Jumatatu, 8 Juni 2026

JAJI MFAWIDHI SONGWE AONGOZA HAFLA YA UZINDUZI WA MAHAKAMA YA MWANZO KANGA

Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama, Songwe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata aongoza hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga iliyopo Kata ya Kanga, Wilaya ya Songwe hivi karibuni

Hafla hiyo, ilifanyika katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Kanga na ilihudhuriwa na sehemu ya Viongozi wa ngazi ya Mkoa wa Songwe pamoja na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Marvis Miti.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Songwe Bw. Agapto Thomas Kilongosi alitoa pongezi kwa Mahakama ya Tanzania kwa kuendelea kuimarisha huduma za upatikanaji wa haki ikiwa ni pamoja na kukamilisha ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga na kuahidi kuendelea kushirikiana na Mahakama katika kuboresha upatikanaji wa haki katika Jimbo la Songwe.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Kanga Bw. Prosper Laurent Nkinga, aliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kusogeza huduma ya Mahakama katika Kata ya Kanga na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano na kulinda miundombinu ya Mahakama hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Songwe Mhe. Fadhili Nkurlu aliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kusogeza huduma ya upatikanaji wa haki katika Kata ya Kanga na maeneo ya Jirani kwa kujenga Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Mhe. Fadhili Nkurlu aliahidi kuendelea kushirikiana na Mahakama ikiwa ni pamoja na kulinda miundombinu ya Mahakama ili kuhakikisha huduma za utoaji wa haki zinatolewa ipasavyo katika Mahakama ya Mwanzo Kanga na Wilaya ya Songwe kwa ujumla.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Songwe Mhe. Jabiri Omari Makame alimshukuru Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga kwa ushirikiano aliouonesha wakati Mkoa wa Songwe ulipokuwa ukipata huduma za Mahakama kutoka Masjala Ndogo ya Mbeya, Pia alimkaribisha Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata na aliahidi kuendelea kutoa ushirikiano ili kufikisha huduma ya upatikaji wa haki kwa wanachi wa Mkoa wa Songwe.

Mkuu wa Mkoa huyo akatumia jukwaa hilo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Goerge Masaju kwa maono yao ya kuendelea kuboresha miundombinu ya Mahakama ya Tanzania, Pia aliwaomba na kuwahimiza wananchi wa Kanga na Songwe kwa ujumla kuilinda na kuitunza miundombinu ya Mahakama kwa sababu imejengwa ili kusogeza huduma ya upatikanaji wa haki katika maeneo yao.

Vilevile, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga alipongeza uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga na alishukuru kwa ushirikiano alioupata wakati Mkoa wa Songwe ulivokuwa ukipata huduma kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, pia alipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kusogeza huduma ya Makama Kuu na Mahakama ya Rufani kwa kuanzisha Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe.

Naye, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata alieleza kuwa, Mahakama ya Mwanzo Kanga imejengwa ili kusogeza huduma ya utoaji wa haki katika Kata ya Kanga na maeneo ya jirani pia aliwataarifu wananchi kwamba, huduma za Mahakama kuanzia ngazi ya Mahakama ya Mwanzo, Mahakama ya Wilaya, Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani zinatolewa na kupatikana ndani ya Mkoa wa Songwe.

Mhe. Malata alisisitiza kwamba, wananchi wote wanawajibika kulinda na kutunza miundombinu ya Mahakama kwa sababu ni mali ya umma na imejengwa kwa kodi za wananchi, pia Mhe. Malata aliwapongeza wananchi wa Kanga kwa kusimama kidete kuitunza na kuilinda Mahakama ya Kanga ilipotaka kuchomwa moto mwezi Oktoba mwaka jana.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (katikati) akiwa katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga, wengine (wa kwanza kulia) ni Mkuu wa Wilaya ya Songwe Mhe. Fadhili Nkurlu, (wa pili kulia) ni Mkuu wa Mkoa wa Songwe Mhe. Jabiri Omari Makame, (wa nne kutoka kulia) ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga na (wa tano kulia) ni Diwani wa Kata ya Kanga Bw. Prosper Laurent Nkinga.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa kamati ya ulinzi na usalama Mkoa wa Songwe mara baada ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata akipanda mti wa kivuli katika viunga vya Mahakama ya Mwazo Kanga baada ya uzinduzi wa Mahakama hiyo.

Sehemu ya wageni waalikwa waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (wa kwanza kushoto), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kushoto), Mkuu wa Mkoa wa Songwe Mhe. Jabiri Makame (wa tatu kushoto), Mkuu wa Wilaya ya Songwe Mhe. Fadhili Nkurlu (wanne kushoto) na Katibu wa Mhe. Mbunge wa Jimbo la Songwe Bw. Agapto Kilongosi katika zoezi la kukata utepe kuashiria uzinduzi wa Mahakama hiyo Mwanzo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata akihotubia wakati wa uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga akitoa neno katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Bw. Sostenes January Mayoka akifurahia jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde akitoa neno la ukaribisho katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni