Jumatatu, 8 Juni 2026

RC KATAVI AWAHIMIZA TANESCO KUTATUA CHANGAMOTO YA UMEME KWENYE JENGO LA IJC

Na. ALLY RAMADHANI – Mahakama, Katavi

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko hivi karibuni alifanya ziara ya kutembele Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi katika ziara hiyo amefanikiwa kutembelea mradi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC).

Katika ziara hiyo Mhe. Mkuu wa Mkoa amefanikiwa kubaini changamoto ya umeme inayolitesa jengo hilo la Mahakama, huku akitioa maelekezo kwa Meneja wa TANESCO Mkoa wa Katavi kwa kumpatia masaa 48 (siku mbili) wawe wametatua changamoto hiyo.

“Changamoto hii ya umeme katika jengo la Mahakama yetu sifurahishwi nayo, hivyo basi nampatia siku mbili Meneja wa TANESCO Mkoa tatizo hili la umeme katika jengo letu la Mahakama liwe limepatiwa jawabu,” alisema Mhe. Mwanamvua Mrindoko

Aidha, kupitia ziara hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya, amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Katavi kwa kusema “Tunatambua mchango wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi kwa kufatilia upatikanaji wa eneo hili na leo unakuja kutembelea jengo likiwa limekamilika tunashukuru sana na nikupongeze kwa hilo”.

Hata hivyo, Mhe. Isaya amemuomba Mkuu wa Mkoa swala la kupatiwa maeneo kwa ajili ya uanzishwaji wa Mahakama za Mwanzo kutokana na jiografia ya Katavi ili huduma za utoaji haki zisogezwe karibu na wananchi.

Pia Jaji Mfawidhi hiyo, alisema kuwa, Mahakama ya Tanzania inasisitiza Utoaji Haki kwa wakati mapema ipasavyo, hivyo basi Mahakama ya Tanzania inatekeleza mpango huo kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi kwa kujenga miundombinu bora.

Kupitia ziara hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Katavi amewatangazia wananchi wa Katavi kuwa huduma za Mahakama Kuu zimeanza mkoani hapo tangu tarehe 30 Machi, 2026, hivyo wananchi wasisumbuke kwenda Sumbawanga kwa kufuata huduma za Mahakama Kuu wakati Katavi wanatoa huduma hizo.

Mkuu wa mkoa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko (Katikati Mwenye nguo nyeupe alievaa shungi), wa Kwanza kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Katavi Mhe Godfrey Ntemi Isaya, na Wakwanza kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Mhe. Bi Jamila Yusuph Kimaro wakiwa kwenye picha ya Pamoja na baadhi ya watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Katavi katika ziara ya Mkuu wa Mkoa Katavi.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Katavi bi. Silivia Lushasi akielezea juu ya uwepo wa ofisi za wadau wa Mahakama ndani ya jengo la IJC katika ziara ya Mkuu wa Mkoa Katavi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo Katavi, Mhe Godfrey Ntemi Isaya akitoa taarifa fupi wakati wa ziara ya mkuu wa mkoa Katavi.  

Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mhe Mwanamvua Mrindoko akisalimiana na watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Katavi wakati wa ziara yake alipotembelea Mahakama kuu Katavi.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mhe Mwanamvua Mrindoko (wa pili kutoka kushoto) akitoa maagizo juu kutatuliwa kwa changamoto ya umeme katika jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Katavi.

(Habari hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni