Jumanne, 9 Juni 2026

JAJI MWENDA AWASISITIZA MAJAJI, MAHAKIMU SINGIDA KUZINGATIA MATUMIZI YA TEHAMA

Na EVA LESHANGE, Mahakama-Singida

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda amewasisitiza Wajumbe wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Singida kuzingatia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ikiwa ni jitihada za kupunguza matumizi ya karatasi.

Akifungua mkutano wa Chama hicho hivi karibuni uliofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Mahakama Kuu Singida, Mhe. Mwenda alisema, “nasisitiza kuendelea kutumia TEHAMA kwenye shughuli zetu za kila siku ikiwemo kusikiliza mashauri, maandalizi ya nakala za hukumu, mienendo ya kesi na shughuli nyingine.”

Vilevile, aliwaeleza wajumbe kuwa, jumla ya watumishi 25 wa kada mbalimbali kutoka Mahakama Kuu hadi Mahakama za Mwanzo Singida, walikwenda Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Geita kujifunza kuhusu matumizi ya TEHAMA katika shughuli mbalimbali za kimahakama na kwamba, zoezi hilo ni endelevu na linaenda sambamba na ununuzi wa vifaa vyenye uwezo kwa kushirikiana na Menejimenti.

Amesema, hatua hiyo ni katika kuhakikisha matumizi ya karatasi yanapungua kwa kiasi kikubwa ili kuendana na kasi ya teknolojia.

Aidha, katika kikao hicho aliwasisitiza wajumbe hao wa TMJA kufanya kazi kwa ushirikiano na watumishi wa kada nyingine ili kufikia malengo ya Taasisi.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi huyo amewasisitiza Mahakimu wafawidhi wa Wilaya kusimamia watumishi walio chini yao ili kuendelea kuwa na nidhamu nzuri kazini na hata nje ya mazingira ya kazi.

Akihitimisha mkutano huo, Mhe. Mwenda amewasisitiza Mahakimu kuviishi viapo vyao vya kazi na kuwajibika ipasavyo kufanya kazi kwa mujibu wa kanuni na taratibu na kuendelea kusimamia maelekezo yote yanayotolewa na viongozi pasipo kuogopa kukosolewa kwani kiongozi mzuri ni yule ambaye anakubali kukosolewa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda (aliyesimama) akizungumza na wajumbe (hawapo katika picha) katika ufunguzi wa Mkutano wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Singida. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Nenelwa Mwihambi na kulia ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi.


Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida na Naibu Msajili Mteule, Mhe Allu Nzowa (wa kwanza kulia ) pamoja na wajumbe wengine wa TMJA Singida wakiwa katika mkutano wa Chama hicho. Anayefuata ni Mhe. Fadhili Luvinga, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Singida, akifuatiwa na Mhe. Aloyce Masua, Hakimu Mahakama ya Wilaya Singida, akifuatiwa na Mhe. Luzango Khamsini, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Iramba, akifuatiwa na Mhe. Alisile  Mwankejela, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Manyoni na Mhe. Egdius Byabajuka, Hakimu Mkazi Mahakama ya Mwanzo Shelui.

 Sehemu ya Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kutoka Vituo mbalimbali vya Mkoa wa Singida waliohudhuria katika Mkutano huo.

 Sehemu ya wajumbe wa Mkutano huo wakifuatilia kwa umakini kilichokuwa kikijiri.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni