonesha mfano na hawajahamishia matatizo yao kwenye majengo hayo mapya.

Jaji Kiongozi amesema kuwa mwaka huu wa 2026 wameanzisha Mahakama nyingine tano, Lindi, Katavi, Njuombe, Songwe na Singida na kote wamewaambia mambo kama hayo.

Mhe. Dkt. Siyani amewapongeza Watumishi wa Mahakama mjini Songea kwa kazi nzuri wanaoifanya, kwani taarifa ya utendaji iliyowasilishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, imeonesha mafanikio makubwa yaliyofikiwa.

Kwenye taarifa yake, Mhe. Karayemaha ameeleza kuwa kwa Mwaka 2025, Masjala Ndogo ya Songea ilibakiwa na mashauri 250, yaliyosajiliwa kuanzia mwezi Januari hadi Juni 19, 2026 ni mashauri 531, yaliyosikilizwa ni 485 na hadi kufikia Juni 19, 2026 idadi ya mashauri yaliyobaki ni 296.

Akizungumzia upade wa Mahakama Kuu, Jaji Mfawidhi ameeleza kuwa mashauri yaliyobaki kwa mwaka 2025 ni 156, yaliyopokelewa Januari hadi Juni ni 174, yaliyosikilizwa 150 na yaliyobaki ni 180.

Kati ya mashauri 180 yaliyobaki, amesema, yaliyopo mbele ya Majaji ni 155 na 15 yapo mbele ya Naibu Msajili (mashauri ya kukaza hukumu saba, maombi ya gharama saba na maombi ya kawaida shauri moja).

Akizungumzia upande wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya, Jaji Mfawidhi ameeleza kuwa kwa mwaka 2025, Mahakama hizo zilibakiwa na mashauri 94, kuanzia mwezi Januari 2026 hadi Juni 19, 2026 zimesajili mashauri 357, zimesikiliza 334 na zimebakiwa na mashauri 117.

Ameeleza pia kuwa Mahakama za Mwanzo kwa mwaka 2025 hazikubakiwa na mashauri, kuanzia mwezi Januari 2026 hadi Juni 19, 2062 zimesajili jumla ya mashauri 2,530, zimesikiliza 2, 305 na zimebakiwa na mashauri 227.

Aidha, Jaji Mfawidhi amebainisha baadhi ya mafanikio yaliyopatikana kama kusimamia na kuratibu uharakishwaji wa usikilizaji na umalizaji mashauri kwa wakati kwa ngazi zote za Mahakam ana kutoa elimu kwa jamii kuhusu huduma za kimahakama.

Mengine ni kurejesha huduma kwa Mahakama ambazo zilikuwa hazifanyi kazi kwa muda ambazo ni Mahakama za Mwanzo Chiwanda, Lukumbule, Namasakata, Myangayanga, Magazini na Wabaki na kufanya ukaguzi wa Mahakama katika ngazi zote na kufanya utatuzi kwa changamoto zinazojitokeza.

Mafanikio mengine ni kusikiliza mashauri 558 kwa njia ya Mkutano Mtandao, kuhakikisha upatikanaji wa vitendea kazi, kufanya ukarabati wa majengo ya Mahakama mbili za Mwanzo Mfaranyaki na Mpambano na kuwa na ushirikiano mzuri na Wadau.

Wakati huo huo, Jaji Kiongozi amewakumbusha Watumishi wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu, kuwajibika kwa weledi na kutoitia madoa Mahakama.

Mhe. Dkt. Siyani ametoa wito huo alipokwa anazungumza na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Namtumbo, kama sehemu ya ziara yake ya kimahakama, kutembelea Mahakama na Magereza katika Mkoa wa Ruvuma.

Amewaambia Watumishi wa Mahakama hiyo kuwa wanapaswa kuwa mfano kwa Watumishiwanaotoa huduma bora kwani mazingira waliyonayo hayafanani na maeneo mengine katika Mkoa huo.

“Fanyeni kazi na msiitie doa Mahakama yenu. Mnapswa katika mazingira yenu kuwa vinara katika maboresho. Kuweni wabunifu ambao utaongeza tija kwenye utendaji wetu, msifanye kazi kwa mazoea,” Mhe. Dkt. Siyani amesema.

Akiwa katika Mahakama hiyo, Jaji Kiongozi pia alipokea taarifa ya utendaji iliyowasilishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mhe. Gloria Lwomile. Katika taarifa yake, Mhe. Lwomile ameeleza kuwa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo Namtumbo kwa pamoja zimezingatia umalizaji wa mashauri kwa wakati kulingana na ukomo wa muda.

“Ngazi zote za Mahakama hazina mashauri ya muda mrefu. Tunao mkakati binafsi wa kumaliza mashauri katika Wilaya ambapo; ukomo wa Mahakama ya Wilaya ni siku sitini na ukomo wa Mahakama ya Mwanzo ni siku 45,” amesema.

Hakimu Mfawidhi ameeleza pia kuwa usajili na uondoaji wa mashauri katika mfumo unatekelezwa ipasavyo katika ngazi zote na mashauri ya mirathi pia yanaendelea kufungwa; yaliyobaki bila kufungwa 2025 yapo 11 pekee.

“Utekelezaji wa hukumu pia umezingatia na kusimamiwa vema. Kwa sasa tuna shauri moja tu la utekelezaji wa hukumu ambalo linaendelea kusubiri utekelezaji. Shauri hili limechelewa kutokana na kukosekana kwa mnunuzi,” amesema.

Katika ziara yake, Jaji Kiongozi pia ametembelea Gereza la Songea na kukutana na Wafungwa na Mahabusu. Baada ya kupokea taaraifa ha lai ya Gereza kutoka kwa Mkuu wa Gereza hilo, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza, Afande Robert Mabeja, Mhe. Dkt. Siyani alipokea changamboto mbalimbali na kuzitolea ufafanuzi na ufumbuzi wa papo kwa papo.

Wafungwa na Mahabusu hao wameonekana kufurahishwa na ujio wa Jaji Kiongozi na ujumbe wake kwani wamepata nafasi ya kueleza kero zao kwa uwazi bila kuingiliwa na mtu yoyote.

Aidha, Jaji Kiongozi ametumia fursa hiyo kurudia wito wake kwa Wafungwa watakaobahatika kutoka gerezani wawe raia wema, kwani kukaa kwao huko ni hasara kwao binafsi na kwa Taifa kwa ujumla.

Katika ziara hiyo, Jaji Kiongozi ameambatana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa na Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele na Mhe. Asha Waziri.

Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mfawizi na Wilaya Songea na Watumishi wengine wa Mahakama Songea.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akizungumza na Watumishi wa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo mjini Songea katika ziara yake ya kimahakama, kukagua Mahakama na Magereza mkoani Ruvuma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, akiwasilisha taarifa ya utendaji wa Mahakama Songea kewenye kikao hicho.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama Songea wakiwa kwenye kikao hicho.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akisalimiana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Namtumbo, Mhe. Gloria Lwomile, baada ya kuwasili kwenye Mahakama hiyo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, (katikati mstari wa mbele) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama Namtumbo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiwasili kwenye Gereza la Songea kufanya ukakguzi na kuzungumza na Wafungwa na Mahabusu.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiwa katika picha ya pamoja na Wadau baada ya kutembelea Gereza la Songea.

 Picha na Magoiga Mtatiro-Mahakama, Songea.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni