Jumatatu, 15 Juni 2026

JAJI MFAWIDHI MPYA GEITA APOKELEWA RASMI OFISINI

Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, tarehe 12 Juni 2026 alikabidhi ofisi kwa Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Projestus Kahyoza, baada ya kuripoti katika kituo chake kipya cha kazi.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano, Mhe. Mhina alisema kuwa taratibu zote za kikazi na taarifa muhimu za ofisi zilishakabidhiwa kwa njia ya barua pepe za kikazi.

Aidha, alibainisha kuwa anamwachia Jaji Kahyoza timu ya Watumishi wenye ushirikiano mkubwa na wenye kujituma katika kuhakikisha majukumu ya Mahakama yanatekelezwa kwa ufanisi.

“Nimekuachia Watumishi wenye ushirikiano mzuri sana ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa kujituma na kuhakikisha huduma za utoaji haki zinaendelea kutolewa kwa Wananchi kwa wakati,” alisema Mhe. Mhina.

Kwa upande wake, akizungumza wakati wa kumpokea Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Mwakapeje alimhakikishia ushirikiano wa hali na mali kutoka kwa Watumishi wote wa Mahakama Geita.

Alieleza kuwa Watumishi wa Mahakama hiyo ni wenye maadili mema na wako tayari kushirikiana ili kuhakikisha majukumu ya Mahakama yanaendelea kutekelezwa kwa ufanisi.

Akizungumza baada ya kupokea ofisi, Mhe. Kahyoza aliwashukuru Viongozi na Watumishi wote wa Mahakama Geita kwa mapokezi mazuri aliyoyapata. Alisisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano uliopo ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa Wananchi.

“Naomba tuendelee kushirikiana kwa dhati ili kuendeleza mafanikio yaliyopatikana na kuimarisha zaidi utoaji wa haki kwa wakati kwa kutumia mifumo ya Teknolojia ya Habari na mawasiliano (TEHAMA),” alisema Mhe. Kahyoza.

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, alimpongeza Jaji Kahyoza kwa kuaminiwa na kuteuliwa kuongoza Mahakama Geita. Alimhakikishia kuwa Watumishi wa Mahakama wataendelea kumpa ushirikiano unaohitajika ili kufanikisha majukumu yake mapya.

Mhe. Lukuna pia alieleza kuwa Mahakama Geita itaendelea kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika shughuli za Mahakama kwa lengo la kuongeza ufanisi na kuboresha huduma kwa Wananchi.

Katika kuonyesha furaha ya ujio wake, Watumishi wa Mahakama Kuu Geita waliandaa keki maalum kwa ajili ya kumkaribisha Jaji Mfawidhi mpya katika kituo chake kipya cha kazi.

Makabidhiano hayo yanaashiria mwanzo wa hatua mpya ya uongozi katika Mahakama Geita, huku yakionesha dhamira ya kuendeleza ushirikiano, ubunifu na matumizi ya teknolojia katika kuimarisha utoaji wa haki kwa Wananchi.

Watumishi wa Mahakama Kuu Geita wakimpokea Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Projestus Kahyoza.

Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Projestus  Kahyoza akisaini kitabu baada ya kuripoti katika kituo chake kipya.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Geita, Mhe Kevin Mhina, akipeana mkono kama ishara ya makabidhiano na Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Projestus Kahyoza.

Picha ya Majaji.

Keki iliyoandaliwa kumkaribisha Jaji Mfawidhi, Mhe. Projestus Kahyoza.

Watumishi wa Mahakama Kuu Geita wakiwa katika kikao kifupi cha kumpokea Jaji Mfawidhi mpya.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni