Jumanne, 16 Juni 2026

MAHAKAMA KUU GEITA YAMUAGA JAJI MFAWIDHI MHINA

Na DOTTO NKAJA –Mahakama,  Geita

Uongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjla Ndogo Geita hivi karibuni walifanya hafla ya kumuaga aliyekuwa Jaji Mfawidhi, Mhe. Kevin Mhina, kufuatia uhamisho wake wa kwenda kutekeleza majukumu katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara.

Hafla hiyo ilifanyika Juni 10, 2026, katika Viwanja vya Mahakama Kuu Geita. Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Mhina aliwashukuru wote kwa ushirikiano waliompatia katika kipindi chote cha utumishi wake. Alisema amefurahishwa na maandalizi ya hafla hiyo na kupongeza mshikamano ulioonyeshwa na Watumishi.

Aidha, aliwahimiza kuendelea kuzingatia maadili ya kazi, ushirikiano, utu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Pia alisisitiza umuhimu wa kuendeleza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuimarisha utoaji wa huduma za haki na kuifanya Mahakama Geita kuwa mfano katika matumizi ya teknolojia ndani ya Mhimili wa Mahakama.

Kwa niaba ya watumishi, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Griffin Mwakapeje, alimpongeza Mhe. Mhina kwa mchango wake mkubwa katika maendeleo ya Mahakama Geita, hususan katika kusimamia uanzishwaji wa Masjala ya Mahakama Kuu Geita.

Alisema uongozi wake wenye maono, uthabiti na kujitolea umechangia kuimarika kwa huduma za Mahakama na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa Wananchi.

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, alimpongeza Mhe. Mhina kwa juhudi zake katika kuhamasisha na kuendeleza matumizi ya TEHAMA katika shughuli za Mahakama.

Alisema maarifa, uongozi na moyo wake wa kusaidia wengine vimechangia kwa kiasi kikubwa kuboresha matumizi ya teknolojia katika uendeshaji wa mashauri, usikilizaji wa kesi na shughuli za kiutawala.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, alisema Mhe. Mhina ameacha alama ya uongozi bora kutokana na malezi ya kitaaluma, msimamo wake katika kusimamia maadili na weledi kazini, pamoja na juhudi zake za kuwajengea uwezo Watumishi.

Alibainisha kuwa uongozi wake umeweka msingi imara wa uwajibikaji, uadilifu na heshima katika mazingira ya kazi, hali iliyochangia kuimarika kwa utendaji wa Mahakama Geita.

Hafla hiyo ilihitimishwa kwa Viongozi na Watumishi mbalimbali kutoa salamu za shukrani na pongezi kwa Mhe. Mhina kwa mchango wake katika maendeleo ya Mahakama Geita, huku wakimtakia mafanikio zaidi katika majukumu yake mapya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina, akitoa shukurani.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akimulishakeki Jaji wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna Pamoja na Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama Kuu Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya Pamoja na watumishi wa mahakama ya wilaya Geita.

Picha Namba 7. Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chato.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Bukombe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Nyanghwale.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbogwe.

 Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni