Na. SHARIFU MOKIWA – Mahakama, Sumbawanga
Watumishi na Viongozi wa Mahakama wampongeza Mhe. Kisasila Saguda kwa kuteuliwa
kwake kuwa Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, katka hafla iliyofanyika katika ukumbi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga.
katika hafla hiyo maalumu ya kumpongeza Mhe. Saguda iliwakutanisha
Watumishi na Viongozi mbalimbali wa Mahakama ili kumpongeza aliyekuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa Sumbawanga kufuatia
kuteuliwa kwake kuwa Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania.
Hafla hiyo
ilifunguliwa
na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo
ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Manyanda na ilihudhuriwa na viongozi
mbalimbali wa Mahakama pamoja na watumishi kutoka Idara mbalimbali. Miongoni
mwa viongozi walioshiriki ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya
Sumbawanga, Mhe. Thadeo Mwenempazi, Mtendaji
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Bw. Machumu
Essaba, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya
Sumbawanga Mhe, Pamela Mazengo pamoja na watumishi.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Saguda alitoa shukrani zake kwa
uongozi wa Mahakama kwa imani waliyoionesha kwake kupitia uteuzi huo, huku
akisisitiza umuhimu wa ushirikiano, upendo na uwajibikaji katika utendaji wa
kazi.
“Ushirikiano,
upendo na kazi vinakwenda pamoja, hivyo tusiviache nyuma. Napenda kushukuru
uongozi wa Mahakama kwa namna ambavyo wameniona nafaa kuchukua nafasi hii ya
Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania na ninaahidi kuwa nitahakikisha nachapa
kazi kuonyesha kwamba uteuzi walioufanya hawakukosea,” alisema Mhe. Saguda
Kwa upande
wake, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Mwenempazi, alimtakia kila la heri Mhe. Saguda katika majukumu yake mapya, akieleza kuwa
mafanikio aliyoyapata yametokana na utendaji wake mzuri wa kazi na mahusiano
mema na wenzake.
“Tunakutakia
kheri katika yote utakayoyatenda katika nafasi yako.
Lakini yote uliyokuwa unatufanyia sisi hapa, popote utakapoenda usisahau
kuyafanya hivyo, kwani baraka zako zimekuja kwa sababu ya hayo mazuri
uliyoyafanya,” alisema Mhe. Mwenempazi.
Naye Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Manyanda, alitumia fursa hiyo kueleza kanuni muhimu
zinazopaswa kuongoza maisha na utendaji wa Afisa wa Mahakama ili kufikia
mafanikio katika kazi.
“Kuna
kanuni sita ambazo Afisa wa Mahakama akiziishi lazima atafanikiwa; uhuru wa
kufanya jambo lolote bila kuingiliwa na bila uoga, kutokuwa na upendeleo,
uadilifu ambao ndiyo msingi wa majukumu yetu, mwenekano, usawa pamoja na
weledi. Hivyo sote tuzingatie kanuni hizi. Lakini pia namtakia kheri, naamini
anaweza, alistahili, anastahili na ataweza. Mwenyezi Mungu aendelee kumuinua
zaidi na zaidi,” alisema Jaji Manyanda.
Katika
kuonesha kuthamini mchango wake katika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Sumbawanga, Mhe. Saguda alipokea Kitabu maalum cha
kumbukumbu za utendaji kazi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga kutoka
kwa Jaji Mfawidhi Mhe. Manyanda. Kitabu hicho kinajumuisha historia ya utendaji kazi wa Mahakama hiyo
pamoja na picha na majina ya watumishi wake, ikiwa ni
sehemu ya kumbukumbu na ukumbusho wa ushirikiano na mchango wake.
Kwa ujumla,
hafla hiyo ilikuwa ishara ya kuthamini utumishi uliotukuka, kujenga moyo wa
kufanya kazi kwa bidii na kuhamasisha watumishi wengine kuendelea kutekeleza
majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kujituma kwa manufaa ya taasisi na
wananchi wanaohudumiwa na Mahakama.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Sumbawanga, Mhe Frederick Manyanda (aliyesimama) akitoa Nasaha fupi wakati wa hafla ya kumpongeza Mhe, Kisasila Saguda wakati wa pongezi hizo.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mteule Mhe. Kisasila Saguda aliyekuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa Sumbawanga akitoa Shukrani baada ya kuteuliwa kuwa Naibu
Msajili wa Mahakama ya Tanzania.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi akimpongeza na kumtakia kheri Mhe. Kisasila Saguda baada ya Uteuzi huo wa kuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo
ya Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo (aliyesimama) akitoa neno wakati wa afla
hiyo, kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Machumu Essaba na kushoto ni Mhe Kisasila
Saguda aliyeteuliwa kuwa Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda [kushoto] akimpatia kitabu Mhe. Kisasila
Saguda [Kulia] kikiwa na picha na majina ya watumishi wake, ikiwa
ni sehemu ya kumbukumbu.
Sehemu ya Watumishi wa Mahakama waliohudhulia katika hafla
hiyo maalum ya kumpongeza Mhe. Saguda kwa Uteuzi huo.

.png)
.png)



Hakuna maoni:
Chapisha Maoni