Jumatano, 10 Juni 2026

JAJI MFAWIDHI WA ZAMANI TANGA AAGWA

Na MUSSA MWINJUMA -Mahakama Kuu Tanga

Jaji Mfawidhi zamani wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Tanga, Mhe. Katarina Mteule, jana tarehe 9 Juni, 2026, aliagwa na Watumishi wa Mahakama na Wadau baada ya kupata uhamisho kwenda Mtwara kuendelea na wadhifa huo.

Hafla hiyo fupi ilifanyika ndani ya ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Tanga. Mhe Mteule amehudumu Tanga kwa muda wa miaka mitatu. Nafasi yake imechukuliwa na Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Abdallah Gonzi.

Wakati wa hafla hiyo, Jaji wa Mahakama Kuu Tanga, Mhe. Messe Chaba alisoma risala ya kumuaga Jaji Mteule kwa niaba ya  watumishi wote na kumshukuru kwa mchango wake mkubwa katika utoaji haki.

 “Tunakushukuru kwa kuimarisha kasi ya usikilizaji wa mashauri pamoja na matumizi ya TEHAMA na kuweka msukumo mkubwa kwenye haki jinai na madai, uwepo wa Wadau kama Polisi, TAKUKURU, Uhamiaji, Magereza na wengine katika hafla hii inaonesha mahusiano bora na madhubuti yaliyopo baina yetu,” alisema Mhe. Chaba.

Akimkaribisha Jaji Gonz,i Mhe. Chaba alisema, “Tunakukaribisha sio kama mgeni bali, kama sehemu ya timu ya Mahakama Tanga na tunasonga mbele, tunaamini uzoefu, maarifa na utaalamu wako katika masuala ya sheria utaleta tija.”

Aliwaasa Watumishi kuwa na nidhamu, bidii na mshikamano wa kweli katika utendaji kazi ili kufikia malengo ambayo Taasisi inayatarajia.

Kwa upande wake, Mhe. Mteule alimpongeza Jaji Gonzi kwa uteuzi na kuwashukuru Watumishi na Wadau kwa ushirikiano waliompatia katika kipindi chote alichohudumu kama Jaji Mfawidhi.

“Mlinivumilia pale nilipokosea na kunishauri pale ilipohitajika, kwakweli namshukuru Mungu kwa kila jambo. Wakati mwingine kukaa sehemu moja kwa muda mrefu inaweza kusababisha kukosa ubunifu, hivyo kwangu jambo hili ni jema kwakua nakwenda kupata changamoto mpya,” alisema.

“Mhe. Gonzi, nakukabidhi Wadau hawa, ushirikiano wao na Mahakama ni dhabiti na imara kwelikweli, nakosa neno la kusema juu yao, ni matumaini yangu ushirikiano huu utaimarika zaidi,” alisisitza Jaji Mteule.

Naye Mhe. Gonzi, akizungumza kwenye hafla hiyo, alisisitiza juu ya utendaji kazi kwa kufuata misingi na taratibu za kazi. Alikemea vikali masuala ya uzembe na kutowajibika kazini.

“Mahakama Kuu Tanga ni sehemu ya Mahakama Kuu ya Tanzania, sasa haiwezekani wengine wanakimbia, sisi tunatembea, maana yake tutakuwa tunadumaza juhudi za wenzetu kwa kuwashika shati. Binafsi siwezi kuvumilia uzembe, lazima tufanye kazi kwa bidii ili tusonge mbele kwa pamoja, ” alisema Jaji Gonzi.

Alisisitiza pia juu ya kuzingatiwa kwa haki na maslahi ya Watumishi na uwajibikaji wa kila mtu katika eneo lake la kazi.



Jaji Katarina Mteule (kulia) akimkabidhi ofisi Jaji Abdallah Gonzi, mbele ya Watumishi na Wadau wa Mahakama.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Hudi Majid Hudi akiongoza hafla ya kumuaga Jaji Katarina Mteule anayehamia Mahakama Kuu Mtwara.

Jaji Abdallah Gonzi (kushoto), Jaji Katarina Mteule na kulia ni Jaji Messe  Chaba wakiwa katika hafla ya kumuaga Jaji Katarina Mteule anayehamia Mahakama Kuu Mtwara.

Jaji Mese Chaba akisoma risala ya kumuaga Jaji Katarina Mteule kwa niaba ya Watumishi. 

Jaji Katarina Mteule akiwaaga Watumishi katika hafla ya kumuaga.

Jaji Abdallah Gonzi akitoa neno la shukrani katika hafla hiyo.

Jaji Messe Chaba akikabidhi zawadi kwa Jaji Katarina Mteule kwa niaba ya Watumishi. Anayeangalia ni Jaji Gonzi.

Watumishi na Wadau mbalimbali waliohudhuria katika hafla hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni